News
Biwott: Polisi waendelea kuwasaka waumini wenye itikadi potovu

Kamanda wa Polisi kaunti ya Kilifi Josephat Biwott amepongeza juhudi za wakaazi wa kaunti hiyo kwa kuwa na ushirikiano mwema na asasi za usalama.
Biwott amesema ni kupitia ushirikiano huo ambapo oparesheni ya kuwanasa waumini wa dini potofu eneo la Binzaro, kilomita chache kutoka eneo la Shakahola imefanikiwa kutokana na juhudi za wakaazi kutoa taarifa kwa maafisa wa usalama.
Akizungumza na Coco Fm, Biwott alithibitisha kwamba eneo la Chakama lipo chini ya ulinzi wa polisi.
Biwott alidhitisha kuwa washukiwa 11 tayari wamekamatwa na wamefikishwa Mahakamani Jumanne 22 Julai 2025 mbele ya Hakimu Mwandamizi Joy Wesonga na wataendelea kuzuiliwa katika kituo cha Polisi mjini Malindi.
Biwott aidha alisema maafisa wa usalama wanachunguza iwapo washukiwa hao walienda msituni wakiwa na watoto.
“Nawashukuru wananchi wetu hasa wakaazi wa Binzaro, kwa kutueleza kwa mapema sana kuhusu yale mambo yalikua yanaendelea huko kwa vile wametueleza tumefaulu kuokoa wale ambao tumeokoa na wanaoendelea dini hiyo tumewakamata na wamefikishwa mahakamani”. …alisema Biwott, kwa njia ya simu.
Tarifa ya Elizabeth Mwende
News
NACADA yapendekeza sheria mpya ya kudhibiti pombe

Mamlaka ya kukabiliana na dawa za kulevya na pombe haramu nchini NACADA inaendelea kushikilia pendekezo lake la kutaka umri wa chini wa unywaji wa pombe uwe wa miaka 21.
Mratibu wa Mamlaka hiyo kaunti ya Mombasa, Wangai Gashoka alisema pendekezo hilo limetokana na ongezeko la vijana wadogo wanaotumia pombe kupindukia.
Wangai alisema kuwa utafiti wa NACADA ulionyesha wazi kwamba akili ya binadamu huendelea kukua hadi miaka 25 hivyo mtu akinywa pombe akiwa na umri mdogo huongeza hatari ya uraibu wa mapema.
NACADA sasa inashinikiza pendekezo hilo kufanywa kuwa sheria ambayo itaidhinishwa bungeni na kuanza kutekelezwa kikamilifu.
Ni hatua ambayo ilipigiwa upato na wakereketwa wa kukabiliana na utumizi wa dawa za kulevya akiwemo Famau Mohamed Famau ambaye alisisitiza haja ya mapendekezo hayo kutopuuziwa.
Taarifa ya Hamis Kombe
News
Philip Charo ateuliwa kaimu waziri wa barabara Kilifi

Gavana wa kaunti ya Kilifi Gideon Mung’aro amefanya mabadiliko katika serikali yake na kumteua afisa mkuu mtendaji wa idara ya barabara Philip Charo kuwa kaimu waziri katika idara ya barabara.
Hii ni baada ya kuchaguliwa kwa aliyekuwa waziri wa idara hiyo Catherine Kenga kuwa spika wa bunge la kaunti ya Kilifi.
Katika taarifa kupitia msemaji wa kaunti Johnathan Mativo, afisa mkuu mtendaji wa idara ya maswala ya fedha Hezekiah Mwaruwa pia aliteuliwa kuwa afisa mkuu mtendaji katika ofisi ya gavana.
Mativo alisema kwamba mabadiliko hayo yanaanza kutekelezwa mara moja ingawa ni ya mda.
Catherine Kenga alijiunga na utumishi wa serikali ya kaunti ya Kilifi mnamo mwaka 2023 baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2022 uliopelekea kuchaguliwa kwa gavana Gideon Maitha Mung’aro.
Pia amewahi kuhuduma kama kaimu katibu wa kaunti baada ya kutimuliwa kwa Martin Mwaro.
Catherine Kenga alichaguliwa kuwa spika wa bunge la kaunti ya Kilifi katika kikao maalum ambacho kiliandaliwa katika bunge hilo Jumatu Julai 21 2025.
Kenga anachukua hatamu ya kuliongoza bunge hilo kutoka kwa aliyekuwa spika Teddy Mwambire ambaye alitimuliwa mapema mwezi uliopita Juni 30, 2025 kupitia kura ya maoni.
Mwambire alibanduliwa kwa tuhuma za matumizi mabaya ya ofisi na ukiukaji wa katiba.
Taarifa ya Joseph Jira