Business
Serikali Yalazimika Kufutilia Mbali Deni la Shilingi Bilioni 6 Kutoka Hazina ya Hustler

Serikali sasa inasema italazimika kufuta deni la takriban shilingi bilioni 6 kutoka kwa Hazina ya Hustler, baada ya waliopewa mikopo kushindwa kulipa.
Katibu wa Idara ya Biashara Ndogo na za Kati, Bi Susan Mang’eni, amesema juhudi za kuwasaka waliokopa kisha kutotoroka na fedha hizo hazijazaa matunda, licha ya kuwa ni zaidi ya miaka miwili tangu kuanzishwa kwa hazina hiyo.
Kwa mujibu wa Mang’eni, ni Wakenya milioni 10 waliochukua mikopo lakini hawajarejesha, huku milioni 9 kati ya watu milioni 25 waliopokea fedha hizo wakilipa mikopo yao kama inavyotakiwa.
Ameeleza kuwa hali hiyo imeathiri kwa kiasi kikubwa uendelevu wa hazina hiyo, ambayo ililenga kuwainua wananchi kiuchumi kupitia uwezeshaji wa biashara ndogondogo.
Kutokana na hali hiyo, serikali sasa inawasihi wabunge kupitisha ombi la kutengewa shilingi bilioni 5 zaidi katika bajeti ya mwaka huu, ili kuendeleza shughuli za hazina hiyo.
Business
Vijana Kaunti ya Tana River Waanzisha Biashara ya Sambusa za Samaki kuinua Uchumi

Vijana katika Kaunti ya Tana River wameanzisha biashara ya upishi wa sambusa za samaki kwa lengo la kujikwamua kiuchumi kwa kutumia rasilimali za baharini.
Wamebuni mbinu ya kipekee ya kuandaa sambusa kwa kutumia samaki wa aina mbalimbali, wakiwemo samaki papa. Mbali na sambusa, vijana hao pia wameweza kuunda bidhaa nyingine za thamani kutokana na samaki, hatua inayochochea ubunifu na kuongeza ajira miongoni mwao.
Kulingana na vijana hao, biashara hiyo inalenga kuongeza kipato chao na kufungua milango ya kuingia katika masoko mapya, ya ndani na hata ya nje ya kaunti.
Hatua hii imesukumwa na changamoto ya uhaba wa soko la samaki katika eneo hilo, hali ambayo husababisha uharibifu wa samaki kutokana na kukosa wanunuzi. Kwa hivyo, ubunifu huu umekuwa suluhisho la kiuchumi na kiteknolojia kwa vijana wa Tana River.
Business
Wafanyabiashara wa Soko la Matano Mane Waililia Serikali ya Kaunti ya Kilifi Kuwajengea Choo

Wafanyabiashara katika soko la Matano Mane, eneo la Vitengeni, Kaunti ya Kilifi, wameitaka serikali ya kaunti hiyo kuwajengea choo, wakisema ukosefu wa huduma hiyo muhimu umekuwa kero kubwa inayozorotesha shughuli za biashara.
Wakiongozwa na Phelisia Mageshi, wafanyabiashara hao wamesema kuwa hali ya sasa imesababisha baadhi yao kuhamishia biashara zao nje ya soko hilo, kutokana na mazingira yasiyofaa kwa shughuli za kila siku.
Bi Mageshi ameeleza kuwa licha ya serikali ya kaunti kufahamishwa kuhusu changamoto hiyo mara kadhaa, hakuna hatua yoyote iliyochukuliwa hadi sasa, hali inayowafanya kuhisi kusahaulika.
Wameitaka serikali ya kaunti kuingilia kati kwa haraka ili kuboresha mazingira ya kufanyia biashara na kuhakikisha afya ya wananchi inalindwa.