National News
Shahidi wa 28 na 29 Waelezea Mahakama Masaibu Waliyopitia Shakahola

Kesi inayomhusu Mhubiri tata Paul Mackenzie na wenzake 92 imesikizwa katika Mahakama ya Mombasa, ambapo shahidi wa 28 na 29 wameeleza ushahidi wao Mahakamani.
Shahidi wa 28, ambaye ni mtoto ametoa ushahidi wake katika chumba cha faraga ambapo amesema kwamba alikamatwa na maafisa wa polisi pamoja na familia yake baada ya wazazi wake kuwaachisha shule kutokana na mafunzo ya Mackenzie.
Mtoto huyo ameeleza kwamba baba yake alikuwa akipinga mafunzo ya Mackenzie lakini baadaye alijiunga na kisha kuhamia Shakahola na familia yake ambapo alishuhudia Mackenzie akikusanya watu na kuwaagiza kufunga kula na kunywa, kabla ya kufanikiwa kutoroka hadi kituo cha watoto huko Watamu.
Kwa upande wake Shahidi wa 29, ameiambia Mahakama hiyo kwamba alipoteza watoto wake 7 kutokana na kufunga kula na kunywa, akisema walinzi waliokuwa wakilinda eneo hilo walichukua chakula chake chote kilichokuwa nyumbani kwao.
Shahidi huyo amesema wakati huo alikuwa mjamzito na alilazimika kufunga ili kuua mtoto aliyekuwa tumboni na wafuasi wa Mackenzie walikuwa hawaruhusiwi kuomboleza kifo chochote katika eneo hilo la Shakahola.
Mackenzie na wenzake 92 wanakabiliwa na mashtaka 238 ikiwemo mauaji ya halaiki, ugaidi, mafunzo ya itikadi kali miongoni mwa mashtaka mengine yanayodaiwa kuyatekeleza kati ya mwaka 2020 na 2023 katika msitu wa Shakahola kaunti ya Kilifi.
Kesi hiyo inaendelea kusikilizwa mbele ya Hakimu mkuu Alex Ithuku.
National News
Chonga: Wakenya Wanaosafiri Ughaibuni Kusaka Ajira Hawazingatii Sheria za Leba

Mwenyekiti wa kamati ya Leba katika bunge la kitaifa Ken Chonga amesema baadhi ya wakenya ambao wanasafiri katika mataifa ya miliki za kiarabu kusaka ajira wamekosa kuzingatia sheria za Wizara ya Leba nchini na kuangukia mikononi mwa walaghai.
Chonga amesema ni lazima wakenya hao wachunguze mawakala wanaowasafirisha katika mataifa hayo kama wanatambulika na serikali, ndipo waingie katika mikataba ya uajiri ambayo imezingatia sheria za Leba nchini.
Akizungumza na Wanahabari mjini Kilifi, Chonga ambaye pia ni Mbunge wa Kilifi Kusini amesema ili wakenya waepuke madhila mbalimbali kutoka kwa waajiri wao katika mataifa hayo ni lazima wasafirishwe na mawakala waliosajiliwa na serikali.
Wakati huo huo amesema japo serikali iko mbioni kuhakikisha inawatafutia wakenya kazi katika mataifa ya ughaibuni ni lazima wanaosaka ajira za ughaibuni waingie katika mkataba wa uajiri kabla ya kusafiri nje ya nchi.
National News
Chibule: Visa vya Dhulma za Kijinsi Vimepungua Kilifi

Serikali ya kaunti ya Kilifi imesema visa vya dhulma za kijinsia katika kaunti hiyo vimepungua kwa kiwango kikubwa.
Kulingana na Naibu Gavana wa kaunti hiyo Flora Mbetsa Chibule, visa hivyo viliongezeka zaidi msimu wa maambukizi ya virusi vya Corona, ambapo kaunti ya Kilifi iliorodheswa nafasi ya tatu nchini baada ya kaunti ya Bungoma na Samburu.
Chibule amesema kwa sasa ni asilimia 12.3 pekee ya visa hivyo vilivyoripotiwa tofauti na asilimia 30 wakati wa maambukizi ya Corona, akisisitiza kwamba juhudi hizo zimefanikiwa kupitia ushirikiano wa jamii na wadau mbalimbali.
Kiongozi huyo amedokeza kwamba serikali ya kaunti imetoa mafunzo kwa maafisa wa kutoa ushauri nasaha ili kusaidia kupambana na visa hivyo mashinani, akisema juhudi hizo zitaendelezwa sawa na kudhibiti madhila hayo.
Wakati uo huo ameweka wazi kwamba kaunti hiyo imekamilisha ujenzi wa sehemu salama ya kuwahifadhi watoto wanaopitia dhulma za kijinsia wakati kesi zao zikiendelea Mahakamani.