News
Gachagua: Upinzani hauna nia ya kupindua serikali

Aliyekuwa naibu wa rais Rigathi Gachagua amekanusha madai kwamba mrengo wa upinzani unapanga kumuondoa rais William Samoei Ruto madarakani.
Katika taarifa yake ya siku ya Jumatano terehe 9 mwezi Julai, 2025 kwa vyombo vya habari, muda mfupi baada ya hotuba ya rais Ruto, Gachagua alisema vuguvugu la ONE TAM halina nia ya kuchukua mamlaka kwa njia ambayo sio halali.
Gachagua alimtaka rais Ruto kutekeleza majukumu yake ipasavyo na pia kudhibiti visa vya vya watu kutekwa nyara na kuuliwa katika mazingira tatanisha.
Gachagua pia alimkosoa rais Ruto akisema amekuwa akipuuza kilio cha wananchi hali ambayo inawafanya Wakenya wengi kuendelea kuhangaika.
‘’Bwana Ruto punguza hasira na kwa unyenyekevu mwingi nakushauri kwamba hasira sio suluhu maana haitakusaidia. Unapaswa kujua nini unapaswa kufanya maana haujakuwa ukiwasikiza Wakenya’’ alisema Gachagua.
Wakati huo huo, Gachagua ambaye pia ni Kinara wa chama cha DCP aliibua madai kwamba Rais Ruto amekuwa akiwatumia wahalifu kuharibu mali ya watu wakati maandamano ya vijana wa kizazi cha Gen Z ambao wamekuwa wakiandamana nchini kuwasilisha matakwa yao kwa serikali.
‘’Siku ya Sabasaba wahalifu hao walipeleka maandamano maeneo mbalimbali nchini hasa eneo la Mlima Kenya na yale mengine ambayo yanakashifu uongozi wa serikali kuu’’ aliongeza Gachagua.
Taarifa ya Janet Mumbi
News
Mahakama ya Malindi yawaachilia washukiwa 3 wa kesi ya Kwa Binzaro

Mahakama Kuu ya Malindi imewaachilia washukiwa watatu wanaohusishwa na kesi ya mauaji ya halaki ya watu katika kijiji cha Kwa Binzaro eneo bunge la Magarini kaunti ya Kilifi.
Hakimu wa Mahakama hiyo Joy Wesonga aliagiza kuachiliwa huru kwa Safari Kenga Nzai, Gona Charo Kalama na Kahindi Kazungu Garama wote wakiwa wakaazi wa kijiji hicho cha Kwa Binzaro.
Watatu hao walikuwa wamekamatwa baada ya kudaiwa kuuza shamba la ekari tano kwa mshukuwa mkuu wa mauaji ya watu katika kijiji cha Kwa Binzaro Sherleen Temba Anido.
Hakimu Wesonga aliwaagiza washukiwa hao kuhakikisha wanasalimisha nakala za vitambulisha vyao vya kitaifa kwa idara husika, kuripoti kwa Naibu Chifu wa eneo hilo mara mbili kwa wiki pamoja na kujisalimisha kwa maafisa wa upelelezi wa kesi hiyo mara moja kila baada ya wiki mbili.

Miili iliyofukuliwa katika kijiji cha Kwa Binzaro
Wakati huo huo upande wa mashtaka ukiongozwa na Naibu mkurugenzi wa mashtaka ya umma Jamie Yamina, uliomba kuwasilisha watu wengine wanne Mahakamani ikiwemo Jairus Otieno na mkewe Lilian Akinyi, Kahonzi Katana Karisa na Loise Zawadi waliojionda kama washukiwa na kugeuka kuwa mashahidi wa serikali.
Upande wa mashtaka pia uliaka kupewa siku 60 zaidi kuendelea kuzuiliwa kwa washukiwa wakuu Sherleen Temba Anido, James Kahindi Kazungu, Thomas Mukunwe na Kahidi Kazungu Garama katika kituo cha polisi cha Ngerenya, Kilifi, Watamu na Kijipwa ili kukamilisha uchunguzi wao kwani wanne hao wanakabiliwa na mashtaka ya itikadi kali, ugaidi, kujihusisha na uhalifu na kupanga mauaji.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
News
Chrispus aomba msahama bunge la kaunti ya Taita Taveta

Mwakilishi wadi ya Bomani mjini Taveta kaunti ya Taita Taveta Chrispus Tondoo ameliomba bunge la kaunti hiyo msamaha kutokana na matamshi aliyoyatoa hapo awali akikashifu bunge hilo kwa madai ya kushamiri kwa visa vya ufisadi na utepetevu.
Tondoo akiomba msamaha katika bunge hilo alisema alitambua athari zilizosababishwa na matamshi hayo kwa wenyeji wa kaunti hiyo na bunge hilo, hali ambayo imemfanya kuchukua hatua hiyo ya kuomba msamaha.
Aidha Tondoo aliahidi kuliheshimu bunge hilo kwa mujibu wa kanuni na Sheria za bunge la kaunti ya Taita Taveta.
‘’Naomba msamaha kutokana na matamshi ambayo niliyatoa tarehe 2 na tarehe 3 mwezi wa Juni mwaka huu wa 2025 kwani hayakuwa yenye heshima kwa wenyeji wa Taita Taveta na bunge la kaunti’’, alisema Tondoo.
Tondoo alikuwa Mwakikishi wa wadi wa pili kuomba msamaha baada ya Mwakilishi wa wadi ya Kaloleni mjini Voi Ahmed Azari kuchukua hatua hiyo mwezi mmoja uliyopita.
Haya yalijiri baada ya kaimu spika wa bunge hilo Anselim Mwadime kuapa kuwachulia hatua za kisheria wanachama wanne wa bunge hilo, wawili wakiwa ni Tondoo na Azari ambayo tayari wameomba msamaha huku wawili wakiwa wamesalia bila kuomba msamaha.
Taarifa ya Janet Mumbi