National News
Wakaazi wa Jomvu Mombasa, Wanalalamikia Kucheleweshwa Kwa Fidia Yao

Wakaazi wa mtaa wa Owino Uhuru katika eneo bunge la Jomvu kaunti ya Mombasa, walioathirika na sumu ya madini ya kemikali ya Lead wanalalamikia kucheleweshwa kwa fidia yao.
Kulingana na wakaazi hao, mnamo Disemba 6 mwaka jana, Mahakama ya upeo nchini iliamua waathiriwa hao kufidiwa shilingi bilioni 2, lakini miezi 3 baadaye serikali haijaonyesha dalili yoyote ya waathiriwa hao kufidiwa.
“Zaidi ya watu 100 waliaga dunia kutokana na sumu ya madini hayo Lead na wengine wanaugua maradhi mbalimbali kama vile kuavya mimba, maradhi ya figo, ukosefu wa nguvu za kiume na maradhi mengine,” Wakaazi.
Kwa upande wake Mkurugenzi mkuu wa Shirika la kimazingira la Center for Justice, Governance and Environmental Action Phyllis Omido, amesema huenda waathiriwa zaidi wakapoteza maisha iwapo hatua za dharua za matibabu hazitachukuliwa.
“Uwino Uhuru sai zaidi ya wananchi 100 walishaaga maisha na watoto, tumepoteza watoto zaidi ya 300 kwa vifo ambavyo viko vinahusiana na simu ya madini ya Lead na kwa hivyo wale ambao wamebaki wengi bado ni wagonjwa na wanahitaji matibabu na hizo fedha zitaenda kuwasaidia pakubwa,” Omido.
Itakumbwa kwamba tangu kesi hiyo ianze mwaka wa 2019 wakaazi hao bado hawajalipwa fidia yao licha ya Mahakama kuagiza familia hizo zilipwe fidia ya kima cha shilingi bilioni 1.3 na shilingi milioni 700 zaidi za kusafisha mazingira yao.
National News
Chonga: Wakenya Wanaosafiri Ughaibuni Kusaka Ajira Hawazingatii Sheria za Leba

Mwenyekiti wa kamati ya Leba katika bunge la kitaifa Ken Chonga amesema baadhi ya wakenya ambao wanasafiri katika mataifa ya miliki za kiarabu kusaka ajira wamekosa kuzingatia sheria za Wizara ya Leba nchini na kuangukia mikononi mwa walaghai.
Chonga amesema ni lazima wakenya hao wachunguze mawakala wanaowasafirisha katika mataifa hayo kama wanatambulika na serikali, ndipo waingie katika mikataba ya uajiri ambayo imezingatia sheria za Leba nchini.
Akizungumza na Wanahabari mjini Kilifi, Chonga ambaye pia ni Mbunge wa Kilifi Kusini amesema ili wakenya waepuke madhila mbalimbali kutoka kwa waajiri wao katika mataifa hayo ni lazima wasafirishwe na mawakala waliosajiliwa na serikali.
Wakati huo huo amesema japo serikali iko mbioni kuhakikisha inawatafutia wakenya kazi katika mataifa ya ughaibuni ni lazima wanaosaka ajira za ughaibuni waingie katika mkataba wa uajiri kabla ya kusafiri nje ya nchi.
National News
Chibule: Visa vya Dhulma za Kijinsi Vimepungua Kilifi

Serikali ya kaunti ya Kilifi imesema visa vya dhulma za kijinsia katika kaunti hiyo vimepungua kwa kiwango kikubwa.
Kulingana na Naibu Gavana wa kaunti hiyo Flora Mbetsa Chibule, visa hivyo viliongezeka zaidi msimu wa maambukizi ya virusi vya Corona, ambapo kaunti ya Kilifi iliorodheswa nafasi ya tatu nchini baada ya kaunti ya Bungoma na Samburu.
Chibule amesema kwa sasa ni asilimia 12.3 pekee ya visa hivyo vilivyoripotiwa tofauti na asilimia 30 wakati wa maambukizi ya Corona, akisisitiza kwamba juhudi hizo zimefanikiwa kupitia ushirikiano wa jamii na wadau mbalimbali.
Kiongozi huyo amedokeza kwamba serikali ya kaunti imetoa mafunzo kwa maafisa wa kutoa ushauri nasaha ili kusaidia kupambana na visa hivyo mashinani, akisema juhudi hizo zitaendelezwa sawa na kudhibiti madhila hayo.
Wakati uo huo ameweka wazi kwamba kaunti hiyo imekamilisha ujenzi wa sehemu salama ya kuwahifadhi watoto wanaopitia dhulma za kijinsia wakati kesi zao zikiendelea Mahakamani.