News
EACC: Wizara ya Usalama na Afya zaongoza kwa ufisadi

Utafiti mpya wa kitaifa uliofanywa na Tume ya maadili ya kupambana na ufisadi nchini EACC umeonya wakenya dhidi ya vitendo visivyo vya kimaadili na ufisadi katika Wizara ya usalama wa ndani na taasisi nyingine za umma.
Kulingana na utafiti wa mwaka 2024 wa tume hiyo, asilimia 47.8 ya wakenya waliotangamana na Wizara ya usalama wa ndani waliripoti kupitia au kushuhudia vitendo vya ufisadi au visivyo vya kimaadili.
Hali hii inaifanya Wizara hiyo kuwa na kiwango kikubwa cha matukio kama haya.
Wizara ya Afya nchini ilishika nafasi ya pili kwa asilimia 19.7, huku hazina ya kitaifa ikifuata kwa mbali kwa asilimia 5.8.
Taasisi nyingine za umma zilizojitokeza kwa wingi ni pamoja na wizara ya Ardhi kwa asilimia 5.6, uchukuzi kwa asilimia 3.9, na elimu kwa asilimia 2.6.
Utafiti huo uliofanywa kati ya Agosti na Oktoba 2024, uliwashirikisha zaidi ya watu 6,000 kote nchini na ulilenga kuelewa mitazamo na uzoefu wa wananchi kuhusiana na rushwa na maadili katika utumishi wa umma.
Ripoti hiyo ilifichua kuwa wakenya bado wanakabiliana na viwango vya juu vya hongo na tabia isiyofaa katika taasisi za umma.
Pia ilifichua hali inayotia wasiwasi ambapo rushwa inazidi kuonekana kama uovu muhimu katika kupata huduma za umma.
Ripoti hiyo pia ilibainisha kuwa wananchi wengi wanahisi wamenaswa katika mzunguko wa unyang’anyi na kuogopa kudhulumiwa ikiwa watazungumza.
Kaunti ya Nairobi iliongoza orodha ya vitengo vya ugatuzi ambapo wakaazi waliripoti kukabiliwa na visa vya juu zaidi vya ufisadi, ikifuatiwa na Kiambu, Machakos, Kisumu na Nakuru.
Tume hiyo iliwataka watumishi wa umma kuzingatia maadili ya uadilifu, uwazi na uwajibikaji katika kutoa huduma kwa Wakenya.
Taarifa ya Joseph Jira
News
Mahakama ya Kilifi imetoa hukumu kwa wanaume 6 wanaokabiliwa na mashtaka ya unajisi

Mahakama ya Kilifi imetoa hukumu kwa wanaume 6 wanaokabiliwa na mashtaka ya unajisi.
Hakimu wa Mahakama hiyo Ivy Wasike alimhukumu Lucky Munga na Hassan Daniel kifungo cha miaka 30 gerezani baada ya Mahakama kubaini kwamba walihusika kwa kuwatendea unyama watoto wa umri wa miaka 13 na 15.
Safari Karisa Lewa alihukumiwa kifungo cha miaka 15 gerezani kwa kumnajisi mtoto wake mwenyewe wa umri wa miaka 14 huku Eric Ruwa na Lucky Katana Kenga wakihukumiwa kifungo cha miaka 6 gerezani kwa kosa sawa na hilo.
Hata hivyo Mahakama hiyo ilimhukumu kifungo cha miaka 3 Kithi Kombe kutokana na kesi hiyo kwa mtoto wa miaka 15, japo baadaye Mahakama ikabaini kwamba mshukiwa sio baba halali wa mtoto aliyezaliwa baada ya Kithi kumnajisi mtoto huyo.
Akizungumza wakati wa vikao vya Mahakama baada ya kutoa hukumu hizo, Hakimu Wasike alisema Mahakama umezingatia ushahidi uliyotolewa Mahakamani huku akiwarai wananchi kujitenga na visawishi vibaya ili kuepuka mkono wa sheria.
Hakimu Wasike alihoji kwamba washtakiwa wa haki ya kukata rufaa dhidi ya uamuzi wa Mahakama lakini kwa kuzingatia taratibu zote za Mahakama na sheria.
Taarifa ya Teclar Yeri
News
Thoya: Serikali kuu iongeze mgao wa fedha kwa sekta ya Afya

Naibu gavana wa kaunti ya Mombasa Francis Thoya ametoa changamoto kwa serikali kuu kuongeza mgao wa fedha ili kufanikisha utaoji wa huduma za afya.
Akizungumza katika kaunti hiyo, Thoya alisema kuwa huduma nyingi za afya katika kaunti hiyo ya Mombasa zinakabiliwa na changamoto ya raslimali ndogo hali ambayo inakwamisha juhudi za kuwahudumia wananchi ipasavyo.
Thoya pia alitaka serikali kuhakikisha inaharakisha kuajiri wahudumu zaidi wa afya ili wenyeji wa Mombasa waweze kupata huduma bora za matibabu bila changamoto zozote.
Aidha, Thoya alisema kwamba hali ya uhaba wa wahudumu wa afya ni changamoto kuu ambayo inazuia utoaji wa huduma bora za matibabu hali inayowafanya wale wachache waliopo kufanya kazi katika mazingira magumu.
Taarifa ya Janet Mumbi