News
Inspekta Jenerali Kanja aomba Msamaha.

Inspekta Jenerali wa polisi Douglas Kanja ameomba msamaha kwa kutoa ripoti isiyo sahihi kuhusu uchunguzi wa mauaji dhidi ya mwalimu na mwanablogu Albert Ojwang.
Mapema wiki hii, Kanja alidai kuwa Ojwang alifariki kwa kujitoa uhai baada ya kujigonga kichwa kwenye kuta za seli za polisi.
Madai hayo yalizua taharuki miongoni mwa wananchi ambao walishutumu polisi kwa kujaribu kuficha ukweli kuhusu kifo cha mwanablogu huyo.
Wakati wa kikao cha bunge la seneti siku ya jumatano tarehe 11 mwaka 2025, inspekta jenerali Kanja alilaani mauaji hayo na kudai hangeweza kutoa tamko lolote hadi mamlaka huru ya kutathmini utendakazi wa polisi (IPOA) ikamilishe uchunguzi wake.
Pia aliapa kuwachukulia hatua maafisa wa polisi waliompatia ripoti hiyo akitaja taratibu za kinidhamu zitaambatana na taratibu za kawaida za uendeshaji.
“Ikiwa katika uchunguzi unaoendelea na IPOA tutajua ukweli, maafisa waliotoa ripoti ya awali watalazimika kukabiliwa na taratibu za kinidhamu, kutokana na kile tulichosikia hapa, tutaendelea na kuchukua hatua zinazohitajika dhidi ya afisa aliyetupa nyenzo siku hiyo,” Kanja alisema.
Hata hivyo maseneta hao walipinga matamshi ya Kanja na kudokeza kuwa IPOA imefutilia mbali madai ya Ojwang’ kujiua kufuatia kutolewa kwa matokeo ya uchunguzi wa maiti.
Ripoti ya upasuaji wa maiti ya mwanapatholojia wa serikali Bernard Midia , ilithibitisha kuwa Ojwang alitendewa ukatili, kunyongwa, kuteswa na kuuawa na maafisa wa polisi.

Albert Ojwang’ mwalimu na mwanablogu anayedaiwa kuuawa na maafisa wa polisi.
Kisa cha mauaji ya mwanablogu huyo Albert Ojwang’ kilizua mihemko miongoni mwa wakenya huku baadhi ya vijana pamoja na wanaharakati wa kutetea haki za kibinadam nchini wakiandamana wakishinikiza naibu inspekta mkuu wa polisi Eliud Lagat kujiuzulu na kuchukuliwa hatua za kisheria.
Taarifa ya Joseph Jira
News
Nassir: Kaunti ya Mombasa wametenga milioni 80 za Afya

Gavana wa kaunti ya Mombasa, Abdulswamad Shariff Nassir amesema serikali ya kaunti ya Mombasa wametenga shilingi milioni 80 kugharamia sehemu ya matibabu ya wakaazi ambao hutibiwa katika hospitali za Level 4 na Level 5.
Akizungumza katika kaunti ya Mombasa, Nassir alisema fedha hizo zitagharamia bima ya afya ya SHA ya wenyeji wa kaunti hiyo kwa muda wa mwaka mmoja.
Gavana Nassir pia alisema fedha hizo zitagharamia madeni ya ziada ya matibabu kwa watoto wa chini ya umri wa miaka 5 ambao wanatibiwa kupitia bima hiyo ya SHA.
“Tumeweka dawati maalum na fedha kuweza kuwalipia ile amana ambayo ilikuwa inalipiwa SHA. Na itakuwa sio ya Public health pekee lakini kando na Public health mnakuwa mumelipiwa kwa mwaka mzima’’, alisema gavana Nassir
Wakati huo huo Gavana Nassir alieleza matumaini kwamba mpango huo utasaidia kwa asilimia kubwa kuimarisha huduma za matibabu kwa wenyeji wa kaunti hiyo.
Taarifa ya Janet Mumbi
News
Chibule, apendekeza adhabu kali kwa wanaoendeleza dhulma za kijinsia

Naibu gavana kaunti ya Kilifi Flora Mbetsa Chibule, amependekeza adhabu kali kwa watu wanaotekeleza visa vya dhulma za kijinsia katika jamii.
Chibule alisema visa vya dhulma za kijinsi dhidi ya watoto vimekithiri katika jamii hasa kaunti ya Kilifi, akiahidi ushirikiano wa hali ya juu na wadau mbalimbali ili kukomesha visa hivyo.
Akizungumza wakati wa maadhimisho ya hamasa kuhusu dhulma za kijinsia katika uwanja wa Bofa Youth mjini Kilifi, Chibule alisema ili kufanikisha ndoto ya mtoto wa kike ni lazima haki zao za kimsingi zilindwe.
“Kwa ambao wanadhulumu mtoto wa kike na kiume, kwa wale ambao wanaingia misuli kwa misuli wanafaa kuwekwa gerezani kabisa”, alisema Chibule.

Wanaharakati wa kijamii wapinga unyanyasaji wa kijinsi, Kilifi
Kwa upande wake Mwakilishi wa kike kaunti ya Kilifi Getrude Mbeyu aliyeandaa hafla hiyo kupitia hazina ya kitaifa ya NGAAF na kutoa hundi ya kima cha shilingi milioni 1.6 kwa makundi 14, alisisitiza hamasa zaidi kwa jamii kuhusu jinsi ya kukomesha visa hivyo.
“Ni jukumu letu la kuwaeleza hawa watu watambua jinsi ya kuripoti hizi kesi, yani kwa mfano umedhulumiwa ni wapi pa kuanzia na hatua hii itakomesha hizi visa”, alisema Mbeyu.
Naye Mzee wa mataa wa Kiwandani mjini Kilifi Elina Nyevu alisema visa vya dhulma za kimapenzi vimekithiri mno katika mtaa huo, akipendekeza hamasa zaidi kwa jamii.
“Hapa kwetu Kiwandani visa vya dhulma za kijinsia ni vingi sana, kuna ulevi na ukosefu wa ajira ambao umechangia utumiaji wa Mihadarati na unyanyasaji wa watoto wadogo kimapenzi, alisema Elina.
Hata hivyo katika halfa hiyo baadhi ya watoto waliopitia madhila hayo hasa ubakaji wameelezea masaibu waliopitia japo haki yao kupitia idara ya usalama walikosa kufaulu.
Taarifa ya Lolani Kalu.