News
Baraza la vyombo vya habari MCK lakerwa na baadhi ya vyombo habari

Baraza la vyombo vya habari nchini MCK limeeleza kusikitishwa na hatua ya baadhi ya vyombo vya habari nchini kumwingilia rais wa chama cha mawakili LSK Faith Odhiambo baada ya kukubali kujumuishwa kwenye kamati ya kuangazia fidia kwa waathiriwa wa maandamano nchini.
MCK ilisema hatua ya Odhiambo kujumuishwa katika kamati hiyo kuhakikisha waathiriwa wa maandamano hayo wanapata haki kwa mujibu wa sheria.
Katika taarifa kwa vyombo vya habari, baraza hilo lilipongeza juhudi za vyombo vya habari kwa kuangazia kwa undani maandamano yaliyofanyika nchini na hata baadhi ya wanabari kujitokeza kutoa ushahidi mahakamani.
MCK ilisema hatua ya baadhi vyombo vya habari kukosoa mwelekeo wa Odhiambo kunaiweka LSK katika hatari ya ukosoaji zaidi, katika juhudi za kuangazia usawa kwenye maswala ya uongozi dhabiti nchini.
Taarifa ya baraza la vyombo vya habari nchini MCK.
Ilieshinikiza wakenya kufahamu kuwa chama cha LSK kinaongozwa na taasisi muhimu za umma ikiwepo idara ya mahakama, ofisi ya mkurugenzi mkuu wa mashtaka ya umma, ofisi ya mkuu wa sheria nchini vile vile tume ya malalamishi kwa vyombo vya habari.
MCK ilivitaka vyombo vya habari kumruhusu Odhiambo kuendelea kutekeleza majukumu yake bila muingilio katika kamati hiyo.
Taarifa ya Joseph Jira
News
Maandalizi ya Maadhimisho ya Chenda Chenda

Ni dhahiri sasa kutakuwa maaadhimisho ya Chenda Chenda siku ya Jumanne Septemba 9, 2025 kwa wakati mmoja katika kaunti ya Kwale na kaunti ya Kilifi.
Waasisi wa maadhimisho haya ambao ni wWazee wa kutoka Kaya zote za Wamijikenda walitangaza mwaka uliopita kwamba maadhimisho ya mwaka huu yafanyika katika kaunti ya Kwale baada ya kuandaliwa eneo la Kaya fungo kaunti ya Kilifi mwaka jana.
Na baada ya vikao vya mashauriano baina ya Wazee wa Kaya zote hivi majuzi katika eneo la Rabai, Wazee hao waliafikiana kwa kauli moja kwamba maadhimisho hayo ya mwaka huu yaandaliwe katika Kaya ya Mtswakara eneo bunge la Kinango katika Kaunti ya Kwale.
Lakini baada ya tangazo hilo kutolewa, serikali ya kaunti ya Kilifi ilitangaza kufanya maadhimisho hayo katika uwanja wa chuo kikuu cha Pwani.
Tangazo hilo liliwaghadhabisha mno Wazee wa Kaya ambao katika taarifa kwa Wanahabari walisema wanaendelea na mipango ya maadhimisho hayo katika kaunti ya Kwale.

Maandalizi ya Maadhimisho ya Chenda Chenda, kaunti ya Kilifi
Hali hii imezua tofauti kubwa baina ya Gavana wa kaunti ya Kilifi Gedion Maitha Mung’aro anayedaiwa kuenda kinyume na utaratibu wa tamaduni za Kaya, ambapo maadhimisho hayo yanapasa kufanyika katika viwanja vya Kaya kama njia moja ya kuwaheshimu wavyele wa Kaya za Kimijikenda.
Huku hayo yakijiri maandalizi ya maadhimisho hayo yanaendelea katika uwanja wa Chuo kikuu cha Pwani.
Wazee wa Kaya wanalaumu kitendo hiki na kuongeza kwamba maandalizi haya yanamsukumo wa kisiasa na wala sio ule wa kitamaduni na unaokusudiwa kuleta umoja wa Wamijikenda.
Taarifa ya Eric Ponda
News
Jopo la kushughulikia fidia kwa waathiriwa wa maandamano laanza kazi

Jopo lililoundwa na Rais William Ruto kushughulikia masuala ya fidia ya waathiriwa wa ukatili wa polisi wakati wa maadamano limeanza kikao cha wiki moja huku mjadala kuhusu uhalali na uwazi wa jopo hili ukitiliwa shaka na kupokea upinzani mkali kutoka kwa baadhi ya wanaharakati wa kutetea haki za kibinadamu na viongozi wa upinzani.
Jopo hilo linaongozwa na Prof. Makau Mutua na naibu wake Rais wa Chama cha Wanasheria nchini (LSK), Faith Odhiambo, ambaye uteuzi wake umeibua mjadala mkali.
Baadhi ya Wanasheria walimshutumu Odhiambo kwa “kusaliti haki,” lakini yeye alisisitiza kwamba jukumu lake ni kuhakikisha waathiriwa wa ukatili wa polisi wanapata haki waliyoikosa kwa muda mrefu.
Aliongeza kuwa jopo hilo lina nafasi ya kuleta mabadiliko ya kihistoria katika upatikanaji wa fidia kwa waathiriwa.
Kwa mujibu wa maelezo yake, jopo hilo si tume ya kikatiba wala chombo cha kisheria chini ya Katiba, bali ni jopo la ushauri lililoanzishwa na Rais chini ya Kifungu cha 132(4)(a).
Vile vile alibainisha kuwa wanachama wa jopo hilo si maafisa wa umma hivyo uteuzi wao hauhitaji mchakato wa Tume ya Utumishi wa Umma kwa mujibu wa Kifungu cha 260 cha Katiba.

Jopo lililoundwa na Rais William Ruto kushughulikia ya fidia ya waathiriwa wa maadamano
Hata hivyo, wakosoaji walisema linaweza kukiuka mamlaka ya ofisi huru kama Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (DPP), Inspekta Jenerali wa Polisi na Tume ya Kitaifa ya Haki za Binadamu (KNCHR). Jopo hilo limekanusha madai hayo, likisema jukumu lake ni kusaidia na sio kuchukua nafasi ya taasisi zilizopo.
Wapo pia wanaouliza uhalali wa serikali kuwalipa fidia waathiriwa ilhali serikali hiyo hiyo imeshtumiwa kwa mauaji, kutoweka kwa baadhi ya wakosoaji wa serikali kwa njia tatanishi na kuacha familia na majeraha yasiyotibika.
Jopo hilo pia linasisitiza kikatiba, serikali ndiyo chombo kinachobeba wajibu wa kurekebisha madhila kwa niaba ya taifa. Hata kama madhara yalisababishwa na maafisa wa serikali, haitazuiwa kuwafidia waathiriwa.
Taarifa ya Elizabeth Mwende