Business
Wafanyabiashara Wakosoa KRA Kuhusu Ushuru wa Juu na Huduma Duni

Baadhi ya wafanyibiashara mjini Malindi kaunti ya Kilifi wanalalamikia kupanda kwa gharama ya maisha sawa na ushuru wa biashara wakati mamlaka ya ukusanyaji ushuru nchini, KRA ikitangaza ongezeko la ukusanyaji wa ushuru kwa asilimia 6.8 katika mwaka wa kifedha 2024/2025.
Wakiongozwa na Kenza Ondiek wafanyibiashara hao wanasema kuwa ongezeko la ushuru nchini limeathiri pakubwa ustawi wa biashara huku uboreshaji wa miundomsingi ukiwa katika viwango vya chini.
Ondiek ameiomba serikali kuhakikisha kuwa inaboresha maisha ya wananchi kupitia mapato ya ushuru hasa baada ya mamlaka ya KRA kukusanya jumla ya shilingi trilioni 2.61 katika mwaka wa kifedha 2024/2025 ikilinganishwa na trilioni 2.40 za mwaka kifedha 2023/2024.
Ondiek aidha ameiomba serikali kuwajibikia kikamilifu matumizi bora ya fedha za ushuru zinazokusanywa nchini ili kubadilisha maisha ya wananchi badala ya kuangazia njia za kuongeza kiwango cha makato ya ushuru pekee kwa wananchi.
Haya yanajiri huku mamlaka ya KRA pia ikifichua kupitisha makadirio yake ya ukusanyaji wa ushuru kutoka kwa shilingi trilioni 2.56 hadi shilingi trilioni 2.61 kwa mwaka wa kifedha 2024/2025.
Business
Bei ya vitunguu katika masoko ya humu nchini kuongezeka

Bei ya Vitunguu katika masoko ya humu nchini huenda ikaongezeka hata zaidi kufuatia uhaba wa bidhaa hiyo.
Kufuatia hatua hiyo wafanyibiashara wa vitunguu humu nchini wamelazimika kuagiza bidhaa hiyo kutoka taifa jirani la Tanzania kufuatia kupanda kwa bei ya bidhaa hiyo.
Wakizungumza na vyombo vya habari, Wafanyibiashara hao walisema kuna uhaba mkubwa wa vitunguu jambo ambalo limefanya bei kupanda.
Kulingana na wakulima wa zao hilo, hawakupanda vitunguu kutakana na gharama ya juu ya mbegu pamoja na changamoto za mabadiliko ya hali ya anga.
Aidha walisema kuwa gharama ya Kilimo cha vitunguu imekuwa juu ikilinganishwa na mapato ya chini na ukosefu wa bei nzuri sokoni.
Taarifa ya Pauline Mwango
Business
KEMFRI kuanzisha mradi maalum wa kuzalisha mbegu za samaki

Taasisi ya utafiti wa bahari na uvuvi nchini, KEMFRI, imeanzisha mradi maalum wa kuzalisha mbegu za samaki, ili kuongeza upatikanaji wao na kuinua sekta ya uvuvi nchini.
Akizungumza jijini Mombasa, kaimu mkurugenzi mkuu wa KEMFRI, Dkt. James Mwaluma, alisema kuwa mradi huo unatekelezwa katika eneo la Shimoni kaunti ya Kwale na unalenga kuzalisha samaki wa thamani kubwa kama vile kamba, matiko, na aina nyingine ambazo upatikanaji wake ni nadra.
Dkt. Mwaluma alisema kuwa mbegu zitakazozalishwa kupitia mradi huo zitasambazwa kwa vikundi vya vijana na wanawake wanaojihusisha na shughuli za ufugaji wa samaki, ili kuwawezesha kujitegemea kiuchumi.
Aidha, aliwahimiza vijana kote nchini wakumbatie fursa zilizopo kwenye uchumi wa baharini akisema ni njia mojawapo ya kujikwamua kimaisha na kupambana na ukosefu wa ajira.
Taarifa ya Pauline Mwango