News
Gataya: Kaunti ya Kilifi Imeonyesha Kuwajibika Kisheria

Kamati ya utekelezaji wa sheria katika bunge la Seneti imefanya kikao na Gavana wa kaunti ya Kilifi Gedion Mung’aro kutathmini jinsi serikali ya kaunti hiyo inavyoendana na sheria za kitaifa.
Mwenyekiti wa kamati hiyo Mwenda Gataya amesema kati ya kaunti ambazo kamati hiyo imezitembelea, serikali ya kaunti ya Kilifi imeonyesha kuwajibika katika kuzingatia sheria.
Akizungumza na Wanahabari baada ya kikao hicho katika makao makuu ya Gavana wa Kilifi, Gataya ambaye pia ni Seneta wa kaunti ya Tharaka Nithi, amesema hatua hiyo imesaidia kuzuia mivutano ya kisheria.
“Tumefurahishwa na kaunti ya Kilifi jinsi ilivyofuata sheria na katiba na kama kamati ya seneti tumeridhia hatua hiyo kwamba kaunti ya Kilifi ni kati ya kaunti bora zaidi kwa kufata sheria na ndio matarajio yetu. Tumeangalia matumizi ya hazina ya wadi pamoja na zengine na kweli ni wazi kwamba imezingatia sheria kwa kuhusisha umma”, Gataya.
Kwa upande wake Gavana wa Kilifi Gedion Mung’aro amesema wanalenga kubuni sheria itakayowawezesha wasimamizi wa vijiji kutambulika kisheria, sawa na kubuni sheria itakayojumuisha wananchi katika ujenzi wa shule za Chekechea ili kudhibiti matumizi mabaya ya fedha pamoja na kubuni sheria itakayosimamia bodi ya ukusanyaji ushuru wa kaunti.
Wakati huo huo Gavana Mung’aro amedokeza kwamba tangu achukue hatamu ya uongozi, kaunti ya Kilifi imefaulu kurejesha zaidi ya shilingi bilioni 1.9 kutoka kwa kesi mbalimbali zilizowasilishwa Mahakamani, akisema ni lazima sheria izingatiwe.
“Kuna kesi moja hii kaunti ilikuwa inadaiwa milioni 926 na nikapambana hadi milioni 114, moja ilikuwa bilioni 1.1 na kuenda Mahakamani na tukashinda hiyo kesi na labda wakate rufaa na tupate taarifa kutoka Mahakamani lakini kesi hiyo tulishinda kwa hivyo kaunti imepata bilioni 1.1 pamoja na milioni 800 hiyo ni bilioni 1.9”, Mung’aro.
News
IPOA: Watu 20 walifariki katika vituo vya polisi mwaka huu

Mamlaka ya kuchunguza utendakazi wa maafisa wa polisi nchini IPOA, imetoa tahadhari kwa taifa kutokana na ongezeko la vifo vya wakenya vinavyotokea katika vituo vya maafisa wa Polisi nchini.
Katika ripoti iliyotolewa na IPOA, takriban watu 20 wamefariki wakiwa chini ya ulinzi wa maafisa wa polisi katika kipindi cha miezi minne pekee iliyopita.
Mwenyekiti wa IPOA Issack Hassan, amesema Mamlaka ya IPOA haijawakamata washukiwa wa visa hivyo kutokana na mamlaka hiyo kutokuwa na uwezo, akisema washukiwa wote wanaohusishwa na kesi hizo wanachukuliwa kama wahalifu.
“Tumenakili visa visivyopungua 20 katika kipindi cha miezi minne pekee kwamba watu hawa walipoteza maisha yao ndani ya seli zetu na kunaendelea na uchunguzi, kesi hizo zitafikishwa kwa Ofisi ya ODDP na wahusika watafunguliwa mashtaka”, alisema Hassan.
Hassan amesema kufikia sasa maafisa wa polisi 17 wamehojiwa kuhusiana na matukio hayo ikiwemo wale waliomkamata Albert Ojwang pamoja na mashahidi 6, akisema haki kwa familia za wale waliopoteza wapendwa wao itapatikana.
Mwenyekiti huyo wa IPOA, ameyasema hayo alipofika mbele ya kamati ya bunge la kitaifa kuhusu usalama, akisema Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi nchini Eliud Lagat pia atafika mbele ya Mamlaka ya IPOA kuandikisha taarifa kuhusu kifo cha Ojwang.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
News
Usalama na Elimu zavuna kwenye bajeti ya kitaifa

Waziri wa Fedha nchini John Mbadi alisoma bajeti ya kitaifa ya mwaka wa Fedha wa 2025/2026 ambayo ni makadirio ya takriban shilingi trilioni 4.23.
Akisoma bajeti hiyo katika majengo ya bunge la kitaifa, Waziri Mbadi alisema mgao wa shilingi trilioni 3.13 ni matumizi ya kawaida ya serikali, shilingi bilioni 693.2 kwa matumizi ya maendeleo na mgao wa shilingi bilioni 474.9 ukitengewa serikali za kaunti.
Katika bajeti hiyo, Waziri Mbadi alipendekeza mgao wa shilingi bilioni 202 kwa idara ya ulinzi nchini, shilingi bilioni 125.7 kwa huduma ya usalama wa kitaifa, shilingi bilioni 51.4 zikitengwa idara ya ujasusi nchini, shilingi bilioni 32.5 kwa idara ya polisi nchini na shilingi bilioni 38.1 kwa idara ya magereza.
Waziri Mbadi alipendekeza mgao wa shilingi bilioni 138.1 kwa sekta ya Afya ili kufanikisha miradi mbalimbali ikiwemo ule wa Afya kwa wote UHC, shilingi bilioni 3.8 kwa masuala ya ardhi nchini huku shilingi bilioni 82.8 kwa sekta ya Kilimo nchini.

Waziri Mbadi, na wabunge katika majengo ya bunge la kitaifa.
Hata hivyo sekta ya elimu nchini ilitengewa mgao wa shilingi bilioni 702.7, ambapo shilingi bilioni 387.2 zimetengwa kuajiri walimu wa CBC, shilingi bilioni 5.9 kusimimia mitihani ya kitaifa, shilingi bilioni 7 kusimamia masomo ya shule za msingi, shilingi bilioni 51.9 kusimamia shule za upili na shilingi bilioni 28.9 kwa sekondari msingi.
Kulingana na Waziri Mbadi, Serikali imepunguza ushuru wa mchele kutoka nje, Wajenzi na wanaofanya kazi za ngozi wamepata afueni huku Mbadi akiongeza ushuru wa bidhaa za Anasa kama vileo Wageni wanaofanya biashara za pesa mtandaoni kulipia
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi