Business
Wafanyabiashara Kilifi Walalamikia Ubomozi wa Vibanda Kupisha Ujenzi wa Barabara

Wafanyabiashara katika eneo la Misufini kuelekea Kwa Mwango, mjini Kilifi, wameelezea hofu yao kuhusu hatma ya biashara zao kufuatia tangazo la serikali ya kaunti ya Kilifi la kubomoa vibanda katika eneo hilo ili kupisha ujenzi wa barabara mpya.
Wakiongozwa na Isaac Thomas, mfanyabiashara wa bidhaa za rehani, wamesema kuwa mpango huo wa ubomoaji utasababisha hasara kubwa kwao, hasa kupoteza wateja wa kudumu, jambo ambalo linaweza kusambaratisha kabisa biashara zao.
“Biashara hii ndiyo tegemeo langu pekee. Nikiondolewa hapa bila mpango mbadala, nitapoteza wateja wangu na maisha yatakuwa magumu,” alisema Thomas.
Wameiomba serikali ya kaunti kuwapatia eneo mbadala la kufanyia biashara kabla ya kutekeleza zoezi hilo la ubomoaji, wakisisitiza kuwa wengi wao hutegemea biashara hizo kwa riziki ya kila siku.
Kwa mujibu wa taarifa kutoka kwa serikali ya kaunti, barabara inayopangwa kujengwa kutoka Misufini hadi Kibaoni inapita katika kiwanja kinachomilikiwa na Chuo Kikuu cha Pwani, hali inayowalazimu kuondoa miundo mbinu isiyo rasmi ili kuwezesha ujenzi huo.
Wafanyabiashara sasa wanasubiri kauli ya mwisho kutoka kwa mamlaka husika kuhusu mustakabali wao.
Business
Vijana Kaunti ya Tana River Waanzisha Biashara ya Sambusa za Samaki kuinua Uchumi

Vijana katika Kaunti ya Tana River wameanzisha biashara ya upishi wa sambusa za samaki kwa lengo la kujikwamua kiuchumi kwa kutumia rasilimali za baharini.
Wamebuni mbinu ya kipekee ya kuandaa sambusa kwa kutumia samaki wa aina mbalimbali, wakiwemo samaki papa. Mbali na sambusa, vijana hao pia wameweza kuunda bidhaa nyingine za thamani kutokana na samaki, hatua inayochochea ubunifu na kuongeza ajira miongoni mwao.
Kulingana na vijana hao, biashara hiyo inalenga kuongeza kipato chao na kufungua milango ya kuingia katika masoko mapya, ya ndani na hata ya nje ya kaunti.
Hatua hii imesukumwa na changamoto ya uhaba wa soko la samaki katika eneo hilo, hali ambayo husababisha uharibifu wa samaki kutokana na kukosa wanunuzi. Kwa hivyo, ubunifu huu umekuwa suluhisho la kiuchumi na kiteknolojia kwa vijana wa Tana River.
Business
Wafanyabiashara wa Soko la Matano Mane Waililia Serikali ya Kaunti ya Kilifi Kuwajengea Choo

Wafanyabiashara katika soko la Matano Mane, eneo la Vitengeni, Kaunti ya Kilifi, wameitaka serikali ya kaunti hiyo kuwajengea choo, wakisema ukosefu wa huduma hiyo muhimu umekuwa kero kubwa inayozorotesha shughuli za biashara.
Wakiongozwa na Phelisia Mageshi, wafanyabiashara hao wamesema kuwa hali ya sasa imesababisha baadhi yao kuhamishia biashara zao nje ya soko hilo, kutokana na mazingira yasiyofaa kwa shughuli za kila siku.
Bi Mageshi ameeleza kuwa licha ya serikali ya kaunti kufahamishwa kuhusu changamoto hiyo mara kadhaa, hakuna hatua yoyote iliyochukuliwa hadi sasa, hali inayowafanya kuhisi kusahaulika.
Wameitaka serikali ya kaunti kuingilia kati kwa haraka ili kuboresha mazingira ya kufanyia biashara na kuhakikisha afya ya wananchi inalindwa.