Entertainment
Drama Imeisha! Hatimaye, Mulamwah na Ruth Wasameheana

Baada ya siku kadhaa za drama ya hadharani iliyojaa hisia kali, maumivu, na mfululizo wa tuhuma zilizosambaa kwa kasi kwenye mitandao ya kijamii nchini Kenya, hatimaye upepo wa maelewano umeanza kuvuma kati ya mchekeshaji maarufu Mulamwah na mama wa mtoto wake, Ruth K.
Wawili hawa walijikuta katika sakata zito la mtandaoni lililoshuhudia siri zao binafsi kuvuja, maneno makali kutupwa hadharani, na maisha yao ya faragha kueka mezani mbele ya umma. Kwa wengi, kilichokuwa kinatokea kilionekana kama muendelezo wa mapenzi yaliyogeuka sumu. Lakini sasa, kuna dalili za matumaini.
Kupitia taarifa aliyochapisha mitandaoni, Mulamwah alionesha toba ya kweli, akieleza kuwa amepitia tafakari ya kina juu ya matendo yake yaliyowavunjia moyo watu wengi, hasa mashabiki wake na mama wa mtoto wake.
“Nimerudi nyuma na kutathmini hatua zangu. Nilichochewa na mambo mengi, lakini hiyo haisabihi kabisa kile nilichofanya. Narudisha maneno yangu nyuma.”
Akiwa mwenye unyenyekevu, aliendelea:
“Poleni sana mashabiki wangu, nimewaangusha wengi kwa njia nyingi. Pole sana kwa R.K, Mama Oyando. Nimekusamehe, na natumaini utanisamehe pia.”
Huu ulikuwa ni msamaha uliosubiriwa kwa hamu, hasa baada ya madai mazito yaliyotolewa awali na Ruth K kuwa Mulamwah alisambaza video yake ya faragha kwa baba na kaka yake — jambo ambalo ni la kusikitisha na pia ni kosa kubwa kisheria chini ya Sheria ya Makosa ya Mitandao ya Kenya.
Kwa upande wake, Ruth K hakukaa kimya. Baada ya kipindi cha maumivu, alichapisha picha ya wazi ya Mulamwah kwenye hadithi zake za Instagram kama kisasi, kabla ya kuitoa na kuomba msamaha.
Katika ujumbe uliojaa hisia, Ruth alikiri kwamba alichukua hatua hiyo akiwa ameumizwa na kukatishwa tamaa, lakini aliamua kutazama mbele kwa sababu ya mwanawe, na kwa ajili ya uponyaji na ukuaji wake binafsi.
“Nataka kuanza kwa kusema — Samahani sana. Najua machapisho ya leo huenda yalionekana vibaya, na ninachukua jukumu kamili. Nilipaswa kufanya vizuri zaidi. Nitafanya vizuri zaidi.”
Ruth aligusa mioyo ya wengi alipoeleza changamoto anazopitia kama mama mlezi, na jinsi mtoto wake amekuwa nguzo ya maisha yake:
“Kama mama mlezi, kulea mwanangu ni jukumu langu kubwa zaidi na pia baraka yangu kuu. Yeye ndiye sababu ninapigana kwa bidii… na sababu pia ya kuchukua hatua ya kurudi nyuma ili kujielekeza upya kwenye mambo ya msingi — yeye, ukuaji wangu, na chapa yangu.”
Na kwa mtazamo wa kutia moyo, aliongeza:
“Huu si msamaha tu — ni ukurasa mpya.”
Wapenzi wa wapenzi hawa wa zamani walikuwa wameanza kuwa na hofu kuwa sakata lao lingeendelea kuwa chungu zaidi, hasa kwa kuwa lilikuwa linahusisha visasi vya kidijitali. Lakini kwa sasa, wote wawili wameonesha ishara za uwajibikaji na utayari wa kuweka tofauti zao pembeni.
Hii imewapa wengi matumaini kuwa hatimaye Mulamwah na Ruth wataanza ukurasa mpya, sio tu kama wazazi wenza, bali kama watu waliokomaa, waliopona, na wanaotazama mbele kwa hekima na heshima.
