News
Chibule, apendekeza adhabu kali kwa wanaoendeleza dhulma za kijinsia

Naibu gavana kaunti ya Kilifi Flora Mbetsa Chibule, amependekeza adhabu kali kwa watu wanaotekeleza visa vya dhulma za kijinsia katika jamii.
Chibule alisema visa vya dhulma za kijinsi dhidi ya watoto vimekithiri katika jamii hasa kaunti ya Kilifi, akiahidi ushirikiano wa hali ya juu na wadau mbalimbali ili kukomesha visa hivyo.
Akizungumza wakati wa maadhimisho ya hamasa kuhusu dhulma za kijinsia katika uwanja wa Bofa Youth mjini Kilifi, Chibule alisema ili kufanikisha ndoto ya mtoto wa kike ni lazima haki zao za kimsingi zilindwe.
“Kwa ambao wanadhulumu mtoto wa kike na kiume, kwa wale ambao wanaingia misuli kwa misuli wanafaa kuwekwa gerezani kabisa”, alisema Chibule.

Wanaharakati wa kijamii wapinga unyanyasaji wa kijinsi, Kilifi
Kwa upande wake Mwakilishi wa kike kaunti ya Kilifi Getrude Mbeyu aliyeandaa hafla hiyo kupitia hazina ya kitaifa ya NGAAF na kutoa hundi ya kima cha shilingi milioni 1.6 kwa makundi 14, alisisitiza hamasa zaidi kwa jamii kuhusu jinsi ya kukomesha visa hivyo.
“Ni jukumu letu la kuwaeleza hawa watu watambua jinsi ya kuripoti hizi kesi, yani kwa mfano umedhulumiwa ni wapi pa kuanzia na hatua hii itakomesha hizi visa”, alisema Mbeyu.
Naye Mzee wa mataa wa Kiwandani mjini Kilifi Elina Nyevu alisema visa vya dhulma za kimapenzi vimekithiri mno katika mtaa huo, akipendekeza hamasa zaidi kwa jamii.
“Hapa kwetu Kiwandani visa vya dhulma za kijinsia ni vingi sana, kuna ulevi na ukosefu wa ajira ambao umechangia utumiaji wa Mihadarati na unyanyasaji wa watoto wadogo kimapenzi, alisema Elina.
Hata hivyo katika halfa hiyo baadhi ya watoto waliopitia madhila hayo hasa ubakaji wameelezea masaibu waliopitia japo haki yao kupitia idara ya usalama walikosa kufaulu.
Taarifa ya Lolani Kalu.
News
Wakaazi wa Voi waonywa dhidi ya ugonjwa wa MPOX

Daktari wa magonjwa ya kuambukiza katika hospitali ya rufaa ya Moi mjini Voi katika kaunti ya Taita Taveta Urbanius Kioko amewataka wenyeji wa kaunti hiyo kuzingatia maagizo ya Wizara ya Afya ili kujikinga dhidi ya maambukizi ya ugonjwa wa Mpox.
Akiongea kwenye warsha ya Wanahabari iliyofadhiliwa na Shirika la Stawisha Pwani, Daktari Kioko alisema wananchi wanapaswa kujikinga ili kudhibiti ugonjwa huo kuenea.
Kioko pia aliwataka wale ambao wana dalili za ugonjwa huo kufika kwenye vituo vya afya ili kutibiwa.
“Huu ugonjwa huwa unaenezwa kupitia kutangamana, kuvaa nguo za mwenzako na kupitia hewa wakati wa kuongea’’, alisema Kioko.

Wadau wa sekta ya Afya katika kikao na Wanahabari mjini Voi
Vilevile, Kioko alitaja kisa cha mgonjwa mmoja wa Mpox kilichothibitishwa siku ya Jumanne wiki hii mjini Voi huku visa vingi vikishamiri katika kaunti Mombasa.
Haya yanajiri huku Wizara ya Afya nchini ikishinikiza wananchi kujiepusha kula nyama za Wanyamapori miongoni mwa tahadhari zingine kama njia mojawapo ya kukabiliana na maambukizi ya ugonjwa wa Mpox.
Taarifa ya Janet Mumbi
News
Mzozo kati ya Kenye na Tanzania waendelea kutokota

Serikali ya Kenya imeiandikia barua jumuiya ya afrika mashariki kupinga vikwazo vilivyowekwa na Tanzania kuhusu kufanya biashara katika taifa hilo.
Katibu mkuu katika idara ya EAC Daktari Caroline Karugu, alisema kenya imebaini kuwa agizo hilo haliambatani kamwe na masharti muhimu ya itifaki ya soko la pamoja la EAC, ambayo inahakikisha uruhu wa watu kusafiri, kuhudumu na haki ya kuanzishwa kwa biashara na raia wa mataifa ya afrika mashariki.
Aidha Kenya iliasema imeandika rasmi barua kwa EAC kuiarifu rasmi jamhuri ya muungano wa Tanzania kuangazia upya agizo hilo ili kuhakikisha inafuata kikamilifu mkataba wa EAC na sheria za Jumuia.
Maafisa wa EAC kwa sasa wanafanya uchambuzi wa hatua hiyo na itawasilisha hatua zozote zilizokiukwa pamoja na kaununi zilizopo katika mkutano ujao wa baraza la kisekta la biashara, viwanda na uekezaji.
Taarifa ya Joseph Jira