News
Murkomen: Machifu Walio Maeneo Hatari Kupewa Bunduki

Waziri wa usalama ndani Kipchumba Murkomen ameamrisha machifu ambao wanahofia maisha yao kutoka kaunti tano ambazo zinashuhudia msukosuko wa kiusalama kupewa bunduki kujihami.
Waziri Murkomen amesema machifu hao kutoka kaunti za Meru, Isiolo, Marsabit, Laikipia na Samburu, watasajiliwa pamoja na kupewa mafunzo ya kumiliki silaha kabla ya kupewa bunduki na serikali kama njia moja wapo ya kulinda usalama wao wanapokuwa kazini.
Akizungumza katika kikao cha kiusalama, Murkomen amesema Wizara ya usalama amepokea malalamishi kutoka kwa machifu ambao wamesema wanawafahamu wezi wa mifugo na majangali wengine ila wanahofia kuwakamata kutokana na uoga wa kuvamiwa.
Kauli yake imejiri baada ya Machifu ambao wanaishi katika maeneo yanayoshuhudiwa utovu wa usalama kulalamikia kwamba maisha yao yako hatarini.
News
Familia ya jamaa aliyezama baharini inalilia haki

Familia ya Mwanamme aliyezama baharini katika kaunti ya Kilifi siku kadhaa zilizopita, inahimiza serikali kuongeza juhudi na kuwapa msaada wa kumtafuta jamaa wao.
Ikiongozwa na Omar Ali Omar ambaye ni Kakake Marehemu, Familia hiyo ilisema wamekuwa na wakati mgumu wa kuelekea baharini kila siku kwani kufikia sasa ni siku ya nne tangu jamaa wao azame baharini.
Aidha aliitaka serikali ya kaunti kutoa taarifa sehemu mbalimbali zinazopakana na ufuo wa bahari kwani huenda mwili wa Marehemu ukasukumwa na mawimbi hadi ufuoni.

Familia ya jamaa aliyezama maji inalilia haki
Omar aliitaka idara ya kukabiliana na majanga katika kaunti kushirikiana na wavuvi wengine eneo la Mnarani pamoja na kutuma maboti zaidi kwa ajili ya uokozi wa mwili wa jamaa huyo kwani wamelazimika kugharamikia mafuta ya boti za ziada.
“Rescu timu ni boti moja, hiyo pekee yake kutafuta mtu kwa bahari ni vigumu vyombo vinatakikana vitoke vingi,washirikiene na sisi familia tuwekuongeza vyombo vya baharini kutafuta jamaa wetu, kwa sasa tunagharimika sasa boti kwenda baharini asubuhi na jioni inatugharimu shilingi elfu 16 kwa siku”, alisema Omar.
Kauli ya Omar imeungwa mkono na Mamake Marehemu ambaye ameshinikiza serikali ya kaunti kuingilia kati na kuhakikisha mwili wa mwanawe unapatikana.
Taarifa ya Joseph Jira
News
Nassir: Kaunti ya Mombasa wametenga milioni 80 za Afya

Gavana wa kaunti ya Mombasa, Abdulswamad Shariff Nassir amesema serikali ya kaunti ya Mombasa wametenga shilingi milioni 80 kugharamia sehemu ya matibabu ya wakaazi ambao hutibiwa katika hospitali za Level 4 na Level 5.
Akizungumza katika kaunti ya Mombasa, Nassir alisema fedha hizo zitagharamia bima ya afya ya SHA ya wenyeji wa kaunti hiyo kwa muda wa mwaka mmoja.
Gavana Nassir pia alisema fedha hizo zitagharamia madeni ya ziada ya matibabu kwa watoto wa chini ya umri wa miaka 5 ambao wanatibiwa kupitia bima hiyo ya SHA.
“Tumeweka dawati maalum na fedha kuweza kuwalipia ile amana ambayo ilikuwa inalipiwa SHA. Na itakuwa sio ya Public health pekee lakini kando na Public health mnakuwa mumelipiwa kwa mwaka mzima’’, alisema gavana Nassir
Wakati huo huo Gavana Nassir alieleza matumaini kwamba mpango huo utasaidia kwa asilimia kubwa kuimarisha huduma za matibabu kwa wenyeji wa kaunti hiyo.
Taarifa ya Janet Mumbi