Business
Wadau wa utalii Watamu waunga mkono ada za maegesho mbugani

Wadau wa sekta ya Utalii eneo la Watamu kaunti ya Kilifi wameunga mkono pendekezo la shirika la huduma kwa wanyamapori nchini KWS la kutathmini upya ada za kuegesha magari mbugani.
Wadau hao walitoa shinikizo kuwa mabadiliko hayo yaainishwe na huduma zilizoboreshwa vile vile matokeo ya uhifadhi mbugani.
Wakizungumza wakati wa kikao cha kubadilishama maoni kuhusu suala hilo mjini Watamu, Patrick Changawa, mmoja wa wahudumu wa safari za kitalii, alisistiza kuhusu mchango muhimu unaotolewa na sekta ya utalii katika uchumi wa taifa.
Alipongeza KWS kwa kushirikisha wahusika wamaeneo hayo katika mchakato wa mashauriano.
“KWS imetuhamasisha kuhusu namna ada za uhifadhi zilizofanyiwa ukarabati zitakavyoanza kutekelezwa, mgao mkubwa wa fedha utatumika katika kuimarisha mbuga za baharini kupitia urejeshaji wa miamba ya matumbawe, udhibiti wa uchafuzi wa mazingira, na programu za kufikia jamii,” alisema Changawa.
Mkurugenzi msaidizi wa eneo la hifadhi ya pwani katika KWS Elema Hapicha alibainisha kuwa vikao sawa vya ushirikishwaji wa umma vinafanyika nchini kote ili kukusanya maoni kutoka kwa wadau.
“Wadau wa Watamu wametoa maoni muhimu kuhusu rasimu ya muundo wa ada ya uhifadhi,” Hapicha alisema.
Mapendekezo hayo yamejikita katika rasimu ya kanuni za uhifadhi na usimamizi wa wanyamapori (Ada ya Ufikiaji na Uhifadhi) za 2025.
Taarifa ya Joseph Jira
Business
Mradi wa kiuchumi wa Dongo Kundu wavutia wawekezaji zaidi

Wawekezaji wa ndani na nje ya nchi wanaendelea kuonyesha nia ya kuekeza katika mradi wa kiuchumi wa dongo kundu kaunti ya Mombasa.
Mradi huo unaotarajiwa kuongeza uzalishaji katika viwanda na thamani ya bidhaa ndani ya nchi na nje, unatarajiwa kukamilika hivi karibuni.
Kampuni ya nishati kutoka China, Ruike Energy Group Limited, ni mwekezaji wa hivi karibuni kuonyesha nia ya kupata nafasi ndani ya eneo hilo la kiuchumi la Dongo Kundu kwa ajili ya kuanzisha kiwanda cha kusafisha mafuta.
Kulingana na halmashauri ya bandari nchini KPA hatua hiyo italeta faida Zaidi ikiwemo kubuni nafasi za ajira, ikuaji wa uchumi, upatikanaji wa vifaa vya baharini, na urahisi wa kufikia masoko ya kanda na ya kimataifa.
Taarifa ya Pauline Mwango
Business
KETRACO kuimarisha usalama wa chakula nchini

Shirika la usambazaji umeme nchini, KETRACO, limethibitisha dhamira yake ya kuimarisha usalama wa chakula, ukuaji wa kijani, na ushirikiano wa kieneo kupitia uekezaji mkubwa katika miundombinu ya umeme.
Katika maonesho ya Kimataifa ya kilimo ASK yanayoendelea kaunti ya Mombasa, KETRACO imeonyesha jinsi miundombinu yake ya umeme inavyowezesha kilimo cha kisasa na uzalishaji wa viwandani.
Kwa mujibu wa kaimu mkurugenzi mkuu, mhandisi Kipkemoi Kibias, KETRACO imekamilisha miradi 43 ya njia za kusafirisha umeme, huku mingine 29 ikitarajiwa kukamilika ifikapo mwaka 2028.
Kibias, alisema shirika hilo tayari limejenga zaidi ya kilomita elfu sita za njia za umeme wa msongo mkubwa, likiwa pia na vituo 46 vya kusambaza umeme na upanuzi wa mitambo 33.
Katika eneo la Pwani, Kibias alisema upanuzi wa mpango wa Green Energy Backbone umewezesha usambazaji wa kawi safi kwa asilimia 93, jambo lililopunguza utegemezi wa mafuta na kuchochea maendeleo ya biashara za kilimo, utalii na uchumi wa baharini.
Kibias alisema KETRACO inaendelea kuwekeza katika teknolojia za kisasa na kuunganisha Kenya na nchi jirani kupitia njia za kimataifa kama zile za Ethiopia, Tanzania na Uganda hatua zitakazowezesha biashara ya umeme Afrika Mashariki.
Taarifa ya Mwanahabari wetu