Entertainment
Usafiri wa Pikipiki: Msichana Anafaa Kukaa Vipi?

Katika maisha ya kila siku, usafiri wa bodaboda umekuwa sehemu muhimu kwa watu wa tabaka mbalimbali mijini na vijijini. Kwa urahisi wake, bei nafuu, na uwezo wa kupenya kwenye foleni, bodaboda imewavutia hasa vijana. Lakini mjadala mpya unaibuka—je, namna msichana anavyoketi kwenye bodaboda inaweza kuashiria nidhamu au ukosefu wake?
Ni swali linalozua hisia tofauti, huku wengine wakiliona kama mjadala wa kijamii unaofaa, na wengine wakihisi ni aina ya kuhukumu bila msingi.
Katika jamii zetu, watu huwa na desturi ya kutafsiri matendo ya mtu kwa mtazamo wa tabia na maadili. Msichana anapoketi kwenye bodaboda kwa mkao unaoonekana kama “kutotunza staha”—kama vile kuachana miguu kupita kiasi au kuvaa mavazi yasiyofaa—huweza kuchukuliwa kama hana nidhamu au heshima kwa nafsi yake. Lakini je, huu ni mtazamo wa haki?
Katika kipindi cha Janjaruka 254, mtangazaji Kassim Mbui aliibua hoja hii kwa kusema kuwa baadhi ya mikao ya wasichana kwenye bodaboda huonyesha ukosefu wa maadili. Hata hivyo, mtangazaji mwenzake Binti Umazi alipinga vikali, akisema kuwa kutanua miguu ni suala la usalama, si maadili. Kwa Umazi, lengo ni kuhakikisha msichana hajateleza, hajavuliwa heshima yake, na amejiweka salama kimwili.
Wewe Unazingatia Nini Unapopanda Bodaboda?
Swali linabaki: Wewe binafsi, unapopanda bodaboda, huzingatia nini zaidi—usalama, maadili, mtazamo wa jamii, au hujali kabisa?
Ni vyema kuelewa kuwa nidhamu haimaanishi maisha ya ukale au ya masharti ya kimapokeo. Badala yake, ni kielelezo cha heshima kwa nafsi yako, kwa jamii, na kwa mazingira yanayokuzunguka. Msichana anayeketi kwa nidhamu, akiwa amevalia kwa staha, huonekana kuwa na fahamu ya mazingira na huchukuliwa kwa heshima katika jamii.
Usalama Kwanza: Si Chaguo, Ni Kipaumbele
Mbali na maadili, usalama ni suala nyeti. Kuketi vibaya kwenye pikipiki kunaweza kusababisha ajali mbaya. Mkao sahihi unasaidia kuimarisha usawa wa mwili na kuzuia abiria kuteleza au kuanguka. Hivyo basi, mkao wa kutanua miguu unaweza kuwa njia salama zaidi kwa baadhi ya wasichana—hasa waliovaa mavazi ambayo hayajaziba vizuri. Ila Elvis mimi najiaminisha kuwa unapojua utasafiria bodaboda unastahili kujipanga kimavazi.
Kujiheshimu ni Sauti ya Kimya Inayosema Mengi
Kujiheshimu ni hatua ya kwanza ya kupata heshima kutoka kwa wengine. Si lazima kusema neno lolote—mavazi yako, mkao wako, na maamuzi yako vinaweza kuzungumza kwa niaba yako. Hata katika jambo rahisi kama kuketi kwenye bodaboda, ujumbe unatumwa: “Najijali, najiheshimu, na najitambua.”
Wakati mwingine tunadhani mambo kama namna ya kuketi kwenye pikipiki si muhimu, lakini ukweli ni kwamba, taswira hiyo huweza kubeba ujumbe mkubwa kwa jamii. Msichana yeyote anapopanda bodaboda—na avae kwa staha, aketi kwa nidhamu, na awe makini kwa usalama wake.
Huu si tu ujumbe wa heshima kwa jamii, bali pia ni njia ya kujitambua, na kujilinda binafsi.
Maoni Yako Je?
Je, unakubaliana na mtazamo wa Kassim Mbui au Binti Umazi? Wewe binafsi huzingatia nini unapopanda bodaboda? Niandikie kwenye sehemu ya maoni hapa chini.
Entertainment
Creative Economy Forum 2025: Ruby Kache Uso kwa Uso na Bien
Ruby Kache na Bien wakutana Nairobi kwenye Jukwaa la Uchumi wa Ubunifu! 🌟

Jiji la Nairobi liling’aa zaidi wiki hii baada ya kuandaa Jukwaa la Uchumi wa Ubunifu — tukio la kipekee lililowakutanisha wabunifu, wanamuziki, na wadau wa sanaa kutoka Kenya na Marekani. Mbali na mijadala ya sera na mipango ya maendeleo, tukio hili lilikutanisha watu mashuhuri.
Mrembo wa redio, Ruby Kache, alikutana na nyota wa muziki, Bien aliyekuwa kwenye kundi la maarufu Sauti Sol!
Kwa wanaosikiliza redio, jina la Ruby Kache si geni. Ni mtangazaji machachari wa kipindi cha “The Wave” kupitia Coco FM, kinachoenda hewani kila Jumamosi kuanzia saa 4 asubuhi hadi saa 7 mchana. Kipindi chake kinajulikana kwa kuangazia maisha ya vijana, muziki wa kisasa, mitindo na mazungumzo yenye msisimko.
Katika kongamano hili, Ruby alihudhuria kama mshiriki, lakini kama ilivyo kawaida yake — aliiba spotlight bila kusema neno jukwaani. Uvaaji wake, tabasamu lake na muingiliano wake na wadau wengine ulitosha kuonyesha uwepo wake wa nguvu.
Moja ya highlights kubwa za siku hii ilikuwa ni wakati Ruby Kache alipokutana na Bien. Ruby alirekodi kipande kifupi na kukipakia kwenye ukurasa wake wa Facebook, huku mashabiki wakishangilia. Bien, nguli wa mziki anayeshikilia tuzo ya muimbaji bora Afrika Mashariki, alikuwa mgeni maarufu katika tukio hilo.
Baadhi ya waunda maudhui maarufu kutoka Pwani waliopamba hafla hiyo ni pamoja na Presenter Kai, Beka Ruga, Mwagwaya Ndani, na Princess Fynick, waliokuja kwa mitoko ya kisasa. Kwa upande wa muziki, Reagan Dandy alikuwa miongoni mwa wanamuziki wachache kutoka Pwani waliobahatika kuhudhuria tukio hilo la hadhi ya kimataifa.
Jukwaa la Uchumi wa Ubunifu limeibuka kama jukwaa muhimu kwa kuvunja mipaka kati ya sanaa, biashara na teknolojia. Kupitia mikutano kama hii, wasanii, waunda maudhui na wadau wa sekta ya ubunifu wanapata nafasi ya kuunganishwa na fursa za kimataifa, kujifunza kuhusu ulinzi wa kazi zao, na kuelewa jinsi ya kujitegemea kiuchumi kupitia vipaji vyao. Kwa kizazi kinachotegemea mitandao na ubunifu kama njia ya kujieleza, majukwaa haya yanakuwa daraja kati ya ndoto na mafanikio halisi.
Kwa washiriki kutoka Pwani na sehemu nyingine za Kenya, kongamano hili halikuwa tu mahali pa kuonekana, bali pa kujifunza, kuunganishwa na kuchochewa kufikiria ubunifu kama ajira na biashara. Uwepo wa majina maarufu kama Ruby Kache, Bien, na waunda maudhui wengine wakubwa ulitoa motisha kwa vijana, huku ikithibitisha kuwa sanaa inaweza kuwa nguvu ya kiuchumi na chombo cha mabadiliko chanya katika jamii.
