Klabu ya Arsenal kiliendeleza harakati zao za kuwania ubingwa wa Premier League baada ya kuibuka na ushindi muhimu wa mabao 2-1 dhidi ya Chelsea waliobaki na wachezaji 10 katika dabi ya London iliyochezwa Jumapili.
Mchezo huo uliochezwa katika Emirates Stadium uliangazia umuhimu wa mipira ya adhabu (set-pieces), huku mabao yote yakitokana na mipira ya kona. Kikosi cha kocha Mikel Arteta kilifunga mabao mawili kupitia kona na pia kuruhusu bao kwa njia hiyo hiyo.
William Saliba aliipa Arsenal uongozi katika kipindi cha kwanza kwa bao lake la kwanza tangu Desemba 2024, akimalizia mpira uliotokana na kona ya Bukayo Saka. Hata hivyo, Chelsea walisawazisha muda mfupi kabla ya mapumziko baada ya Piero Hincapie kujifunga kufuatia kona kali ya Reece James.
Kipindi cha pili, Jurrien Timber aliibuka shujaa kwa kufunga bao la ushindi kwa kichwa dakika ya 66 akimalizia kona ya Declan Rice. Licha ya malalamiko ya wachezaji wa Chelsea wakidai kulikuwa na madhambi kwa kipa wao, bao hilo lilikubaliwa.
Huo ulikuwa ni ushindi wa pili mfululizo kwa Arsenal na umewarejeshea uongozi wa pointi tano dhidi ya Manchester City, ambao wana mchezo mkononi.
Chelsea walipata pigo jingine dakika ya 70 wakati winga Pedro Neto alipotolewa nje kwa kadi ya pili ya njano baada ya kumchezea vibaya Gabriel Martinelli.
Hata hivyo, Arsenal walihitaji uokozi wa hali ya juu wa kipa David Raya katika dakika za nyongeza kuzuia shuti la Alejandro Garnacho kabla ya kusherehekea ushindi huo muhimu.
Ushindi huo unaifanya Arsenal kuendelea kujiimarisha kileleni huku Chelsea wakipata pigo katika mbio zao za kutafuta nafasi ya kushiriki Ligi ya Mabingwa Ulaya msimu ujao.
