News
Ripoti ya upasuaji:Wakili Mathew Kyalo Mbobu alipigwa risasi mara nane

Ripoti ya upasuaji wa maiti kuhusu kifo cha wakili Mathew Kyalo Mbobu imebaini alipigwa risasi mara nane katika tukio la uvamizi ambalo lilisababisha kifo chake.
Kulingana na mpasuaji mkuu wa serikali Dkt. Johansen Oduor, risasi mbili zimepatikana zikiwa zingali mwilini, moja ikiwa imekwama kwenye uti wa mgongo.
Oduor alidokeza kuwa uvamizi huo ulitekelezwa kwa maksudi na kwa karibu zaidi ambapo risasi nyingi zilimpiga upande wake wa kulia.
Oduor vile vile alifichua kuwa majeraha kwenye sehemu ya shingo na uti wa mgongo yalisababisha uvujaji wa damu nyingi hali iliyochangia kifo.
Awali spika wa bunge la seneti Amason Kingi aligiza asasi za usalama kufanya uchunguzi wa haraka kufuatia kifo cha wakili Mbobu.
Kingi alimtaja mauaji ya wakili huyo kama yakinyama huku akimtaja wakili Mbobu kama mtu jasiri na aliyejitolea kuhudumia raia.
Wakili huyo alifariki baada ya kupigwa risasi jioni siku ya jumanne tarehe 9 Septemba 2025, akiwa katika gari lake kwenye barabara ya Lang’ata.
Taarifa za polisi zilisema mwathiriwa alipigwa risasi na watu waliokuwa kwenye pikipiki muda mfupi baada ya saa moja na nusu usiku.
Ilisemekana wakili huyo alikuwa akiendesha gari kuelekea nyumbani wakati mshambuliaji aliposimamisha pikipiki kando ya gari lake na kufyatua risasi kabla ya kuondoka kwa kasi.
Taarifa ya Joseph Jira
News
IEBC inaendelea kutambua vituo vya kusajili wapiga kura

Maafisa wa tume ya uchaguzi na mipaka nchini IEBC wamesema wanaendelea na zoezi la kutambua sehemu za kuweka vituo vya kusajili wapiga kura hasa maeneo ya mashinani.
Afisa msimamizi wa tume ya IEBC eneo bunge la Ganze kaunti ya Kilifi, Mohammed Bahero Aboud alisema juhudi hizo ni kuhakikisha zoezi la usajili wapiga kura litakaloanza rasmi Septemba 29, mwaka huu linafaulu.
Akizungumza mjini Kilifi, Bahero alisema tume hiyo inatumia mbinu mpya ya kutambua vituo vya jadi vya usajili wapiga kura na kuweka vituo vipya kulingana na mapendekezo ya sheria.
Wakati huo huo alidokeza kwamba tume ya IEBC imekuwa ikihamashisha wakenya kutokubali kushawishiwa na wanasiasa na kujisajili katika maeneo yasiokuwa yao hasa msimu huu ambao zoezi hilo linakaribia kuanza.
Taarifa ya Joseph Jira
News
Kaunti ya Mombasa kukumbatia matumizi ya mfumo wa miale ya jua

Serikali ya kaunti ya Mombasa imesema imeanza kutekeleza mpango wa kutumia nishati mbadala katika vituo vyote vya huduma za kaunti, kwa kuanza na mabadiliko ya mfumo wa taa hadi kutumia umeme wa miale ya jua.
Kwa mujibu wa waziri wa kawi, rasilimali asili na ustahimilivu dhidi ya mabadiliko ya tabianchi kaunti ya Mombasa, Emily Achieng, hatua hii inalenga kupunguza gharama za matumizi ya umeme na kuhimiza matumizi ya nishati safi na rafiki kwa mazingira.
Mbali na hilo, waziri huyo alisema kaunti inaendelea kuweka vifaa maalum vya kupima ubora wa hewa katika maeneo mbalimbali ya mji na ndani ya taasisi za umma.
Lengo ni kupata ushahidi wa kisayansi kuhusu kiwango cha uchafuzi wa hewa, na kuchukuliwa kwa hatua za kisheria kwa wanaokiuka sheria.
Vifaa hivyo tayari vimewekwa katika hospitali ya rufaa ya Coast General na baadhi ya shule ikiwa ni sehemu ya mpango wa muda mrefu wa kaunti, kujenga ustahimilivu dhidi ya madhara ya mabadiliko ya tabianchi.
Mikakati hiyo pia itasaidia kaunti katika kufanya maamuzi kuhusu maeneo yanayofaa kuwekwa biashara fulani, ili kulinda wananchi dhidi ya maradhi yanayosababishwa na uchafuzi wa hewa.
Taarifa ya Mwanahabari wetu.