News
Kenya Yatoa ufadhili wa Asilimia 20 kwa WHO

Kenya imejitolea kuongeza ufadhili wake kwa Shirika la Afya duniani WHO kwa asilimia 20 katika kipindi cha miaka 4 ijayo.
Waziri wa Afya nchini Aden Duale ameyasema hayo wakati wa Kongamano la 78 la Afya duniani linaloendelea mjini Geneva nchini Uswizi, ambapo amesisitiza haja ya serikali ya Kenya kujitolea katika kuboresha sekta ya afya ulimwenguni.
Waziri Duale amesisitiza umuhimu wa ufadhili endelevu kwa Shirika la Afya duniani WHO, akisema licha ya bajeti kurekebishwa na kuweka ufadhili huo mdogo pia utasaidia sekta ya afya.
Waziri Duale ameangazia dhamira ya serikali ya Kenya ya kuhakikisha wananchi wananufaika na huduma za afya kwa wote UHC, kuimarishwa kwa ufadhili wa afya na kuendeleza miundombinu ya afya ya kidijitali ili kuendesha sera inayotumia data.
Kwa upande wake Mkurugenzi mkuu wa WHO Dkt Tedros Adhanom Ghebreyesus amepongeza kujitolea kwa mataifa wanachama katika kufadhili WHO, akisema ahadi zilizotolewa na mataifa hayo zitachangia kuimarika kwa sekta ya afya duniani.
News
Kimotho: Deni lililosalia kwa waathiriwa wa bwawa la Mwache ni shilingi bilioni 2

Serikali imesema itakamilisha malipo ya fidia kwa waathiriwa wote wa ujenzi wa mradi wa Bwawa la Mwache katika eneo la Kinango kaunti ya Kwale ifikapo mwishoni mwa mwaka huu.
Katibu katika Idara ya unyunyizaji maji nchini Ephastus Kimotho amesema deni lililosalia kwa waathiriwa wa mradi huo ni shilingi bilioni 2 na tayari limeanza kulipwa.
Kimotho amesema hatua hiyo imeafikiwa baada ya Tume ya kitaifa ya ardhi NLC kupewa shilingi milioni 600 ambazo zitapewa waathiriwa kama fidia kuanzia wiki ijayo.
Akizungumza baada ya kutembelea mradi huo sawa na kuzindua kituo cha afya cha Mazeras kinachojengwa kama sehemu ya mradi huo, Kimotho amesema fedha zilizosalia zitaanza kutolewa kuanzia mwezi Julai ili kuafikia mipango iliyowekwa.
“Kufikia mwezi Julai mwaka huu tutakuwa tumeanza kusambaza mgao mwengine wa fedha zilizosalia ili kukamilisha fidia hizo kufikia mwezi Disemba mwaka huu”, alisema Kimotho.
Shughuli za ujenzi wa Bwawa la Mwache
Kwa upande wake Gavana wa Kwale Fatuma Achani amesema mradi huo uko na manufaa mengi kwa wakaazi wa kaunti ya Kwale ikiwemo ujenzi wa vituo vya afya, shule, miongoni mwa manufaa mengine.
“Tumeona manufaa mengi kupitia mradi huu, umeleta vituo vya afya karibu na wananchi, ujenzi wa shule za Chekechea na miradi mingi muhimu ya umma, hivyo basi tunafaa kuunga mkono kikamilifu”, alisema Gavana Achani.
Mradi huo ambao ulikuwa umetengewa shilingi bilioni 4.6 kama fidia ya wakaazi waliopeyana ardhi zao kwa ujenzi wa mradi huo zimekuwa zilipiwa kwa njia ya awamu hali ambayo ilisababisha maandamano kutokana na kucheleweshwa kwa fidia hiyo.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
News
Watu watatu wakamatwa katika Mahakama ya Milimani

Watu watatu wanaodaiwa kuwa wafanyakazi wa kaunti ya Trans Nzoia wamekamatwa na maafisa wa polisi waliokuwa wamevalia sare baada ya kusikiza kesi inayomkabili gavana wa kaunti hiyo George Natembeya katika Mahakama ya Milimani jijini Nairobi.
Watatu hao walikamtwa mda mfupi baada ya Jaji Zipporah Gichana, kuagiza upande wa mashtaka kuwasilisha ushahidi dhidi ya kesi ya ufisadi inayomkabili gavana huyo.
Agizo hilo lilifuata tamko la upande wa mashtaka kwamba ilifeli kufuta agizo la awali la Mahakama la kuwasilisha ushahidi.
“Nyaraka na taarifa hizo zilipaswa kuwa zimetolewa kufikia sasa, kwa hiyo ninaelekeza upande wa mashtaka kufuata maagizo ya awali”, aliagiza Jaji Gichana.
Upande wa mashtaka uliomba mda wa wiki mbili zaidi ili kutii maagizo ya awali ya kuwasilisha ushahidi wa nyaraka.
“Hati nyingi zinapatikana kutoka kaunti ya Trans Nzoia na tumeshindwa kuzipata, tunaomba wiki mbili za ziada ili kutii,” Wakili wa Serikali Victor Awiti aliwasilisha.
Hata hivyo, upande wa utetezi ulipinga ombi hilo, ukisema ni sawa na matumizi mabaya ya mchakato wa Mahakama.
Upande wa mashtaka uliamriwa kufichua nyenzo zote husika kabla ya Juni 16 kesi hiyo itakapotajwa.
Taarifa ya Joseph Jira