News
Kikao Cha Kujadili Jinsi ya Kusafisha Sumu ya Lead Eneo la Owino Uhuru Kimetibuka

Kikao cha kujadili jinsi kijiji cha Owino Uhuru katika eneo bunge la Jomvu kaunti ya Mombasa kitakavyosafishwa sumu ya Lead kimetibuka.
Hii ni baada ya wakaazi hao ambao ni waathiriwa wa sumu hiyo kutaka kikao hicho kilichojumuisha maafisa wa Mamlaka ya mazingira nchini NEMA na Wanaharakati wa kijamii kusitishwa.
Wakaazi hao wamelalaka kwamba kikao hicho kinatekelezwa kinyume cha sheria huku wakilalamikia kunyanyaswa na Mamlaka ya NEMA katika mchakato wa kupata fidia yao.
Wakiongozwa na Mkurugenzi wa Shirika la Center for Justice, Governance and Environment Action Phyllis Omido wamesema tangu Mahakama iagize wakaazi hao walipwe fidia ya shilingi bilioni 2 hakuna hatua zozote zilizochukuliwa.
Kwa upande wake Mkuu wa kitengo cha sheria katika Mamlaka ya NEMA Erastus Gitonga amesema zoezi la kusafisha mazingira ya Owino Uhuru litafanywa kwa hatua ikiwemo kufanya vipimo vya mchanga, maji na mimea katika eneo hilo ili kutathmini kiwango cha sumu.
News
Kadinali Bacciu Atangaza Kutohudhuria Kikao cha Conclave

Kadinali Giovanni Angela Bacciu ametangaza kujiondoa katika kikao cha siri cha kumchagua Papa mpya kilichopangwa na Ofisi ya Vatican kuanza rasmi mwezi Mei 7.
Katika taarifa yake aliyoitoa kupitia Wakili wak siku ya Jumanne tarehe 29, Kadinali Bacciu amesema ameamua kutii wasia ulioweka wa Hayati Papa Francis ingawa alidumisha kutokuwa na hatia.
“Kwa kuwa moyoni mwangu nina wema wa Kanisa ambalo nimelitumikia na nitaendelea kulitumikia kwa uamunifu na upendo na kuchangia ushirika na utulivu wa Conclave, nimeamua kutii kama nilivyofanya siku zote wakati wa Papa Francis na nitasalia kuamini kwamba sina hatia”, alisema Kadinali Bacciu.
Kadinali Bacciu mwenye umri wa miaka 78 na mzaliwa wa taifa la Italia amegongwa vichwa vya habari kutokana na msimamo wake huku baadhi ya wachanguzi wakisema uamuzi wake umetokana na sintofahamu zilizokuwepo kati yake na Hayati Papa Francis mwaka wa 2020 baada ya kuagizwa na Papa Francis kujiuzulu kwa kupatikana na kashfa ya ufisadi.
News
Mbogo: Kaunti ya Mombasa Imeshindwa Kutatua Mzozo wa Ardhi

Aliyekuwa mbunge wa Kisauni Ali Mbogo ameikosoa serikali ya kaunti ya Mombasa kwa kushindwa kutatua suala tata la uskwota linalowakumba wakaazi wengi wa kaunti hiyo.
Akizungumza katika eneo la Kisauni katika kaunti ya Mombasa, Mbogo amesema tatizo la uskwota limeendelea kuwa chanzo kikuu cha migogoro ya ardhi na ukosefu wa usalama katika maeneo mengi ya kaunti ya Mombasa huku serikali ya kaunti hiyo ikionekana kulifumbia macho suala hilo.
Mbogo amedai kwamba maelfu ya wakaazi wa Kisauni na Mombasa kwa jumla wanaishi kwa hofu ya kufurushwa katika ardhi zao walizoishi tangu jadi kufuatia ukosefu wa hati miliki.
Wakati huo huo amedokeza kwamba baadhi ya maafisa wa serikali ya kaunti hiyo wanahusishwa na visa vya uporaji wa ardhi za umma kwa kushirikiana na waekezaji jambo ambalo amelitaja kuwa dhulma.