Uncategorized
Kaunti ya Mombasa Yatakiwa Kuchukua Hatua za Dharura Kusafisha Soko la Marikiti

MOMBASA – Serikali ya Kaunti ya Mombasa imetakiwa kuchukua hatua za haraka kuondoa taka zilizorundikana katika soko la Marikiti, hatua inayolenga kupunguza hatari ya kiafya na uvundo unaosababishwa na uchafu huo, hasa katika msimu huu wa mvua.
Akizungumza na wanahabari, Mwenyekiti wa soko hilo, Muhammad Ali, amesema kuwa hali ya uchafu sokoni hapo imefikia kiwango cha kutisha, huku baadhi ya wanunuzi wakikwepa kufika sokoni humo kutokana na harufu kali na mazingira yasiyovutia.
“Tumejaribu kuwasiliana na serikali ya kaunti mara kadhaa kuhusu suala hili, lakini hadi sasa hatujapata suluhisho la kudumu. Taka zimejaa kila kona ya soko, na hali hii si tu inatishia afya ya wananchi, bali pia inasababisha hasara kwa wafanyabiashara,” alisema Ali.
Kwa mujibu wa mwenyekiti huyo, mvutano kati ya serikali ya kaunti na baadhi ya wafanyabiashara kuhusu ni nani anapaswa kukusanya taka umekuwa kizingiti kikuu katika kutatua changamoto hiyo. Hata hivyo, amesisitiza kuwa ni jukumu la moja kwa moja la serikali ya kaunti kuhakikisha kuwa huduma za ukusanyaji taka zinatolewa kwa wakati katika masoko yote ya umma.
“Hili si suala la kubebana lawama. Serikali ya kaunti ina wajibu wa kuhakikisha mazingira safi na salama kwa wafanyabiashara na wateja,” aliongeza.
Wafanyabiashara sokoni Marikiti wanasema hali hiyo imeathiri sana mapato yao, huku wakiitaka kaunti kuingilia kati na kurejesha heshima ya soko hilo linalohudumia maelfu ya wakazi wa Mombasa kila siku.
Uncategorized
Rais Ruto: Usajili wa makurutu wa NYS utaongezeka hadi laki moja

Rais William Samoei Ruto amesema usajili wa makurutu watakaojiunga na huduma ya vijana kwa taifa NYS utaongezeka kutoka vijana 18,000 hadi 100,000 katika miaka mitatu ijayo.
Akizungumza katika hafla ya 89 ya kufuzu kwa makurutu wa NYS katika kambi ya Gilgil katika kaunti ya Nakuru, Rais Ruto alisema ongezeko hilo linaonyesha uimarishaji katika mafunzo na ujuzi ili kudhibiti hali ya ukosefu wa kazi miongoni mwa vijana nchini.
‘’Serikali pia imeanzisha mipango kadhaa inayolenga kukabiliana na ukosefu wa ajira kwa vijana’’ alisema rais Ruto.
Rais Ruto pia alisema NYS imekuwa yenye tija katika masuala ya kama ya kilimo, uhandisi na ujenzi miongoni mwa mengine.

Makurutu wa NYS katika kambi ya Gilgil katika kaunti ya Nakuru
“Tayari inazalisha unga wa mahindi, mafuta ya kupika, na bidhaa za matunda, kupunguza gharama, na kuzalisha mapato. Hivi karibuni, NYS pia itatoa sifa zinazotambulika kitaifa na kimataifa.” aliongeza rais Ruto.
Zaidi ya makurutu 18,000 idadi ambayo ni kubwa zaidi katika historia ya NYS, baada ya kufanya mafunzo ya miezi sita rais Ruto aliagiza wizara ya mambo ya ndani kuhakikisha makurutu 4000 wanajiunga na huduma ya kitaifa kwa polisi wakati wa kuwasajili makurutu 10,000 katika usajili ujao wa maafisa wa polisi.
Waliohudhuria hafla hiyo ni Gavana wa Nakuru Susan Kihika, waziri wa utumishi wa umma nchini Geoffrey Ruku na Kamanda Mkuu wa NYS James Tembur.
Taarifa ya Janet Mumbi
Uncategorized
Douglas Kanja, Mohammed Amin wakosa kufika mahakamani.

Siku kumi baada ya mwanablogu Ndiang’ui Kinyagia kutoweka, kesi ya kumtaka inspecta jenerali wa polisi Doglas Kanja kueleza alipo mwanablogu huyo iliendelea kusikilizwa katika mahakama ya Milimani jijini Nairobi.
Inspecta jenerali wa polisi Douglas Kanja pamoja na mkurugenzi wa idara ya upelelezi wa makosa ya jinai DCI Mohammed Amin walikosa kufika katika mahakama kama ilivyo amriwa hapo awali.
Haya yanajiri huku maafisa wa DCI wakiongozwa na mkurugenzi wa DCI wakiiambia mahakama siku ya jumatatu 30 juni 2025 kwamba hawakumkamata mwanablogu huyo.
Kwa upande wake Jaji Chacha Mwita aliwataka wawili hao kuhakikisha wanaeleza alipo mwanablogu huyo.
“Hakuna vile mtu anaweza toweka ghafla na hajulikani alipo, hatutaki maneno mengi tunachotaka ni huyu mtu ako wapi mleteni mbele ya mahakama awe hai au mfu tunachotaka ni huyu mtu yupo wai?”,aliuliza jaji Chacha Mwita.
Viongozi mbalimbali akiwemo kinara wa chama cha PLP Martha Karua, mbunge wa Embakasi Mashariki Paul Ongili Owino maarufu Babu Owino miongoni mwa viongozi wengine walihudhuria kikao cha kesi hiyo huku Karua akisema kwamba, wawili hao wameonyesha utovu mkubwa na nidhamu kwa kukiuka amri ya mahakama.
Ikumbukwe kwamba mwanablogu Kinyagia alikamatwa tarehe 21 juni 2025 kwa kosa la uhalifu wa kimitandao ikiwa ni kuchapisha ratiba ya maandamano yaliyofanyika Jumatano tarehe 25 Juni 2025.
Taarifa ya Elizabeth Mwende