News
Mahakama kuu yatupilia mbali ombi la Gachagua

Mahakama kuu imetupilia mbali ombi la pili la aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua la kutaka jopo la majaji watatu wanaosikiliza kesi ya kupinga kubanduliwa wake mamlakani kuzuiliwa kuskiza kesi hiyo.
Gachagua alisema kwamba majaji hao watatu akiwemo Jaji Eric Ogola, Anthony Mrima na Fridah Mugambi wanafaa kuondolewa kwenye kesi hiyo kwa misingi kwamba uteuzi wao haujazingatia sheria.
Mahakama hiyo ilitupilia mbali ombi hilo, na kusema kwamba jopo hilo la majaji watatu liliteuliwa na Jaji mkuu Martha Koome kwa kuambatana na sheria na kanuni za idara ya Mahakama.
Mahakama imeshikilia kwamba jopo hilo la majaji wa Mahakama kuu litaendelea kusikiliza kesi hiyo hadi wakati wa kutoa uamuzi kwa kuzingatia sheria, na kanuni za idara ya Mahakama pamoja na Katiba ya Kenya.
Mahakama hiyo pia ilitupilia mbali ombi la Mwanaharakati Fredrick Mula ambaye alitaka kubadilishwa kuwa mlalamishi katika kesi nne za kuondolewa mashtaka dhidi ya aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua ambazo alikuwa amewasilisha awali na kisha kutaka kujiondoa.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
News
Wakaazi wa Voi waonywa dhidi ya ugonjwa wa MPOX

Daktari wa magonjwa ya kuambukiza katika hospitali ya rufaa ya Moi mjini Voi katika kaunti ya Taita Taveta Urbanius Kioko amewataka wenyeji wa kaunti hiyo kuzingatia maagizo ya Wizara ya Afya ili kujikinga dhidi ya maambukizi ya ugonjwa wa Mpox.
Akiongea kwenye warsha ya Wanahabari iliyofadhiliwa na Shirika la Stawisha Pwani, Daktari Kioko alisema wananchi wanapaswa kujikinga ili kudhibiti ugonjwa huo kuenea.
Kioko pia aliwataka wale ambao wana dalili za ugonjwa huo kufika kwenye vituo vya afya ili kutibiwa.
“Huu ugonjwa huwa unaenezwa kupitia kutangamana, kuvaa nguo za mwenzako na kupitia hewa wakati wa kuongea’’, alisema Kioko.

Wadau wa sekta ya Afya katika kikao na Wanahabari mjini Voi
Vilevile, Kioko alitaja kisa cha mgonjwa mmoja wa Mpox kilichothibitishwa siku ya Jumanne wiki hii mjini Voi huku visa vingi vikishamiri katika kaunti Mombasa.
Haya yanajiri huku Wizara ya Afya nchini ikishinikiza wananchi kujiepusha kula nyama za Wanyamapori miongoni mwa tahadhari zingine kama njia mojawapo ya kukabiliana na maambukizi ya ugonjwa wa Mpox.
Taarifa ya Janet Mumbi
News
Mzozo kati ya Kenye na Tanzania waendelea kutokota

Serikali ya Kenya imeiandikia barua jumuiya ya afrika mashariki kupinga vikwazo vilivyowekwa na Tanzania kuhusu kufanya biashara katika taifa hilo.
Katibu mkuu katika idara ya EAC Daktari Caroline Karugu, alisema kenya imebaini kuwa agizo hilo haliambatani kamwe na masharti muhimu ya itifaki ya soko la pamoja la EAC, ambayo inahakikisha uruhu wa watu kusafiri, kuhudumu na haki ya kuanzishwa kwa biashara na raia wa mataifa ya afrika mashariki.
Aidha Kenya iliasema imeandika rasmi barua kwa EAC kuiarifu rasmi jamhuri ya muungano wa Tanzania kuangazia upya agizo hilo ili kuhakikisha inafuata kikamilifu mkataba wa EAC na sheria za Jumuia.
Maafisa wa EAC kwa sasa wanafanya uchambuzi wa hatua hiyo na itawasilisha hatua zozote zilizokiukwa pamoja na kaununi zilizopo katika mkutano ujao wa baraza la kisekta la biashara, viwanda na uekezaji.
Taarifa ya Joseph Jira