News
Kesi ya Wakili Joseph Munyithia na Farid Salim Yachukua Mkondo Mpya

Kesi ya wizi wa ardhi inayomuhusisha Wakili Joseph Munyithia na mfanyabiashara Farid Salim Almaary imechukua mkondo mpya.
Hii ni baada ya mwanasheria huyo kuandikisha taarifa katika kituo cha polisi cha Makupa mjini Mombasa akijitenga na madai ya wizi wa kipande hicho cha ardhi kilichoko katika eneo la Shelly Beach eneo bunge la Likoni.
Katika taarifa yake kwa Polisi, Munyithia ameeleza kwamba alishughulikia ardhi hiyo ambayo alikabidhiwa hatimiliki na Gabriel Mutiso ambaye kwa sasa ni marehemu.
Aidha ameeleza kwamba mnamo Machi tarehe 4 mwaka 2024 alipeana cheti cha kukodisha shamba hilo pamoja na barua ya uhamisho hadi kwa kampuni ya J Katisya and Co Advocates.
Wakili huyo mkuu katika kampuni ya Munyithia, Mutugi na Umazi Advocates ameandikisha taarifa takriban wiki moja baada ya ofisi ya mkurugenzi wa mashtaka ya umma nchini ODPP, kuagiza kukamatwa kwake pamoja na mfanyabiashara Farid.
Munyithia pamoja na mfanyabiashara huyo wanadaiwa kuiba na kuficha hati miliki ya ardhi hiyo kulingana na malalamishi yaliowasilishwa na wamiliki wa shamba hilo.
News
Mombasa inaongoza kwa maambukizi ya MPOX nchini

Wizara ya afya nchini imesema kaunti ya Mombasa inaongoza kwa visa vya maambukizi ya ugonjwa wa Mpox.
Kwa mujibu wa mkurugenzi mkuu wa idara ya afya nchini Daktari Patrick Amoth, kaunti ya Mombasa imerekodi visa 139 kati ya visa 300 vilivyoripotiwa na wizara hiyo.
Amoth alidokeza kuwa serikali itatangaza siku maalum ya kutoa chanjo ya kudhibiti msambao wa ugonjwa huo wakishirikiana na shirika la afya ulimwenguni WHO.
Mkurugenzi huyo vile vile alimesema zoezi hilo litaambatana na hamasa kwa wananchi kuhusu namna ya kujikinga na maambukizi zaidi.
“Kwa wakati huu Mombasa ndio inaongoza kwa idadi ya visa 139 kwa hivyo tuchuke tahadhari kuhakikisha kwamba tunazuia maambukizi, na tunafanya mpango pamoja na shirika la afya duniani WHO, hapa tutakuja na mpango wa chanjo na ikifika huo wakati tunaomba watu wajitokeze wapate chanjo ili wapate kinga”,alisema Daktari Amoth.
Wakati huo huo Amoth aliokeza kuwa uchunguzi wa vifo vya watu wanne walioaga dunia wiki chache zilizopita huko Migadini, eneo bunge la Changamwe kaunti ya Mombasa umebaini walifariki kutokana na magonjwa mengine na wala sio maambukizi ya ugonjwa wa MPOX kama ilivyodhaniwa na wakaazi.
Taarifa ya Mwanahabari wetu.
News
Wavuvi wawili wafa maji Watamu,Kilifi

Jamii ya wavuvi katika eneo la Watamu eneo bunge la Kilifi Kaskazini inaiomba serikali ya kaunti ya Kilifi na ile ya kitaifa kununua boti za uokozi ili kusaidia kuokoa maisha wakati kunapotokea dharura baharini.
Hii ni baada ya wavuvi wawili kupotoea katika bahari hindi eneo la Watamu walipokuwa wakiendeleza shughuli zao za uvuvi siku ya Alhamisi 24, Julai 2025.
Kufikia sasa wawili hao hawajapatikana licha ya juhudi za wadau mbalimbali ikiwemo jeshi la wanamaji kuwatafuta.
Kiongozi wa vijana eneo la Watamu Bakari Shaban, alisema kuwa juhudi za kuwatafuta wavuvi hao ambao ni mandugu wanaotambulika kama Athman Lali na Huzefa Lali zinaendelea.
Shaban alisistiza haja ya serikali kuangazia suala la ununuzi wa mashua za kisasa za uokozi ili kupunguza visa vya wavuvi kuangamia baharini wakati wanapoelekea kuvua.
“Mpaka sasa juhudi zote zimefanyika lakini ndugu zetu hatujajua wako sehemu gani, serikali itusaidie mji wetu wa Watamu ni mji wa utalii, tunaomba tupate boti za kuokoa maisha baharini, popote alipo waziri Ali Joho angalau tupate boti za uokozi kama mbili hapa Watamu ni kitovu cha utalii kunamahoteli mengi, watalii wote wanaokuja Watamu mpaka leo hakuna boti za uokozi”, alisema Shaban.
Kwa upande wao wazazi wa wavuvi waliopotea baharini Lali Athman Lali na Dhurai Mohamed Ali waliiomba serikali kuweka juhudi zaidi za kuwasaidia kuwapata wana wao kwani ndio tegemeo kubwa kwa familia yao.
“Uko usaidizi unatumika, kuna vijana wanaojitolea kwa maboti wanaenda ile sehemu ambayo wavuvi wanavua, wanajaribu kuzunguka lakini toka siku hiyo hawajapata chochote: Katika Maisha yangu mimi nawategemea hawa watoto kunisomeshea hawa watoto wangu ambao ni wadogo zao mashule, kwa chakula kwa hivyo naomba serikali inisaidie kwa sababu ndio tegemeo langu hao watoto”.walisema wazazi.
Kisa hiki kinajiri miezi kadhaa baada ya mvuvi mmoja kutoka eneo la Mnarani mjini Kilifi kufariki baharini baada ya kugongwa kichwani kwa pondo na wavuvi wenzake kulipotokea mzozo kuhusu pato la samaki.
Kufikia sasa mwili wa mvuvi huyo haujapatikana
Taarifa ya Mwanahabari wetu