News
Maambukizi ya Homa ya Chikungunya Yaripotiwa Mombasa

Maafisa wa afya katika kaunti ya Mombasa wamethibitisha kuwepo na mkurupuko wa ugonjwa wa Chikungunya huku zaidi ya wakaazi 25 wakiripotiwa kuambukizwa.
Kwa mujibu wa maafisa hao, mkurupuko wa ugonjwa huo umetokana na mvua nyingi inayoendelea kunyesha kaunti hiyo ambayo imepelekea kuongezeka kwa mbu ambao wanasambaza virusi vya maradhi hayo.
Kaimu mkurugenzi wa idara ya afya ya umma kaunti ya Mombasa, Aisha Wayua, alisema kwamba serikali ya kaunti tayari imeanza kuchukua hatua mbalimbali ili kudhibiti kusambaa zaidi kwa maambukizi.
“Kama nilivyotaja kulingana na takwimu ni kwamba mwaka jana hatukuwa na visa vingi vya maambukizi ya Chikungunya kwa hivyo mwaka huu hasa msimu huu wa mvua ndio tunashuhudia visa vingi ya Chikungunya na ndio maana tumekuwa tukichukua sampuli ili kuzifanyia uchunguzi wa Vinasaba katika maabara ya KEMRI”, alisema Wayua
Visa vya maambukizi vimeripotiwa katika maeneo ya Likoni, Mvita, Kisauni na Nyali huku wakaazi wakihimizwa kuchukua tahadhari ili kuzuia kuenea zaidi kwa ugonjwa huo.
“Tumekuwa na homa ya Malaria na Dengu, watu wengi wana ufahamu kuhusu maumivu ya viungo na haya maambukizi labda ni yanakuja pamoja na viungo kuvimba, maumivu kuongezeka na pia mwili kuwa na vipele, labda ndio maana watu wamefikiria ni maradhi mapya”, aliongeza Wayua.
Taarifa ya Mwanahabari wetu.
News
Serikali yaombwa kuondoa miili 400 hospitali ya Malindi

Kamati ya afya ya bunge la seneti sasa imetoa wito kwa serikali kuu kuiondoa miili zaidi ya 400 ambayo inaendelea kuhifadhiwa katika makafani ya hospitali ya Malindi kaunti ya Kilifi baada ya kufukuliwa katika msitu wa Shakahola.
Akizungumza kwa niaba ya kamati hiyo, seneta wa kaunti ya Bungoma David Wakoli, alisema maiti hizo zimezuia serikali ya kaunti ya Kilifi kuendeleza ujenzi wa makafani mpya katika hospitali hiyo.
Wakoli alisema ikiwa serikali itazingatia hilo basi serikali ya kaunti ya Kilifi itaweza kujenga makafani hiyo bila changamotoz zozote.
“Tunataka kuiomba serikali kuu kuruhusu serikali ya kaunti ya Kilifi kuendeleza ujenzi huo, na serikali inapaswa kutafuta eneo maalumu la kuhifadhi na kuizika miili hiyo’’ Alisema Wakoli
Hii ni baada ya serikali kutenga fedha katika bajeti ya mwaka jana ili kujenga makafani mpya kushindwa kuendeleza ujenzi huo kutokana na miili ambayo bado haijatambuliwa.
Ni kauli ambayo iliungwa mkono na seneta wa kaunti ya Kilifi Stewart Madzayo ambaye aliitaka serikali kuu kukamilisha shughuli ya uambatanishaji wa chembechembe za msimbojeni-DNA, ili kupeana miili hiyo kwa wapendwa wao kabla ya kuanza kufukua miili mingine katika eneo la Kwa Binzaro huko Shakaholo.
“Kule Shakahola tumeona watu wanaendelea kufa na wengine kuzikwa, kwahivyo tunaomba zile maita ambazo ziko hapa ziweze kuondolewa na serikali kuu maana hakuna nafasi,’’ alisisitiza Madzayo.
Taarifa ya Janet Mumbi
News
Rais Ruto amteua Amani Yuda Komora kuwa Mwenyekiti wa NPSC

Rais William Ruto amemteua Amani Yuda Komora kuwa Mwenyekiti wa Tume ya kitaifa ya Huduma ya Polisi (NPSC) na Angeline Yiamiton Siparo kuwa mwanachama.
Uteuzi huo unafuatia mahojiano ya hivi majuzi yaliyofanywa na Tume ya Utumishi wa Umma (PSC) kati ya Julai 1 na Julai 3 2025, baada ya kuorodhesha wagombea wanane wa uwenyekiti na 11 wa wajumbe.
Wawaniaji walitakiwa kuwasilisha kitambulisho halisi cha kitaifa, hati za masomo, na idhini halali kutoka kwa mashirika ya serikali.
Stakabadhi nyingine ilikuwa ni pamoja na nyaraka za mamlaka ya ukusanyaji ushuru nchini (KRA), tume ya maadili na kupambana na ufisadi (EACC), fomu maalum kutoka kwa mkurugenzi wa idara ya upelelezi wa jinai (DCI), bodi ya mikopo ya elimu ya juu (HELB) na ofisi yoyote iliyosajiliwa ya marejeleo ya mikopo.
Wale walio na shahadi ya digrii za mataifa ya kigeni walilazimika kuwasilisha barua za utambulisho kutoka kwa tume ya elimu ya vyuo vikuu.
Shughuli ya uteuzi ilianza mnamo mwezi Februari baada ya kujiondoa kwa tume ya awali, inayoongozwa na Eliud Kinuthia, ambaye muhula wake wa miaka sita ulimalizika mapema mwaka huu wa 2025.
Iwapo itaidhinishwa na Bunge, NPSC itajumuisha Komora kama Mwenyekiti na wanachama watano wakiwemo, Peris Muthoni Kimani, Edwin Cheluget, Benjamin Juma Imai, Collete Suda na Angeline Yiamiton Siparo
Komora ni naibu mwenyekiti wa zamani wa tume ya kutathmini mishahara na marupurupu ya wafanyakazi wa umma (SRC), na hapo awali alikuwa na majukumu ya juu ya rasilimali watu katika Mamlaka ya Bandari KPA na KRA.
Taarifa ya Joseph Jira