News
Wahudumu wa Sekta ya Uchukuzi Wanahimiza Ukarabati wa Barabara ya Kibaoni-Ganze-Bamba

Wahudumu wa sekta ya uchukuzi mjini Kilifi kaunti ya Kilifi wanashinikiza serikali kuu na ile ya kaunti kuzingatia ukarabati wa barabara ya Kibaoni-Ganze hadi Bamba licha ya kushinikizwa kusitisha maandamano ya kufunga barabara hiyo.
Wakizungumza na Coco FM, wahudumu hao wamesema barabara hiyo ingali na hitilafu nyingi na wanahofia huenda ikaharibika vibaya msumu huu wa mvua.
Wakiongozwa na Praise Majimbo ambaye ni mhudumu wa bodaboda, wamesema hatua ya kulima barabara hiyo kwa tinga tinga haitoshi kwani bado kuna vumbi na mashimo hali inayowatatiza shughuli zao za kibiashara.
“Kwa sasa kidogo iko na afadhali lakini bado hatujaridhika na kile chenye tunapitia, kwa sababu kwengine kushatengenezwa na mvua imenyesha tayari sasa hivi mashimo yako mengi, vyenye niko tayari nyewe nimechoka kutoka Kakanjuni mpaka barabara vyenye iko kwa ukweli, vumbi na mashimo pia yashaongezeka kwa sababu ya mvua”, alisema Majimbo.
Nao wahudumu wa magari ya uchukuzi wa umma wakilongozwa na Samson Kitsao Wako, wanasema wanapitia changamoto za kukarabati magari yao kila mara kutokana na hali mbaya ya barabara hiyo.
“Lakini kwa saa tutasema inaafadhali kwa sababu, tuliandamana na tukafunga na baadaye serikali ikaleta tinga tinga ikapiga msasa kutoka hapa Kibaoni mpaka Silala, lakini sasa kutoka Ganze mpaka Bamba ndio barabara ni mbaya sana, mvua ikianza kunyesha tutapata shida sana kwa sababu barabara wakati wa mvua hua inateleza”, alisema Kitsao.
Vile vile wachuuzi wa vyakula kando ya barabara hiyo Wakiongozwa na Fiki Kenga wanasema idadi ya wateja imekuwa ikipungua kutokana na vumbi linalotoka barabarani kila mara, wakisinikiza serikali kuzingatia kilio chao.
“Tunapata taharuki hata vyakula vyetu huwa haviendi vizuri kila siku, hii barabara ilifanya kukwaruzwa kwaruzwa huko, angalau tusiumizwe na hili vumbi, barabara iko na vumbi wateja wanalalamika kwa sababu vumbi si nzuri kwa chakula, kwa hivyo tunaomba msaada tuwe nasi tutakaa vizuri mahali tuko”, waliongeza baadhi ya wachuuzi.
Aidha wameshinikiza serikali kuangazia matatizo wanayopitia baadhi yao wakidai wanawake wajawazito wamekuwa wakipoteza watoto wachanga hasa wanaposafirishwa kwa pikipiki kuelekea hospitali kujifungua kutokana na ubovu wa barabara hiyo.
Itakumbukwa kwamba wakaazi pamoja na wahudumu wa uchukuzi wa umma waliandamana na kufunga barabara hiyo kwa majuma kadhaa na kutatiza shughuli za usafiri.
News
Kadinali Bacciu Atangaza Kutohudhuria Kikao cha Conclave

Kadinali Giovanni Angela Bacciu ametangaza kujiondoa katika kikao cha siri cha kumchagua Papa mpya kilichopangwa na Ofisi ya Vatican kuanza rasmi mwezi Mei 7.
Katika taarifa yake aliyoitoa kupitia Wakili wak siku ya Jumanne tarehe 29, Kadinali Bacciu amesema ameamua kutii wasia ulioweka wa Hayati Papa Francis ingawa alidumisha kutokuwa na hatia.
“Kwa kuwa moyoni mwangu nina wema wa Kanisa ambalo nimelitumikia na nitaendelea kulitumikia kwa uamunifu na upendo na kuchangia ushirika na utulivu wa Conclave, nimeamua kutii kama nilivyofanya siku zote wakati wa Papa Francis na nitasalia kuamini kwamba sina hatia”, alisema Kadinali Bacciu.
Kadinali Bacciu mwenye umri wa miaka 78 na mzaliwa wa taifa la Italia amegongwa vichwa vya habari kutokana na msimamo wake huku baadhi ya wachanguzi wakisema uamuzi wake umetokana na sintofahamu zilizokuwepo kati yake na Hayati Papa Francis mwaka wa 2020 baada ya kuagizwa na Papa Francis kujiuzulu kwa kupatikana na kashfa ya ufisadi.
News
Mbogo: Kaunti ya Mombasa Imeshindwa Kutatua Mzozo wa Ardhi

Aliyekuwa mbunge wa Kisauni Ali Mbogo ameikosoa serikali ya kaunti ya Mombasa kwa kushindwa kutatua suala tata la uskwota linalowakumba wakaazi wengi wa kaunti hiyo.
Akizungumza katika eneo la Kisauni katika kaunti ya Mombasa, Mbogo amesema tatizo la uskwota limeendelea kuwa chanzo kikuu cha migogoro ya ardhi na ukosefu wa usalama katika maeneo mengi ya kaunti ya Mombasa huku serikali ya kaunti hiyo ikionekana kulifumbia macho suala hilo.
Mbogo amedai kwamba maelfu ya wakaazi wa Kisauni na Mombasa kwa jumla wanaishi kwa hofu ya kufurushwa katika ardhi zao walizoishi tangu jadi kufuatia ukosefu wa hati miliki.
Wakati huo huo amedokeza kwamba baadhi ya maafisa wa serikali ya kaunti hiyo wanahusishwa na visa vya uporaji wa ardhi za umma kwa kushirikiana na waekezaji jambo ambalo amelitaja kuwa dhulma.