News
Godhana, awataka wakaazi kutoingiza siasa miradi ya maendeleo

Gavana wa kaunti ya Tana River Dhadho Godhana amewataka wenyeji wa kaunti hiyo kujiepusha na wanasiasa ambao wanaingiza siasa kwenye masuala ya maendeleo.
Godhana alisema hilo limechangia kaunti ya Tana River kusalia nyuma kimaendeleo hali ambayo itasababisha miradi mingi kuzidi kukwama.
Godhana alisema ni lazima viongozi na wenyeji wa kaunti ya Tana River washirikiane na uongozi wa kaunti ili kuafikia utekelezaji wa miradi ya maendeleo.
Wakati huo huo Godhana aliesema mradi wa Village Cluster ambao umekuwa ukipingwa ndio utakaosaidia kudhibiti changamoto ambazo zinaikumba kaunti ya Tana River.
Naye Mahat Ali Loka ambaye ni Naibu Gavana wa kaunti ya Tana River, aliwaonya wanasiasa kutoka kaunti zingine dhidi ya kuingilia siasa za kaunti hiyo huku Spika wa bunge la kaunti hiyo Osman Noor Galole, akitoa onyo kwa wafanyikazi wa umma dhidi ya kujumu la serikali ya kaunti ya Tana River.
Taarifa ya Janet Mumbi
News
Mwili wapatikana baharini Shelly Beach Likoni

Polisi kaunti ya Mombasa wanachunguza kisa ambapo mwili wa mwanamme ambaye hajafahamika umepatikana ukielea katika maji ya bahari hindi kwenye ufuo wa Shelly Beach eneo bunge la Likoni.
Ripoti ya polisi ilibaini kuwa mwili huo uligunduliwa na wavuvi eneo hilo, ambao walipiga ripoti katika kituo cha polisi cha Shelly Beach kuhusiana na tukio hilo.
Polisi walisema hawakubaini mara moja anakotoka mtu huyo.
Vile vile haikubainika iwapo marehemu alizama au aliuawa kabla ya mwili wake kutupwa baharini.
Polisi walisema hawajakutana na stakabadhi zozote za kumtambulisha mtu huyo huku wakiwasihi wananchi kutoa taarifa iwapo wanafahamu familia ya marehemu.
Mwili unahifadhiwa katika hifadhi ya maiti katika hospitali ya Rufaa ya Coast General Mombasa wakati uchunguzi zaidi ukiendelea.
Taarifa ya Joseph Jira
News
Mung’aro: Ushirikiano wa viongozi utaimarisha muundomsingi

Ushirikiano baina ya viongozi wa kaunti ya Kilifi na serikali kuu kupitia Wizara ya madini na raslimali za baharini umepelekea kuimarika kwa miundo msingi eneo la Jaribuni, Ganze kaunti ya Kilifi.
Haya ni kwa mujibu wa viongozi wa Kilifi wakiongozwa na Gavana Gideon Maitha Mung’aro.
Wakizungumza katika mkutano uliowaleta pamoja wawekezaji wa timbo na wakaazi katika uwanja wa Mbudzi Dispensary, viongozi hao walisisitiza haja ya wawekezaji hao kuwajibika vilivyo.
“Hakuna kazi yoyote ya timbo itakayoendelea hadi barabara imalizwe” alisema Gavana wa Kilifi Gideon Mung’aro.
Ni kauli iliyoungwa mkono na Mwakilishi wa Kike kaunti ya Kilifi, Getrude Mbeyu alisema kuwa wawekezaji ambao bado hawajakamilisha majukumu yao ya ujenzi wa barabara wanachangia kuzuia wenzao wasiendeleze shughuli zao uchimbaji madini.
Serikali ya kaunti ya Kilifi kwa ushirikiano na serikali kuu ilitoa amri kwa wawekezaji hao kujenga barabara hiyo kutoka Jaribuni hadi Dzitsoni ili kuwaepusha wakaazi dhidi ya vumbi.
Hata hivyo wawekazaji hao waliagizwa kujenga barabara hiyo kwa ushirikiano ambapo kufikia sasa ni mwekezaji mmoja pekee ambaye amekamilisha ujenzi huo eneo la Marere huku wengine wakisalia kujikokota.
Taarifa ya Hamis Kombe