News
Mahakama ya Shanzu Imeagiza Mshukiwa wa Ugaidi Kuzuiliwa kwa Siku 14

Mahakama ya Shanzu katika kaunti ya Mombasa imeagiza mshukiwa wa kundi la kigaidi la Al-Shabab Ramadhan Mohammed Hassan kuzuiliwa kwa siku 14 zaidi ili kuwawezesha maafisa wa Idara ya upelelezi kukamilisha uchunguzi wao.
Mahakama imeelezwa kwamba Hassan alikamatwa katika eneo la Kichangii katika gatuzi dogo la Nyali kaunti ya Mombasa akiwa na vifaa vinavyodaiwa kutumiwa na kundi la Al-shabab kutekeleza mashambulizi.
Maafisa hao wa idara ya upelelezi wameeleza Mahakama kwamba simu ya mshukiwa ilipelekwa katika makao makuu ya kitengo cha kupambana na ugaidi nchini ATPU kwa uchunguzi zaidi.
Kulingana na maafisa hao, baada ya kufanya uchunguzi wa simu ya mshukiwa wamebaini kwamba mshukiwa alikuwa akiwasiliana na wanachama wengine wa kundi la kigaidi la Al-shabab ambao wako mafichoni katika mataifa ya Tanzania na Somalia.
Hata hivyo maafisa hao wameitaka Mahakama kutomuachilia mshukiwa huyo kwa dhamana, wakisema kwamba huenda akatoroka na kuathiri uchunguzi wa kesi hiyo, ombi ambalo Mahakama imelikubali.
Kesi hiyo itatajwa tena tarehe 16 mwezi huu.
News
Ruku: Serikali kuajiri vijana laki moja kwa NYS

Serikali inalenga kuajiri zaidi ya vijana laki moja katika Shirika la huduma kwa vijana wa taifa NYS.
Waziri wa utumishi wa umma nchini Geoffrey Ruku amesema hatua hiyo itachangia kuboreshwa kwa huduma za umma sawa na kuhakikisha Shirika la NYS linakuwa nguzo muhimu kwa maendeleo ya taifa.
Akizungumza katika kaunti ya Machakos, Waziri Ruku amesema hatua hiyo itapunguza utegemeaji wa ufadhili wa umma kwani shirika hilo itapanua mikakati bora ya serikali ya kibiashara pamoja na kufanikisha utoaji wa huduma kwa wananchi.
Waziri Ruku amelishinikiza bunge la kitaifa kuharakisha marekebisho ya mswada wa NYS ambao utawalishwa na Wizara yake bungeni ili kusawazisha mfumo wa kisheria wa shirika hilo.
Wakati huo huo amewataka vijana kukumbatia mipango ya serikali ya kujumuisha wananchi wote pamoja katika kufanikisha ajenda ya serikali ya maendeleo endelevu hadi mashinani.
News
Nyakang’o, apendekeza mgao wa shilingi bilioni 1.6

Mdhibiti wa bajeti nchin Margaret Nyakang’o amependekeza kuongezwa kwa kiwango cha bajeti ya ofisi yake kutoka shilingi milioni 7.2 hadi shilingi bilioni 1.6 ili kufanikisha majukumu yake.
Akizunguza mjini Mombasa wakati wa kikao na kamati ya uekezaji wa umma na hazina maalum katika bunge la Seneti, Nyakang’o amesema bajeti hiyo ya ofisi yake iko chini mno katika kufanikisha mikakati endelevu ya majukumu yake ya kikazi.
Hata hivyo amesema iwapo bajeti hiyo itaongezwa ofisi yake itakuwa na wakati mwafaka wa kukagua miradi ya maendeleo katika kaunti zote nchini.