County
Kenya Yashuhudia Ongezeko la Watalii

Kenya ilirekodi jumla ya watalii milioni 7.6 mwaka wa 2024, hii ikiwa ni ongezeko la asilimia 11 ikilinganishwa na mwaka 2023.
Waziri wa Utalii nchini Rebecca Miano amesema watalii milioni 2.4 kati yao walikuwa wa kimataifa huku watalii milioni 5.2 wakiwa wa ndani kwa ndani na kwamba Kenya ilikusanya takriban shilingi bilioni 452.2 kupitia sekta ya utalii ikiwa ni ongezeko la asilimia 15.
Waziri Miano amesema hatua hiyo imechangiwa na kuboreshwa kwa mbinu za mauzo ya kitalii, kuimarishwa kwa vivutio na kuzinduliwa kwa mashirika zaidi ya ndege za kimataifa zinazotua humu nchini.
Akizungumza jijini Mombasa wakati wa uzinduzi wa ripoti ya Utalii ya mwaka wa 2024, Waziri Miano amesema wanalenga kufikisha watalii milioni 3 wa kimataifa na ongezeko la mapato hadi shilingi bilioni 560 mwaka huu.
County
Kilifi Imeweka Mikakati Bora ya Kuhakikisha Hospitali na Zahanati Zinakuwa na Madawa ya Kutosha

Naibu Gavana wa kaunti ya Kilifi Flora Mbetsa Chibule amesema serikali ya kaunti ya Kilifi imeweka mikakati bora ya kuhakikisha hospitali na zahanati zote za umma katika kaunti hiyo zinakuwa na madawa ya kutosha.
Chibule amesema tayari serikali ya kaunti hiyo imepitisha bajeti ya fedha za ziadi ili kuhakikisha huduma bora za afya zinawafikia wananchi mashinani, akiwarai wakaazi na wahudumu wa afya kuhakikisha wanalinda madawa hayo.
Akizungumza wakati wa zoezi la uzinduzi wa ujenzi wa jengo la Huduma Centre katika eneo bunge la Ganze, Chibule amesema sekta ya afya hadi mashinani itaboreshwa zaidi.
“Kuna mpango ambao tunaufanya ambao ni kuchukua madawa yetu kutoka KEMSA, japo ule mpango tulikuwa tunataka iko chini ya asilimia 20 lakini madawa yalifika. Nawahimiza wahudumu wa afya na wananchi kulinda raslimali zetu’, alisema Chibule.
Wakati uo huo amepongeza uzinduzi wa ujenzi wa jengo la huduma Centre katika eneo bunge la Ganze, akisema kwamba huduma zote za umma sasa itakuwa zinapatikana kwa urahisi hadi mashinani pindi ujenzi huo utakapokamilika.
County
Mung’aro Awaonya Madaktari na wahudumu wa Afya Wenye Hulka ya Kuiba Dawa Hospitalini

Gavana wa kaunti ya Kilifi Gedion Mung’aro amewaonya madaktari na wahudumu wengine wa afya katika kaunti hiyo wenye hulka ya kuiba madawa hospitalini, akisema kwamba watakaopatikana watakabiliwa kisheria.
Akizungumza baada ya kuzindua kitengo cha Radiolojia katika jengo la Kilifi County Medical Complex, Gavana Mung’aro amesema tangu aingie uongozini Serikali yake imefanikiwa kuwakamata wale ambao wamekuwa wakihusika na wizi wa madawa hospitalini.
Kiongozi huyo amesema serikali ya kaunti hiyo kwa ushirikiano na wadau wengine wanaendeleza mikakati ya kuhakikisha hospitali na zahanati za umma katika kaunti hiyo zinakuwa na vifaa vya kisasa vya matibabu.
“Nilipoingia kama Gavana nilianza kusafisha hii kaunti kwa sababu tulipokuwa walikuwa wengi sana lakini inakaa bado wako kwamba watu wanalipa pesa na watu wanapeleka pesa kwa akaunti zao ama wanatengezewa liseni bandia apewe na watu wachukue pesa waeke mfumo, nataka kuwahakikisha kwamba siku chache zijazo nitangaza watu wengi sana ambao wataenda nyumbani,” Gavana Mung’aro.
Kwa upande wake Naibu Gavana wa kaunti hiyo Flora Chibule amesema ushirikiano zaidi utaendelezwa, kati ya serikali ya kaunti na wadau wengine ili kuhakikisha miradi ya maendeleo inatekelezwa ipasavyo.
Ameahidi kumuunga mkono Gavana Mung’aro kufanikisha juhudi bora za utoaji wa huduma kwa wakaazi wa kaunti ya Kilifi, akisema hiyo ndio hatua pekee ya kuhakikisha wananchi wananufaika na miradi ya maendeleo.
“Sisi tuko nyuma yake kumuunga mkono na kwa yeyote yule ambaye ataingia kwa siasa hayo ni ya 2032 lakini tugange haya ya leo ya kwamba siku hii ya leo tunafurahikia tuna mashine ya kufanya ukaguzi wa kiafya,” Chibule.