News
Biwot: Familia zilizoathirika na ujenzi wa barabara ya Kilifi-Mtwapa zafidiwa

Idara ya usalama kaunti ya Kilifi imesema serikali inaendelea na zoezi la kufidia familia zilizoathirika na ujenzi wa barabara kuu ya Kilifi kuelekea Mtwapa.
Kamisha wa kaunti ya Kilifi Josephat Biwot alidokeza kuwa kwa sasa maafisa wa shirika la Kenya power wanaendelea kuondoa nyaya za stima ili kutoa nafasi kwa mkandarasi kuendelea na shughuli za ujenzi.
Vile vile Biwot alisema ujenzi daraja mbili kubwa kaunti ya Kilifi unaendelea pamoja na ujenzi wa barabara ya Sabaki Sosoni kueleke Baricho hadi Baolala.
“Ujenzi wa barabara kuu ya Kilifi kuelekea Mtwapa unaendelea vyema, tunachokifanya sasa ni kufidia walioathirika, pia kenya power inaondoa nyaya kupisha mwanakandarasi kuendelea na ujenzi, vile vile ujenzi wa daraja mbili kuu kilifi unaendelea hasa ya Galana Kulalu na Baricho”, alisema Biwot.
Vile vile Kamishna huyo alidokeza kuwa serikali inaendelea na ujenzi wa miradi mbali mbali inayoambatanishwa na sekta ya uchumi wa bahari.
“Upande wa uchumi wa bahari miradi mingi inaendelea mfano ujenzi wa eneo la kuegesha boti kilifi, pia tunajenga makao makuu ya eneo la samaki ya kaunti, tuko na soko la samaki Malindi, tuko na eneo la kuhifadhi samaki la kichwa cha kati ambalo limekamilika na liligharimu shilingi milioni 250”, aliongeza Biwot.
Wakati huo huo wadau wa sekta ya Uvuvi eneo la Ngomeni wakiongozwa na Mwenyekiti wa Ngomeni BMU Said Athman aliitaka serikali kufuatilia kwa kina fedha zinazotolewa na serikali kudaidi miradi ya wavuvi.
“Tunapewa pesa ya makundi kwa mfano shilingi milioni tatu, ile pesa mpaka ikifikia jamii imeliwa, kwa mfano unapewa boti lakini halina vifaa sababu ile pesa imeliwa juu na maofisa mpaka ikifika nyanjani imeisha”, alisema Athman.
Mwenyekiti wa Ngomeni BMU Said Athman akizungumza na wanahabari Kilifi.
Taarifa ya Joseph Jira.
News
IEBC inaendelea kutambua vituo vya kusajili wapiga kura

Maafisa wa tume ya uchaguzi na mipaka nchini IEBC wamesema wanaendelea na zoezi la kutambua sehemu za kuweka vituo vya kusajili wapiga kura hasa maeneo ya mashinani.
Afisa msimamizi wa tume ya IEBC eneo bunge la Ganze kaunti ya Kilifi, Mohammed Bahero Aboud alisema juhudi hizo ni kuhakikisha zoezi la usajili wapiga kura litakaloanza rasmi Septemba 29, mwaka huu linafaulu.
Akizungumza mjini Kilifi, Bahero alisema tume hiyo inatumia mbinu mpya ya kutambua vituo vya jadi vya usajili wapiga kura na kuweka vituo vipya kulingana na mapendekezo ya sheria.
Wakati huo huo alidokeza kwamba tume ya IEBC imekuwa ikihamashisha wakenya kutokubali kushawishiwa na wanasiasa na kujisajili katika maeneo yasiokuwa yao hasa msimu huu ambao zoezi hilo linakaribia kuanza.
Taarifa ya Joseph Jira
News
Kaunti ya Mombasa kukumbatia matumizi ya mfumo wa miale ya jua

Serikali ya kaunti ya Mombasa imesema imeanza kutekeleza mpango wa kutumia nishati mbadala katika vituo vyote vya huduma za kaunti, kwa kuanza na mabadiliko ya mfumo wa taa hadi kutumia umeme wa miale ya jua.
Kwa mujibu wa waziri wa kawi, rasilimali asili na ustahimilivu dhidi ya mabadiliko ya tabianchi kaunti ya Mombasa, Emily Achieng, hatua hii inalenga kupunguza gharama za matumizi ya umeme na kuhimiza matumizi ya nishati safi na rafiki kwa mazingira.
Mbali na hilo, waziri huyo alisema kaunti inaendelea kuweka vifaa maalum vya kupima ubora wa hewa katika maeneo mbalimbali ya mji na ndani ya taasisi za umma.
Lengo ni kupata ushahidi wa kisayansi kuhusu kiwango cha uchafuzi wa hewa, na kuchukuliwa kwa hatua za kisheria kwa wanaokiuka sheria.
Vifaa hivyo tayari vimewekwa katika hospitali ya rufaa ya Coast General na baadhi ya shule ikiwa ni sehemu ya mpango wa muda mrefu wa kaunti, kujenga ustahimilivu dhidi ya madhara ya mabadiliko ya tabianchi.
Mikakati hiyo pia itasaidia kaunti katika kufanya maamuzi kuhusu maeneo yanayofaa kuwekwa biashara fulani, ili kulinda wananchi dhidi ya maradhi yanayosababishwa na uchafuzi wa hewa.
Taarifa ya Mwanahabari wetu.