Kama Ruth alivyoeleza kwa ujasiri:
“Nimechagua kusonga mbele kwa neema zaidi, ukomavu zaidi, na moyo unaoendana na kusudi langu.”
Na kwa Mulamwah kusema “Pole”, huku akichukua hatua ya kuomba msamaha hadharani, pengine huu ni mwanzo mpya waliouhitaji kwa dhati — wao wawili na mwana wao mpendwa.
Katika dunia ya sasa ya mitandao ya kijamii ambapo kila hisia huwekwa hadharani, ni nadra kuona watu maarufu wakikiri makosa yao kwa uwazi na kuchukua hatua za kweli kurekebisha hali. Mulamwah na Ruth wametufundisha kuwa si aibu kusema samahani, na kuwa kila mtu ana nafasi ya kuanza upya — kwa upole, busara na upendo.
Entertainment
Young Njita: Mr. Malindi ni Brand Yangu ya Biashara – Wanaonilalamikia Wanahofia Mafanikio Yangu

Msanii wa muziki wa rap kutoka Pwani, Ramadhan Ngao Mangale maarufu kama Young Njita – Njigiri, amezungumza kwa mara ya kwanza kwa kina kuhusu mgogoro unaomkabili kuhusu jina lake maarufu – Mr. Malindi.
Akiwa mgeni kwenye kipindi cha COCO ASUBUHI wakati akizindua EP yake mpya ya nyimbo 8 iliyopewa jina “1996” (mwaka wake wa kuzaliwa), Young Njita alisisitiza kuwa jina la Mr. Malindi si tu alilolichagua kwa mapenzi, bali limekuwa sehemu ya maisha yake ya kisanii, ya biashara, na ya jamii.
“Wanaonisema hawana hoja – wana wivu tu na mafanikio yangu. Jina hilo liliibuka baada ya kushinda tuzo ndani ya mji wa Malindi, na watu wenyewe wakaanza kunitambua hivyo. Nikaamua kulitumia kujenga brand yangu,” alisema kwa kujiamini.
Kwa mujibu wa Njita, jina hilo halihusiani tu na muziki. Limekuwa kivutio katika miradi mbalimbali ya kijamii na kibiashara kama vile: Ziara kwenye vituo vya watoto yatima (orphanages), Biashara ya boti, Uzalishaji wa filamu ya Mr. Malindi na Uuzaji wa nguo za chapa ya Mr. Malindi.
“Siwezi kuwa na jina ambalo lina nguvu kiasi hiki kisha niache tu kwa sababu watu wachache wamelalamika. Kila mtu anaweza kujiita Mr. Chonyi, Mr. Kilifi, hata Mr. Coast — hakuna anayemzuia. Jina la mji si milki ya mtu mmoja,” alisisitiza Njita.
Mgogoro huu ulizidi moto baada ya Lufdon Land, kampuni inayojihusisha na matukio ya urembo kama Miss Malindi, kuandika kwenye ukurasa wao wa Facebook tarehe 12 Mei:
“Tumeona jina la Mr. Malindi likitumika na msanii tajika toka Malindi. Jina hilo linamilikiwa kihalali na kampuni ya Lufdon Land… Tumekuwa tukimpa kazi msanii huyo, lakini hatukumchagua kama Mr. Malindi Kenya. Tunaomba kwa heshima asitishe kulitumia.”
Kampuni hiyo ilieleza kuwa hawafanyi shindano la Mr. Malindi kila mwaka, na linapofanywa, hupewa mshindi mmoja pekee. Kwao, jina hilo ni brand ya heshima na sura ya kampuni, hivyo kuliona likitumika kwenye biashara nyingine kuliwafanya wachukue hatua ya kutoa onyo hadharani.
Young Njita kwa upande wake anasema hali ya watu kumtaka aachane na jina hilo si kwa sababu ya sheria, bali kwa sababu ya mafanikio yake.
“Kila mtu anapigania jina baada ya kuona nimefanikiwa nalo. Mbona miaka yote walikaa kimya? Leo hii Mr. Malindi imekuwa gumzo kwa bidii zangu wanaanza kulalamika, kivipi?”