Entertainment
#UlijanjarukaVipi! Safari ya Mpishi Nguli, Don Moses: Kutoka Kukosa Karo Hadi Kuwa Head Chef

Katika dunia ya leo ambapo changamoto za kiuchumi zimewaacha vijana wengi wakihangaika, simulizi ya Don Moses ni mwanga wa matumaini kwa wengi.
Akiwa mgeni katika kipindi cha Janjaruka 254, kinachorushwa kila siku ya wiki kuanzia Jumatatu hadi Ijumaa, Moses alisimulia safari yake ya ajabu kutoka kwa kijana aliyezuiwa na karo ya shule hadi kuwa mpishi mashuhuri hadi kuwa Head Chef aliyesimamia wapishi waliosomea fani hiyo chuoni.
Baada ya kuhitimu kidato cha nne, Moses alikuwa ameweka ndoto ya kujiunga na chuo lakini maisha yalikuwa na mpango tofauti. Mama yake alipata ajali mbaya, hali iliyolazimu familia kuhamishia raslimali kwenye matibabu badala ya karo yake ya chuo.
“Nilijua wazi kuwa singeweza kulazimisha familia ichague kati ya maisha ya mama na elimu yangu. Ilibidi nitafute njia mbadala,” anasema Moses.
Jiko la YouTube: Darasa la Ukombozi
Akiwa hana karo, lakini akiwa na shauku, Moses alianza kujifunza sanaa ya upishi kupitia video za YouTube. Binamu yake, Moses Gambo, ndiye aliyemfungulia mlango wa maarifa kwa kumtambulisha kwenye tutorials mbalimbali mtandaoni.
Ni ujuzi huo wa mtandaoni uliomfungulia milango ya ajira katika hoteli za kifahari, ambapo aliweza kupanda ngazi hadi kuwa mpishi mkuu (Head Chef) — akiongoza wapishi waliopitia vyuo vya kitaaluma. Ni mafanikio ambayo wengi hawakuyatarajia kutoka kwa kijana ambaye hakuingia darasa la kawaida, bali alikaa mbele ya skrini.
“Najua kwenye upishi kuna kupika mashendea ama kupika chakula kibaya ila sijawahi kufeli. Siku zote mimi ni makini na ratio ya viungo. Ndiyo silaha yangu,” anasema kwa kujiamini.
Mwaka wa Mageuzi: 2020
Kama ilivyokuwa kwa wengi, mwaka wa janga la COVID-19 – 2020 – ndiyo ulikuwa mwaka wa mabadiliko makubwa kwa Moses. Akiwa na muda mwingi na motisha mpya, alianza kupika kibiashara, akihudumia watu waliokuwa majumbani.
“Kabula ya hapo, nilikuwa napika kwa kujifurahisha tu. Lakini corona ilinifungua macho. Nikaanza kuona kuwa mapishi ni biashara yenye nguvu,” anasema Moses.
Karo Iliyogeuka Mtaji
Kipindi fulani baadaye, Moses alipata nafasi ya kujiunga na chuo hatimaye. Lakini kwa mshangao wa wengi, alikataa ofa hiyo kwa hiari na kuomba fedha hizo zitumike kupanua biashara yake ya upishi.
“Nitamudu gharama ya chuo siku moja. Kwa sasa, najenga misingi. Muda wa kusoma utafika,” anasema.
💡 Ushauri kwa Vijana: Anza na Kile Kilicho Mkono Wako
Don Moses sasa ni sauti ya matumaini kwa vijana wengi wanaohisi kuwa elimu ya juu au mtaji mkubwa ndio tiketi pekee ya mafanikio. Anasisitiza umuhimu wa kuanza na huduma, si lazima mtaji.
“Kama huna kazi wala mtaji, toa huduma kwanza. Ukiwa na bidii na ubunifu, malipo yatafuata,” anashauri.
Leo hii, sehemu kubwa ya mapato ya Moses huingia moja kwa moja kwenye ununuzi wa vifaa bora vya upishi, huku akiendeleza ndoto yake ya kuwa mmoja wa wapishi wakubwa zaidi nchini Kenya.