Entertainment
Diamond Platnumz: Nilishawahi Kuoa, na Kuna Siku Nitawaambia Ikawaje
Kauli ya Diamond Platnumz kuhusu ndoa imewavuruga mashabiki mitandaoni, baada ya picha zenye taswira ya harusi kusambaa. Ingawa hajasema wazi kama ameoa, ujumbe wake wa kina kuhusu kukaa kimya na uvumilivu umeacha maswali mengi kuliko majibu. Je, Diamond ameoa kwa siri? Au ni ujanja wa kisanii?

Kauli ya msanii nyota na mfanyabiashara mashuhuri Diamond Platnumz, iliyoambatanishwa na picha zinazodaiwa kuhusiana na ndoa ya mkeka, imewaacha mashabiki wengi katika hali ya sintofahamu—wengi wakijiuliza iwapo msanii huyo maarufu ameoa au la.
Kupitia chapisho lake katika mitandao ya kijamii, Diamond alieleza kuwa amekuwa akikwepa mahojiano na vyombo vya habari kwa makusudi, akisema kufanya hivyo kumemsaidia kuepuka maneno ya upotoshaji na uzushi kutoka kwa watu.
Akiongea kwa tafakari na kina na kwa hisia, Diamond alisema kuwa kukaa kimya wakati anakumbwa na maneno ya uongo ni jambo linalohitaji ukomavu wa hali ya juu, na kumshukuru Mungu kwa kumpa hekima hiyo:
“Miongoni mwa vitu ambavyo nimejifunza ni ukomavu wa kukaa kimya… Ukomavu huu unahitaji uvumilivu wa hali ya juu, moyo wa subira, na roho ya kukaza pale ambapo mtu au watu wanapokupaka matope kwenye jamii ilhali wewe unajua ukweli, lakini unachagua kukaa kimya. Si jambo jepesi, lakini faida yake ni kubwa – unapambana vita zako kwa msaada wa Mungu, na mwisho wake unakuwa mshindi.”
Hata hivyo, katika ujumbe huo, Diamond hakuthibitisha moja kwa moja kama kweli ameoa, licha ya picha zinazomuonesha akiwa katika mazingira yanayofanana na hafla ya harusi. Kauli yake ya mwisho nayo haikufafanua jambo hilo kikamilifu:
“Anyways: Najua kila mmoja wenu ana picha tofauti kabisa kuhusu Diamond Platnumz na KUOA, ila tu nataka leo niwaambie kuwa HUYU DIAMOND PLATNUMZ ALISHAWAHI KUOA, na kuna siku nitawaambia ikawaje,” aliandika.
Kauli hiyo imeongeza maswali miongoni mwa mashabiki, huku wengine wakichukulia comment ya Juma Jux kama ushahidi wa ndoa hiyo. Jux aliandika:
“Welcome to the team my brother 🤝”
View this post on Instagram
Kumbuka kuwa mwezi huu, Diamond anatarajiwa kutangaza msanii mpya atakayesajiliwa chini ya lebo yake ya muziki WCB Wasafi, kufuatia kuondoka kwa Mbosso mapema mwaka huu.
Baadhi ya Hisia za Mashabiki:
-
Simba_Bhoy: Brother mbona ndoa ya mkeka iyoooo……………….😮
-
Msafitheswagg: HII ITAKUWA NDOTO NGOJA NIENDELEE KULALA
-
Popineshine: Sikuwahi waza kama itatokea hii miaka hii ya karibuni kwa kweli ni surprise..😱 ONGERA SIMBA🫡
-
Kimkayndo: Mimi naondoka na paragraph ya mwisho tajiri
Entertainment
Creative Economy Forum 2025: Ruby Kache Uso kwa Uso na Bien
Ruby Kache na Bien wakutana Nairobi kwenye Jukwaa la Uchumi wa Ubunifu! 🌟

Jiji la Nairobi liling’aa zaidi wiki hii baada ya kuandaa Jukwaa la Uchumi wa Ubunifu — tukio la kipekee lililowakutanisha wabunifu, wanamuziki, na wadau wa sanaa kutoka Kenya na Marekani. Mbali na mijadala ya sera na mipango ya maendeleo, tukio hili lilikutanisha watu mashuhuri.
Mrembo wa redio, Ruby Kache, alikutana na nyota wa muziki, Bien aliyekuwa kwenye kundi la maarufu Sauti Sol!
Kwa wanaosikiliza redio, jina la Ruby Kache si geni. Ni mtangazaji machachari wa kipindi cha “The Wave” kupitia Coco FM, kinachoenda hewani kila Jumamosi kuanzia saa 4 asubuhi hadi saa 7 mchana. Kipindi chake kinajulikana kwa kuangazia maisha ya vijana, muziki wa kisasa, mitindo na mazungumzo yenye msisimko.
Katika kongamano hili, Ruby alihudhuria kama mshiriki, lakini kama ilivyo kawaida yake — aliiba spotlight bila kusema neno jukwaani. Uvaaji wake, tabasamu lake na muingiliano wake na wadau wengine ulitosha kuonyesha uwepo wake wa nguvu.
Moja ya highlights kubwa za siku hii ilikuwa ni wakati Ruby Kache alipokutana na Bien. Ruby alirekodi kipande kifupi na kukipakia kwenye ukurasa wake wa Facebook, huku mashabiki wakishangilia. Bien, nguli wa mziki anayeshikilia tuzo ya muimbaji bora Afrika Mashariki, alikuwa mgeni maarufu katika tukio hilo.
Baadhi ya waunda maudhui maarufu kutoka Pwani waliopamba hafla hiyo ni pamoja na Presenter Kai, Beka Ruga, Mwagwaya Ndani, na Princess Fynick, waliokuja kwa mitoko ya kisasa. Kwa upande wa muziki, Reagan Dandy alikuwa miongoni mwa wanamuziki wachache kutoka Pwani waliobahatika kuhudhuria tukio hilo la hadhi ya kimataifa.
Jukwaa la Uchumi wa Ubunifu limeibuka kama jukwaa muhimu kwa kuvunja mipaka kati ya sanaa, biashara na teknolojia. Kupitia mikutano kama hii, wasanii, waunda maudhui na wadau wa sekta ya ubunifu wanapata nafasi ya kuunganishwa na fursa za kimataifa, kujifunza kuhusu ulinzi wa kazi zao, na kuelewa jinsi ya kujitegemea kiuchumi kupitia vipaji vyao. Kwa kizazi kinachotegemea mitandao na ubunifu kama njia ya kujieleza, majukwaa haya yanakuwa daraja kati ya ndoto na mafanikio halisi.
Kwa washiriki kutoka Pwani na sehemu nyingine za Kenya, kongamano hili halikuwa tu mahali pa kuonekana, bali pa kujifunza, kuunganishwa na kuchochewa kufikiria ubunifu kama ajira na biashara. Uwepo wa majina maarufu kama Ruby Kache, Bien, na waunda maudhui wengine wakubwa ulitoa motisha kwa vijana, huku ikithibitisha kuwa sanaa inaweza kuwa nguvu ya kiuchumi na chombo cha mabadiliko chanya katika jamii.
Entertainment
#UlijanjarukaVipi! Safari ya Mpishi Nguli, Don Moses: Kutoka Kukosa Karo Hadi Kuwa Head Chef