Hili ndilo swali kuu linalozua mjadala mkali mitandaoni. Je, jina kama Mr. Malindi linaweza kuwa milki ya mtu binafsi au kampuni moja? Au linapaswa kuwa huru kwa yeyote mwenye mapenzi, asili au mchango kwa mji huo?
Kwa sasa, bado hakuna tamko la kisheria lililotolewa wazi kuhusu uhalali wa usajili huo, lakini bila shaka, huu ni mgogoro unaoibua maswali mapya kuhusu haki za wasanii, biashara za majina, na nguvu ya brand binafsi zinazojengwa na watu wa kawaida.
Entertainment
Msiiweke Hadharani, Bahati Awambia Mulamwah na Ruth

Katika kile kinachoonekana kama sauti ya busara katikati ya hali ya sintofahamu na maumivu ya hadharani, msanii na mwanamuziki maarufu wa Kenya, Bahati, ameweka ujumbe mzito kwenye kurasa zake za mitandao ya kijamii akiwahimiza Mulamwah na Ruth K kumaliza mgogoro wao kwa njia ya heshima — nje ya macho ya umma.
Kupitia chapisho lake lililojaa hekima na upole, Bahati alieleza kuwa, ingawa huwa hajihusishi sana na maisha ya watu binafsi, alihisi kulazimika kuzungumza kutokana na uchungu wa kuona familia ikivunjika hadharani.
“Siwezi toa maoni kirahisi kuhusu maisha ya watu, lakini sifurahii kuona familia zinavunjika 💔.”
Bahati aliwaomba wakenya na wafuasi wa wanandoa hao wa zamani kuwasaidia kupitia maombi badala ya hukumu, akisisitiza umuhimu wa uponyaji wa moyo na kulindwa kwa mtoto wao asiye na hatia.
“Naomba umma kuwaombea wanandoa hawa vijana. Zaidi ya yote, Mungu AWAREJESHE yale waliyopoteza katika drama hii na APONYE mioyo yao na ALINDE mtoto wao asiye na hatia.”
Kwa uchungu na matumaini, Bahati alitoa ombi lake la moja kwa moja kwa Mulamwah na Ruth, akisema kuwa hajawafikia kwa simu, hivyo anaweka ujumbe wake hadharani kwa nia njema:
“OMBI LANGU PEKEE KWA WAZAZI WENZANGU MULAMWAH NA RUTH (MAANA SIWAPATI KWA SIMU)… TAFADHALI TOENI HII KITU MITANDAONI… NI YA KUUMIZA LAKINI ITAKUWA SAWA KWA JINA LA YESU 🙏”
Akamalizia kwa mafundisho ya kiroho akimnukuu Biblia, akiwakumbusha kwamba hasira haziwezi kuleta haki ya kweli:
Yakobo 1:20 – “HASIRA YA MTU HAIWEZI KULETA HAKI YA MUNGU.”
Ujumbe huu wa Bahati umepokelewa kwa mikono miwili na wafuasi wake pamoja na wale wa Mulamwah na Ruth. Katika kipindi ambacho maisha ya watu maarufu mara nyingi hugeuka kuwa sinema ya hadharani, sauti kama ya Bahati ni ya nadra — akisimama sio kuhukumu, bali kusaidia.
Kwa wengi, alichokifanya ni mfano wa kile ambacho wenzetu katika tasnia au jamii wanapaswa kufanya — kusimama kama ndugu katika imani, katika upendo, na katika nia ya kulinda msingi wa familia, hasa pale penye watoto.
Kwa Mulamwah na Ruth, huu unaweza kuwa mwanzo wa safari mpya — sio ya kutafuta nani alikuwa sahihi au mwenye makosa, bali ya kuweka msingi wa uzazi wa pamoja kwa heshima, kwa upendo, na juu ya yote, kwa busara.
Na kama Bahati alivyosema: “Itakuwa sawa kwa jina la Yesu.”
🔔 Je, unakubaliana na Bahati? Unadhani ni sawa kwa watu maarufu kupeana ushauri wa wazi kwa wenzao hadharani?