News
Mwandishi wa Vitabu vya Tamthilia Ngugi wa Thiong’o amefariki

Mwandishi nguli wa vitabu vya tamthilia Ngugi wa Thiong’o ameaga dunia akiwa na umri wa miaka 87.
Familia imethibitisha kifo chake kilichotokea siku ya Jumatano Mei 28, 2025 nchini Marekani.
Ngũgĩ wa Thiong’o ni mmoja wa waandishi mashuhuri na wenye ushawishi mkubwa kutoka Afrika, hasa nchini Kenya. Anafahamika sana kwa maandishi yake ya kifasihi, hasa Riwaya, Tamthilia, Insha na tafakari kuhusu Lugha, Siasa, Utamaduni na Ukoloni.
James Ngugi wa Thiong’o, baadaye alijulikana kama Ngũgĩ wa Thiong’o baada ya kuacha jina la Kikristo.
Alizaliwa tarehe 5 Januari 1938 katika kijiji cha Kamĩrĩthũ, eneo la Limuru katika kaunti ya Kiambu.
Ngugi alisoma katika shule ya upili ya Alliance High School – mojawapo ya shule za kitaifa nchini Kenya, kisha akaelekea katika chuo kikuu cha Makerere nchini Uganda na kuhitimu mwaka 1963 na akajiunga na chuo kikuu cha Leeds nchini Uingereza ambako aliendelea na masomo yake ya fasihi.
Ngũgĩ alianza kuandika vitabu katika lugha ya Kiingereza lakini baadaye aliacha kutumia Kiingereza katika kazi zake za fasihi na kuanza kuandika kwa lugha za Kikuyu na Kiswahili, kama njia ya kuendeleza utamaduni na lugha za Kiafrika.
Baadhi ya vitabu vyake maarufu ni pamoja na Weep Not, Child (1964) – riwaya ya kwanza ya Mwafrika kuchapishwa kwa Kiingereza.
Vingine ni pamoja na The River Between (1965), A Grain of Wheat (1967), Petals of Blood (1977), Devil on the Cross (Caitaani Mutharaba-ini, 1980) – aliandika akiwa gerezani, kwenye karatasi za chooni na Matigari (1986) – kitabu hiki kilipigwa marufuku Kenya kwa sababu ya ujumbe wake wa mapinduzi.
Baada ya vitisho vya kisiasa na kushambuliwa nchini Kenya, Ngũgĩ alihamia Uingereza, kisha Marekani, ambako ameendelea kufundisha katika vyuo vikuu mbalimbali hadi kifo chake.
Taarifa ya Eric Ponda
News
Godhana, awataka wakaazi kutoingiza siasa miradi ya maendeleo

Gavana wa kaunti ya Tana River Dhadho Godhana amewataka wenyeji wa kaunti hiyo kujiepusha na wanasiasa ambao wanaingiza siasa kwenye masuala ya maendeleo.
Godhana alisema hilo limechangia kaunti ya Tana River kusalia nyuma kimaendeleo hali ambayo itasababisha miradi mingi kuzidi kukwama.
Godhana alisema ni lazima viongozi na wenyeji wa kaunti ya Tana River washirikiane na uongozi wa kaunti ili kuafikia utekelezaji wa miradi ya maendeleo.
Wakati huo huo Godhana aliesema mradi wa Village Cluster ambao umekuwa ukipingwa ndio utakaosaidia kudhibiti changamoto ambazo zinaikumba kaunti ya Tana River.
Naye Mahat Ali Loka ambaye ni Naibu Gavana wa kaunti ya Tana River, aliwaonya wanasiasa kutoka kaunti zingine dhidi ya kuingilia siasa za kaunti hiyo huku Spika wa bunge la kaunti hiyo Osman Noor Galole, akitoa onyo kwa wafanyikazi wa umma dhidi ya kujumu la serikali ya kaunti ya Tana River.
Taarifa ya Janet Mumbi
News
Mwili wapatikana baharini Shelly Beach Likoni

Polisi kaunti ya Mombasa wanachunguza kisa ambapo mwili wa mwanamme ambaye hajafahamika umepatikana ukielea katika maji ya bahari hindi kwenye ufuo wa Shelly Beach eneo bunge la Likoni.
Ripoti ya polisi ilibaini kuwa mwili huo uligunduliwa na wavuvi eneo hilo, ambao walipiga ripoti katika kituo cha polisi cha Shelly Beach kuhusiana na tukio hilo.
Polisi walisema hawakubaini mara moja anakotoka mtu huyo.
Vile vile haikubainika iwapo marehemu alizama au aliuawa kabla ya mwili wake kutupwa baharini.
Polisi walisema hawajakutana na stakabadhi zozote za kumtambulisha mtu huyo huku wakiwasihi wananchi kutoa taarifa iwapo wanafahamu familia ya marehemu.
Mwili unahifadhiwa katika hifadhi ya maiti katika hospitali ya Rufaa ya Coast General Mombasa wakati uchunguzi zaidi ukiendelea.
Taarifa ya Joseph Jira