News
Tahadhari Yatolewa Kuhusu Mvua Kubwa

Idara ya utabiri wa hali ya hewa nchini imetoa tahadhari kwa wakenya kuhusu mvua kubwa itakayonyesha katika maeneo mbalimbali ya nchi kwa kipindi cha siku saba.
Mkurugenzi wa idara ya hali ya hewa nchini, Dkt David Gikungu, amesema mvua hiyo itakayoambatana na ngurumo za radi inatarajiwa wakati wa alasiri na usiku, huku baadhi ya maeneo yakitarajiwa kupata mvua chache asubuhi kabla ya hali ya jua kuchomoza kwa muda mfupi.
Idara hiyo imesema viwango vya joto usiku katika maeneo haya vitashuka hadi chini ya nyuzi joto 9, hali inayoweza kuathiri watoto, wazee, na wagonjwa.
Kaunti za Siaya, Kisumu, Homa Bay, Migori, Kisii, Nyamira, Trans Nzoia, Baringo, Uasin Gishu, Elgeyo-Marakwet, Nandi, Nakuru, Narok, Kericho, Bomet, Kakamega, Vihiga, Bungoma, Busia, na Pokot Magharibi pia zimeorodhesha kati ya ya maeneo yanayotarajiwa kupokea mvua nyingi.
Hali kama hiyo inatarajiwa katika kaunti za Kitui, Makueni, Machakos, Kajiado, Taita Taveta, na sehemu za Tana River, ambako asubuhi kutakuwa na mawingu na mvua nyepesi kabla ya hali ya mvua kubwa kuanza alasiri na kuendelea hadi usiku.
Wakati mvua ikinyesha maeneo mengi ya kaunti za Mombasa, Kilifi, Lamu, Kwale, Marsabit, Mandera, Wajir, Garissa, na Isiolo yametabiriwa kupata joto nyakati za mchana hadi kufikia nyuzi joto 33.
Wataalamu wa hali ya hewa wamewahimiza wananchi kuwa waangalifu na kufuata ushauri wa serikali, hasa wale wanaoishi maeneo yenye historia ya mafuriko, maporomoko ya ardhi, na miundombinu dhaifu.
News
Alubbe: Tutazuru kaunti za Pwani kushughulikia suala tata la ardhi

Mkurugenzi mkuu wa shirika la utetezi wa haki za ardhi nchini Kenya Land Alliance Faith Alubbe amesema wameanzisha mchakato wa kuzuru kaunti zote 6 za pwani kuangazia suala tata la mizozo ya ardhi.
Akizungumza mjini Kilifi, Alubbe alisema kwamba ukanda wa Pwani ni mojawapo ya maeneo humu nchini ambayo yamesheheni dhulma za kihistoria kwenye masuala ya umiliki wa ardhi.
Alubbe ambaye pia ni Wakili wa masuala ya ardhi alihoji kwamba mikakati yao katika mchakato huu ni kuhakikisha kuwa wapwani wanaelewa kwa kina haki zao kuhusiana na umiliki wa ardhi za kibinafsi lakini pia za kijamii.
“Kuna hazina ya ardhi ambayo ilibuniwa baada ya mswada kuhusiana na hazina hiyo kupitishwa. Rais William Ruto tayari aliwekeza fedha kwenye hazina hiyo ila idadi kubwa ya wakaazi wa pwani hawana ufahamu kuhusu hazina hiyo” alisema Alubbe.
Alubbe alisema kuwa watahakikisha kuwa wapwani wanapata hamasa za kutosha kuhusiana na suala hilo lakini pia haki zao za ardhi kwa jumla.
“Inaweza kuwa muhimu watu wa pwani kuambiwa kuhusu hii hazina, ili wakapate kuelewa ni vipi hazina hizi zinawahusu”, aliongeza Alubbe.
Taarifa ya Hamis Kombe
News
Chahale, aishutumu serikali kutokana na dhulma za kijinsia

Mkurugenzi mkuu wa Shirika la kutetezi haki za kibinadamu la International Justice Mission, IJM, Vincent Chahale ameishutumu serikali kwa kuzembea katika kukabiliana na dhulma dhidi ya wasichana na wanawake nchini.
Chahale alisema kwamba wasichana wadogo wamekuwa wakidhulumiwa kingono na wengi wao huishia kukosa haki.
Alirejelea kisa ambapo msichana wa umri wa miaka 17 kwa jina Farida Julius Changawa aliyeuawa kinyama kwa kudungwa kesu eneo la Msumarini kaunti ya Kilifi ambali alisema ni sharti serikali iwe ange katika kuhakikisha kwamba wasichana wanalindwa dhidi ya dhulma katika jamii.
“Kuna pengo katika jamii yetu ambapo wasichana wadogo wanaendelea kudhulumiwa bila kupata haki. Kesi kama ya Farida ni kesi ya kusikitisha sana na tutaifuatilia hadi pale familia yake itakapopata haki” alisema Chahale.
Akiunga mkono kauli hiyo, Aggrey Juma meneja msimamizi wa Shirika la international Justice Mission alisema serikali inapaswa kutilia mkazo suala la dhulma dhidi ya Wanawake akieleza kusikitishwa na mauaji ya kinyama aliyotekelezewa marehemu Farida Julius.
Wawili hawa waliyasema haya wakati wa mazishi ya mwendazake Farida yaliyofanyika eneo la Mavueni siku Jumamosi ya tarehe ya 21 mwezi Juni 2025.
Farida alipitia dhulma ya kubakwa akiwa na umri wa miaka 13 kudhulimiwa tena miaka minne baadaye ambapo aliishia kuuawa kwa kudungwa kisu hivi majuzi.
Marehemu aliacha mtoto mmoja wa kiume mwenye umri wa miezi 9.
Taarifa ya Hamis Kombe