News
Felkin: Tumeweka mikakati ya kutoa elimu ya juu kupitia mtandao

Waziri wa Elimu kaunti ya Kilifi Felkin Kaingu alisema serikali ya kaunti ya Kilifi imeweka mikakati ya kuimarisha mpango wa elimu kwa wote unaotoa elimu ya juu kupitia mtandao.
Akizungumza na Coco Fm, Waziri Kaingu alikariri kuwa tayari serikali ya kaunti ya Kilifi imetenga bajeti ya kufanikisha utumizi wa mtandao wa bure yani Wi-Fi katika maeneo kadhaa ya kaunti.
Kaingu alisema eneo la bustani ya Mazingira mjini Kilifi, Soko la kwa Charo ya Mae, Mtwapa, Mariakani miongoni mwa maeneo mengine yaliteuliwa kuwekewa mtandao huo wa Wi-Fi.
“Tuko na mipango mizuri ya kuhakikisha tumeweka mitandao wa Wi-Fi, katika maeneo mbalimbali ili kuhakikisha vijana wanaweza kupata elimu kupitia mtandao”, alisema Felkin.
Waziri Kaingu alisema kuwa Gavana wa kaunti ya Kilifi Gideon Mung’aro, anapania kuimarisha vijana kupitia mifumo mbalimbali ikiwemo elimu mtandaoni.
Waziri huyo pia alibaini kuwa watakaofuzu kupitia mpango huo wa elimu kwa wote watanufaika na ajira sio tu za humu nchini lakini pia ughaibuni.
Taarifa ya Hamis Kombe
News
Karua na Mutunga, waishtaki Tanzania

Aliyekuwa Jaji mkuu nchini Willy Mutunga pamoja na Kinara wa chama cha People’s Liberation Party Martha Karua kuishtaki serikali ya Tanzania katika Mahakama ya Haki ya Afrika Mashariki (EACJ).
Mutunga na Karua pamoja na Wanaharakati wengine wanne wa haki za binadamu akiwemo Hussein Khalid, Gloria Kimani, Lyn Nguji na Hanifa Adan walishtumu serikali hiyo kwa kuwazuia kuingia nchini humo.
Wanne hao wadai kwamba haki zao zilikiukwa kwa kuondolewa kwa nguvu huku wakidai kwamba serikali ya Tanzania imekiuka mikataba ya Kikanda.

Jumba la Jumuiya ya Afrika Mashariki iliyo na Mahakama ya EACJ
Wanne hao sasa wanaitaka Mahakama hiyo kuishurutisha serikali ya Tanzania kuondoa alama zozote hasi za uhamiaji kwenye Pasipoti zao za usafiri na kuwalipa fidia maalum kwa gharama walizopata wakitafuta ushauri wa kisaikolojia kutokana na msongo wa mawazo na kihisia.
Haya yanajiri wiki chache baada ya Willy Mutunga, Martha karua na Wanaharakati wanne wa kutetea haki za kibinadamu pamoja na Boniface Mwangi na Agatha Atuhaire kutoka nchini Kenya na Uganda kutimuliwa nchini humo baada ya kuzuiliwa.
Wakenya hao walikuwa wamezuru nchini kusikiliza na kumuakilisha Kiongozi wa chama cha upinzani nchini humo Tundu Lissu katika kesi ya uhaini inayomkabili.
Lissu ambaye anakabilia na kesi ya uhaini pamoja na tuhuma za kuchapisha taarifa za uongo yupo rumande akisubiri kesi yake kutajwa tena tarehe 16 mwezi Juni 2025.
Taarifa ya Elizabeth Mwende
News
Wanafunzi wa chuo kikuu cha Pwani wanataka uwazi kuhusu kifo cha Ojwang’

Baadhi ya wanafunzi wa chuo kikuu cha pwani mjini Kilifi kaunti ya Kilifi walijitokeza na kuilaumu serikali wakidai kwamba imezembea kulinda usalama wa raia wake kutokana na visa vya mauaji ya mara kwa mara dhidi ya raia.
Wakizungumza nje ya lango la chuo hicho wakiongozwa na Vincent Obondo wanafunzi hao waliitaka serikali kuwachukulia hatua maafisa wote wanaohusishwa na kifo cha Albert Ojwang’ mwanablogu ambaye alikuwa mwanafunzi wa chuo hicho.
Obondo pia alilaumu viongozi wa kisiasa nchini ambao wameonekana kunyamazia kisa hicho cha mauaji ya Ojwang wakisisitiza kujiuzulu kwa Naibu Inspekta Jenerali wa polisi Eliud Laga’t ili kupisha uchunguzi.
“Albert hakujigongesha kwa ukuta jinsi ambavyo polisi wenyewe wanasema, sasa tunauliza serikali ni nini ambayo vijana walifanya ambacho kinakufanya uwachukie hivi, kwa viongozi wetu kwa nini mmenyamaza sana hamjajitokeza waziwazi kuuliza serikali kwa nini wanafanya, tuko hapa kuuliza na kuagiza serikali kuchukua hatua kwa Eliud Laga’t aweze kujiuzulu pamoja na msemaji wa huduma ya kitaifa ya polisi”, walisema wanafunzi hao.

Wanafunzi wa chuo kikuu cha Pwani wakilalamikia mauaji ya Albert Ojwang’
Walidai lalama zote zinaelekezwa kwa Naibu Inspekta jenerali wa polisi Eliud Laga’t hivyo anapaswa kuwajibishwa wakidai hakuna uhuru wa kujieleza nchini na serikali imekuwa ikiendekeza udikteta na kunyamazisha wakosoaji wake.
“Hata hiyo nafasi heri ibaki wazi kuliko yule jamaa awe pale, kwa sababu nchi yetu haiwezi kuwa namna hii, sisi vijana tutajitokeza namna gani kuonyesha tuko salama au hatuko salama, Nasimama hapa nikiwa na wasiwasi sana kwa sababu sijui nitakujiwa lini lakini hatuogopi na ikifika mwaka 2027 tunaambia kila mtu kuwa unakuja kwa kituo cha kupigia kura na vitu viwili, kwanza kitambulisho cha kitaifa na pili akili yako timamu”, waliongeza wanafunzi hao.
Kwa upande wao Wanaharakati wa kutetea haki za binadamu kaunti ya Kilifi wakiongozwa na Mwanase Ahmed, wameitaka serikali kuhakikisha maafisa wote wa polisi wanaohusishwa na visa vya mauaji ya raia kuwajibishwa.
“Sio mara ya kwanza kwa polisi kua wananchi hii kitu inaendelea na hakuna mtu ambaye amekamatwa na kufunguliwa mashtaka tangu mwaka jana, mimi nataka wachukuliwe hatua, tuko na jela, huu ni uhalifu dhidi ya binadamu”, aliongeza Mwanase.
Taarifa ya Joseph Jira