News
Kenya, Ufaransa kukabili mabadiliko ya tabia nchi.

Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron amesisitiza ushirikiano kati ya ufaransa na Kenya katika kutetea ajenda ya kimataifa inayojumuisha maendeleo endelevu na hatua za kukabili mabadiliko ya tabia nchi, kabla ya mkutano mwengine utakaohusisha bara afrika na Ufaransa jijini Nairobi mwaka ujao.
Akizungumza kutoka Seville katika kongamano la ngazi ya juu kuhusu ushirikiano wa kimataifa, Rais Macron alisisitiza maono yake ya pamoja na Rais William Ruto akisema hakuna nchi inapaswa kulazimishwa kuchagua kati ya maendeleo ya kiuchumi na ulinzi wa mazingira.
“Pamoja na Rais William Ruto, tunashiriki ahadi moja: kwamba hakuna nchi inapaswa kuchagua kati ya maendeleo na kulinda sayari,” Macron alisema. “Haya ndiyo matamanio tunayoleta leo Seville na washirika wetu, kama sehemu ya mkataba wa mafanikio, watu na sayari uliozinduliwa miaka miwili iliyopita huko Paris.”
Viongozi hao wawili wanatarajiwa kuendeleza ajenda hii katika kongamano la Afrika na Ufaransa 2026, ambalo litasimamiwa na Kenya na Ufaransa jijini Nairobi.
Mkutano huo unatazamiwa kuangazia ushirikiano wa kibunifu unaoshughulikia malengo ya maendeleo endelevu ya afrika sambamba na kukuza ukuaji wa uchumi jumuishi.
Rais Macron pia alisema kuwa Kenya na Ufaransa zinashirikiana kikamilifu katika miradi muhimu ya nchi mbili kama vile mpito wa nishati, miundombinu endelevu ya uchukuzi na maendeleo ya kilimo.
Alisema miradi hii, inaonyesha aina ya ushirikiano wa kimantiki unaohitajika ili kufikia maendeleo yanayostahimili hali ya hewa.
Mbali na ushirikiano wa kiuchumi na kimazingira, marais hao wawili walisisitiza dhamira yao ya pamoja ya kukuza amani na usalama kote barani Afrika, hasa katika eneo la Maziwa Makuu, Sudan na Somalia.
“Tulisisitiza dhamira yetu ya pamoja ya amani na usalama katika eneo la Maziwa Makuu, Sudan, na Somalia,” Rais Macron alibainisha, akisisitiza jukumu la Ufaransa na Kenya kusaidia utulivu wa kikanda kupitia ushirikiano wa kidiplomasia na usaidizi wa maendeleo.
Tarifa ya Joseph Jira
News
Serikali yaombwa kuondoa miili 400 hospitali ya Malindi

Kamati ya afya ya bunge la seneti sasa imetoa wito kwa serikali kuu kuiondoa miili zaidi ya 400 ambayo inaendelea kuhifadhiwa katika makafani ya hospitali ya Malindi kaunti ya Kilifi baada ya kufukuliwa katika msitu wa Shakahola.
Akizungumza kwa niaba ya kamati hiyo, seneta wa kaunti ya Bungoma David Wakoli, alisema maiti hizo zimezuia serikali ya kaunti ya Kilifi kuendeleza ujenzi wa makafani mpya katika hospitali hiyo.
Wakoli alisema ikiwa serikali itazingatia hilo basi serikali ya kaunti ya Kilifi itaweza kujenga makafani hiyo bila changamotoz zozote.
“Tunataka kuiomba serikali kuu kuruhusu serikali ya kaunti ya Kilifi kuendeleza ujenzi huo, na serikali inapaswa kutafuta eneo maalumu la kuhifadhi na kuizika miili hiyo’’ Alisema Wakoli
Hii ni baada ya serikali kutenga fedha katika bajeti ya mwaka jana ili kujenga makafani mpya kushindwa kuendeleza ujenzi huo kutokana na miili ambayo bado haijatambuliwa.
Ni kauli ambayo iliungwa mkono na seneta wa kaunti ya Kilifi Stewart Madzayo ambaye aliitaka serikali kuu kukamilisha shughuli ya uambatanishaji wa chembechembe za msimbojeni-DNA, ili kupeana miili hiyo kwa wapendwa wao kabla ya kuanza kufukua miili mingine katika eneo la Kwa Binzaro huko Shakaholo.
“Kule Shakahola tumeona watu wanaendelea kufa na wengine kuzikwa, kwahivyo tunaomba zile maita ambazo ziko hapa ziweze kuondolewa na serikali kuu maana hakuna nafasi,’’ alisisitiza Madzayo.
Taarifa ya Janet Mumbi
News
Rais Ruto amteua Amani Yuda Komora kuwa Mwenyekiti wa NPSC

Rais William Ruto amemteua Amani Yuda Komora kuwa Mwenyekiti wa Tume ya kitaifa ya Huduma ya Polisi (NPSC) na Angeline Yiamiton Siparo kuwa mwanachama.
Uteuzi huo unafuatia mahojiano ya hivi majuzi yaliyofanywa na Tume ya Utumishi wa Umma (PSC) kati ya Julai 1 na Julai 3 2025, baada ya kuorodhesha wagombea wanane wa uwenyekiti na 11 wa wajumbe.
Wawaniaji walitakiwa kuwasilisha kitambulisho halisi cha kitaifa, hati za masomo, na idhini halali kutoka kwa mashirika ya serikali.
Stakabadhi nyingine ilikuwa ni pamoja na nyaraka za mamlaka ya ukusanyaji ushuru nchini (KRA), tume ya maadili na kupambana na ufisadi (EACC), fomu maalum kutoka kwa mkurugenzi wa idara ya upelelezi wa jinai (DCI), bodi ya mikopo ya elimu ya juu (HELB) na ofisi yoyote iliyosajiliwa ya marejeleo ya mikopo.
Wale walio na shahadi ya digrii za mataifa ya kigeni walilazimika kuwasilisha barua za utambulisho kutoka kwa tume ya elimu ya vyuo vikuu.
Shughuli ya uteuzi ilianza mnamo mwezi Februari baada ya kujiondoa kwa tume ya awali, inayoongozwa na Eliud Kinuthia, ambaye muhula wake wa miaka sita ulimalizika mapema mwaka huu wa 2025.
Iwapo itaidhinishwa na Bunge, NPSC itajumuisha Komora kama Mwenyekiti na wanachama watano wakiwemo, Peris Muthoni Kimani, Edwin Cheluget, Benjamin Juma Imai, Collete Suda na Angeline Yiamiton Siparo
Komora ni naibu mwenyekiti wa zamani wa tume ya kutathmini mishahara na marupurupu ya wafanyakazi wa umma (SRC), na hapo awali alikuwa na majukumu ya juu ya rasilimali watu katika Mamlaka ya Bandari KPA na KRA.
Taarifa ya Joseph Jira