News
Maagizo ya waziri Murkomen yaendelea kuzua mihemko.

Wabunge wanaoegemea chama chake aliyekuwa naibu rais Rigathi Gachagua DCP wametangaza mipango ya kuwasilishwa hoja bungeni ya kutaka kutimuliwa madarakani kwa waziri wa usalama wa kitaifa Kipchumba Murkomen.
Wabunge hao walidai matamshi aliyotoa waziri Murkomen ya kuagiza maafisa wa polisi kupiga risasi na kuua-Shoot to Kill hasa wakati wa maandamano yanatosha kumuondoa ofisini.
Akitangaza mipango hiyo mbunge wa Manyatta Gitonga Mukunji, alimkosoa Murkomen akidai anachochea ongezeko la visa vya mauaji ya kiholela nchini vile vile watu kutoweka katika njia tatanishi.
Mbunge huyo alidai visa hivyo vimekuwa vikishuhudiwa chini ya uongozi wa serikali ya Kenya Kwanza.
Alishinikiza bunge la kitaifa kutekeleza jukumu lake la uangalizi na kulinda maisha na uhuru wa wakenya.
Murkomen amekuwa akikosolewa kutokana na matamshi yake ya wiki jana baada ya kushuhudiwa uharibifu wa miundombinu ya maafisa wa polisi vile vile baadhi ya maafisa wa usalama kujeruhiwa na waandamanaji, ambapo baadaye alionekana akijitetea.
Taarifa ya Joseph Jira
News
Anselim, ashutumu utovu wa usalama Taita Taveta

Kaimu Spika katika bunge la kaunti ya Taita Taveta Anselim Mwadime alieleza kusikitishwa na mauaji ya mhudumu mmoja wa bodaboda aliyeuliwa na kisha pikipiki yake kuchukuliwa katika eneo la chuo kikuu cha Taita Taveta.
Mwadime alisema kuna baadhi ya abiria ambao ni wahuni hubebwa na kisha kuwashambulia wahudumu wa pikipiki hadi kuwaua au hata kutoweka na pikipiki.
Aidha, Mwadime alisema kama viongozi wa kaunti ya Taita Taveta hawataruhusu visa hivyo kuendelezwa katika kaunti hiyo.
Vilevile, Mwadime aliishinikiza idara ya usalama kwenye kaunti ya Taita Taveta kuwajibika ipasavyo ili kudhibiti visa vya utovu wa usalama katika sekta ya bodaboda na wanaohusika wakabiliwe kisheria.
“Hili jambo linafaa kufuatiliwa kwa undani. Na tunalilaani vikali sisi kama viongozi wa Taita Taveta’’ alisema Mwadime.
Taarifa ya Janet Mumbi
News
Viongozi wahimizwa kushirikiana kubuni ajira kwa vijana

Mwakilishi wa wadi ya Sabaki eneo bunge la Magarini kaunti ya Kilifi Rose Baraka alitoa wito kwa viongozi wa kaunti ya Kilifi kushirikiana na mashirika ya kijamii pamoja na wawekezaji katika kaunti ya Kilifi ili kudhibiti changamoto za ukosefu wa ajira miongoni mwa vijana.
Rose alisema hatua hiyo itasaidia pakubwa kuwaepusha vijana kujiingiza kwenye utumizi wa mihadarati sawa na uhalifu.
Akizungumza wakati wa kikao kilichowaleta pamoja maafisa wa shirika la SHOFCO pamoja na wakaazi wa Sabaki, Rose aliahidi kushirikiana na mashirika mbalimbali ya kijamii katika juhudi za kuwasadia wananchi kujiendeleza kupitia mpango wa ajira.
“Vijana ni wengi, kazi ni kidogo. Sisi kama viongozi tunastahili kutia bidii kutafuta haya mashirika ili tuangalie vijana wetu wasaidika vipi’’ alisema Rose Baraka.
Kwa upande wake Afisa wa Shirika la SHOFCO eneo la Magarini Kelvin Mtawali Karisa aliupongeza ushirikiano wa mwakilishi wa wadi huyo na shirika hilo na kuwataka vijana kujiunga kwenye makundi mbalimbali ili waweze kupata mikopo ya kujiendeleza kimaisha.
Taarifa ya Janet Mumbi