News
Kikao cha Kusafisha eneo la Owino Uhuru Chachukua Mkondo tofauti

Mamlaka ya Mazingira nchini NEMA imefanya kikao na waathiriwa wa sumu ya Lead kutoka kijiji cha Owino Uhuru eneo bunge la Jomvu kaunti ya Mombasa ili kuwaeleza jinsi zoezi la kusafisha mazingira litakavyotelekelezwa katika kijiji hicho.
Kikao hicho kilichofanyika katika mtaa wa mataa ya ndege na wala sio eneo la Owino Uhuru kama ilivyoratibiwa awali kutokana na sababu za kiusalama, idadi ndogo ya wakaazi ndiyo waliyojitokeza kuhudhuria kikao hicho.
Akizungumza wakati wa kikao hicho, Mkurugenzi wa uzingatiaji na utekelezaji katika Mamlaka ya NEMA Robert Orina amekanusha madai yaliyoibuliwa kwamba mda uliyopewa Mamlaka ya NEMA wa kusafisha mazingira umepita, akiwataka wakaazi kushirikiana na mamlaka hiyo.
Kwa upande wake Mwakilishi wadi ya Mikindani kaunti ya Mombasa Jackton Madialo amewataka wakaazi kujiepusha na propaganda, na badala yake kuhakikisha wanaipa Mamlaka ya NEMA nafasi ya kusafisha mazingira ya Owino Uhuru.
Hata hivyo wakaazi waliohudhuria kikao hicho wakiongozwa na Samuel Obwaka wameeleza kuridhishwa na hatua ya NEMA kusafisha eneo hilo, wakiwataka wenzao kushirikiana na NEMA kutekeleza zoezi hilo.
News
Amref, yaikabidhi kaunti ya Kilifi vifaa ya matibabu vya milioni 13.2

Shirika la Afya la AMREF kwa ushirikiano na serikali ya kaunti ya Kilifi wawekeza zaidi katika sekta ya afya ili kukabiliana na magonjwa yaliyosaulika.
Shirika hilo limeikabidhi serikali ya kaunti ya Kilifi vifaa vya matibabu vya thamani ya shilingi milioni 13.2 ili kuwawezesha wahudumu wa afya kutathmini magonjwa mbalimbali yaliyosaulika na kuboresha sekta ya afya mashinani.
Mkurugenzi wa Shirika la Afya la AMREF humu nchini Daktari Ndirangu Wanjuki, amesema vifaa hivyo vitasaidia katika kubaini magonjwa yaliyosaulika kama vile Kichocho na kuwawezesha wahudumu wa afya kuwahuhudumia wagonjwa ipasavyo.
Akizungumza wakati wa halfa ya kupokea vifaa hiyo katika hospitali kuu ya rufaa ya Kilifi, Gavana wa kaunti Kilifi Gedion Mung’aro amesema vifaa hiyo vitasambazwa katika hospitali na zahanati 15 za kaunti hiyo.
Gavana Mung’aro amesema magonjwa kama vile Kichocho na Matende miongoni mwa wagonjwa mengine yatagunduliwa kwa urahisi na kutibiwa kwani mengi husababishwa na viini kwenye maji machafu hasa kandokando ya mito.
News
Wakaazi wa Matano Mane Walalamikia Ubovu wa Barabara

Wakaazi wa maeneo ya Matano Mane katika wadi ya Sokoke kaunti ya Kilifi wameandamana na kufunga barabara ya kutoka Chuo cha ufundi cha Godoma inayopitia shule ya upili ya Vitengeni Baptist hadi Vitengeni Mjini wakilalamikia ubovu wa barabara hiyo.
Wakaazi hao wakiongozwa na Dan Mwangome, wamesema barabara hiyo imesalia kwa muda mrefu bila ya kukarabatiwa hali ambayo inatatiza shughuli za kibiashara na uchukuzi wa umma.
Wakaazi hao sasa wanasema mvua inazoendelea kuonyesha imesababisha shughuli za uchukuzi kukatizwa mara kwa mara huku viongozi wa eneo hilo wakishindwa kuwajibikia majukumu yao.
Wakati huo huo wakaazi hao wamemkosa Wanakandarasi aliyepewa zabuni ya ujenzi wa barabara hiyo kwa kuzembea kuwajibikia majukumu yake ya kujenga barabara hiyo.