Katika dunia ya leo ambapo changamoto za kiuchumi zimewaacha vijana wengi wakihangaika, simulizi ya Don Moses ni mwanga wa matumaini kwa wengi.
Akiwa mgeni katika kipindi cha Janjaruka 254, kinachorushwa kila siku ya wiki kuanzia Jumatatu hadi Ijumaa, Moses alisimulia safari yake ya ajabu kutoka kwa kijana aliyezuiwa na karo ya shule hadi kuwa mpishi mashuhuri hadi kuwa Head Chef aliyesimamia wapishi waliosomea fani hiyo chuoni.
Baada ya kuhitimu kidato cha nne, Moses alikuwa ameweka ndoto ya kujiunga na chuo lakini maisha yalikuwa na mpango tofauti. Mama yake alipata ajali mbaya, hali iliyolazimu familia kuhamishia raslimali kwenye matibabu badala ya karo yake ya chuo.
“Nilijua wazi kuwa singeweza kulazimisha familia ichague kati ya maisha ya mama na elimu yangu. Ilibidi nitafute njia mbadala,” anasema Moses.
Jiko la YouTube: Darasa la Ukombozi
Akiwa hana karo, lakini akiwa na shauku, Moses alianza kujifunza sanaa ya upishi kupitia video za YouTube. Binamu yake, Moses Gambo, ndiye aliyemfungulia mlango wa maarifa kwa kumtambulisha kwenye tutorials mbalimbali mtandaoni.
Ni ujuzi huo wa mtandaoni uliomfungulia milango ya ajira katika hoteli za kifahari, ambapo aliweza kupanda ngazi hadi kuwa mpishi mkuu (Head Chef) — akiongoza wapishi waliopitia vyuo vya kitaaluma. Ni mafanikio ambayo wengi hawakuyatarajia kutoka kwa kijana ambaye hakuingia darasa la kawaida, bali alikaa mbele ya skrini.
“Najua kwenye upishi kuna kupika mashendea ama kupika chakula kibaya ila sijawahi kufeli. Siku zote mimi ni makini na ratio ya viungo. Ndiyo silaha yangu,” anasema kwa kujiamini.
Mwaka wa Mageuzi: 2020
Kama ilivyokuwa kwa wengi, mwaka wa janga la COVID-19 – 2020 – ndiyo ulikuwa mwaka wa mabadiliko makubwa kwa Moses. Akiwa na muda mwingi na motisha mpya, alianza kupika kibiashara, akihudumia watu waliokuwa majumbani.
“Kabula ya hapo, nilikuwa napika kwa kujifurahisha tu. Lakini corona ilinifungua macho. Nikaanza kuona kuwa mapishi ni biashara yenye nguvu,” anasema Moses.
Karo Iliyogeuka Mtaji
Kipindi fulani baadaye, Moses alipata nafasi ya kujiunga na chuo hatimaye. Lakini kwa mshangao wa wengi, alikataa ofa hiyo kwa hiari na kuomba fedha hizo zitumike kupanua biashara yake ya upishi.
“Nitamudu gharama ya chuo siku moja. Kwa sasa, najenga misingi. Muda wa kusoma utafika,” anasema.
💡 Ushauri kwa Vijana: Anza na Kile Kilicho Mkono Wako
Don Moses sasa ni sauti ya matumaini kwa vijana wengi wanaohisi kuwa elimu ya juu au mtaji mkubwa ndio tiketi pekee ya mafanikio. Anasisitiza umuhimu wa kuanza na huduma, si lazima mtaji.
“Kama huna kazi wala mtaji, toa huduma kwanza. Ukiwa na bidii na ubunifu, malipo yatafuata,” anashauri.
Leo hii, sehemu kubwa ya mapato ya Moses huingia moja kwa moja kwenye ununuzi wa vifaa bora vya upishi, huku akiendeleza ndoto yake ya kuwa mmoja wa wapishi wakubwa zaidi nchini Kenya.