News
Rais Ruto amewaongoza wakenya kuadhimisha sherehe za Madaraka za 62

Rais William Ruto amewaongoza wakenya katika kuadhimisha sherehe za Madaraka za 62 tangu taifa lijipatie uhuru.
Katika maadhimisho hayo ambayo yamefanyika katika uwanja wa Raila Odinga kaunti ya Homabay, Rais Ruto amesema taifa limepiga hatua kidemokrasia na maendeleo tangu lijipatie uhuru.
Kiongozi wa taifa ametoa changamoto kwa wakenya kuhakikisha wanaweka kipau mbele masuala ya kutekeleza mabadiliko yanayoleta ufanisi wa Taifa.
Wakenya washeherekea Madaraka, Homabay
Naye Naibu rais Prof Kithure Kindiki amemhakikishia Rais Ruto kuwa ataendelea kushirikiana naye katika kuunganisha taifa huku akimtaja Kinara wa Chama cha ODM Raila Odinga kama kiongozi aliyechangia zaidi mshikamano wa taifa.
Kwa upande wake Kinara wa Chama cha ODM Raila Odinga amemtaka Rais Ruto kuhakikisha serikali inafidia familia za wakenya walipoteza wapendwa wao wakati wa Maandamano ya vijana wa Gen Z mwezi Juni mwaka jana.
Kauli mbiu ya maadhimisho ya sherehe za mwaka huu ni “uchumi wa sanawati na maswala ya bahari”, huku ikilenga kuangazia fursa za kiuchumi zinazotokana na raslimali ya maji.
News
ODM Na PAA, Wafanya mikutano tofauti kuhusu bunge la Kilifi

Mikutano miwili muhimu ya faragha imefanyika Jumatatu Juni 2 2025, kujadilia usimamizi wa vyama vya ODM na PAA ndani na nje ya Bunge la Kaunti ya Kilifi.
Taarifa za kuamika zasema, mikutano hiyo miwili ilikusudia kujadili matukio ya hivi majuzi katika Bunge la Kaunti ya Kilifi na usimamizi wake.
Mazungumzo ya Chama cha ODM yaliofanyika mjini Kilifi na kuhudhuriwa na viongozi wote waliochaguliwa, yalijikita katika tetesi za kumtimua Spika wa Bunge Teddy Mwambire, huku kukiwa na mpasuko baina ya wafuasi wa Spika Teddy Mwambire na kwa upande mwengine, wandani wa Gavana Gideon Mung’aro.
Tofauti kubwa za uongozi wa chama hicho cha ODM zilizuka tangu mchakato wa uchaguzi wa mashinani uliotibuka mwaka uliopita na uhasama huo sasa kuelekezwa ndani ya bunge la Kaunti kutaka kumuondoa Spika mamlakani kupitia kura ya kutokuwa na Imani naye ikidaiwa anahujumu serikali ya Gavana Mung’aro.
Pia mkutano huo ulijadili uwezo Mwakilishi Wadi wa Watamu Ibrahim Matumbo wa kuendelea kuwa kiongozi wa wengi Bungeni.
Kuna habari ambazo hazijathibitishwa kwamba huenda chama cha ODM kinataka kumuondoa Ibrahim Matumbo na wadhfa wake kuchukuliwa na Mwakilishi Wadi ya Ganda Oscar Wanje.
Kwa upande mwengine katika mkutano wa Chama cha PAA uliofanyika katika makao makuu ya chama eneo la Nyali kaunti ya Mombasa, yalijikita katika masuala ya usimamizi ndani ya bunge hilo na kumlenga zaidi kiongozi wa walio wachache katika bunge hilo la kaunti Tom Chengo.
Chengo ambaye pia ni Mwakilishi Wadi wa Tezo- kaunti ya Kilifi, anashtumiwa kwa kuhujumu upinzani ndani ya bunge hilo kutokana na usuhuba wake na Gavana Gideon Mung’aro.
Akizungumza na Cocofm kwa njia ya simu, Katibu mkuu wa Chama cha PAA, amnaye pia ni mbunge wa Ganze Kenneth Kazungu, alikiri kufanyika kwa mkutano huo, siku ya Jumatatu Juni 2, na kwamba mkutano huo ulikuwa kuweka sawa usimamizi na shughuli za chama ndani na nje ya bunge la kaunti.
Katika siku za hivi majuzi bunge hilo limeshuhudiwa mpasuko mkubwa wa kiutawala na kupelekea kutatizwa kwa vikao vya bunge vya kujadili masuala nyeti yanayogusia bejeti na usimamizi wa fedha na utekelezwaji wa miradi katika Wizara ya Afya.
News
Seneta Cherargei, Anataka Waziri Murkomen Kujiuzulu

Baadhi ya viongozi wa kisiasa wamemtaka Waziri wa usalama wa ndani Kipchumba Murkomen kujiuzulu kwa madai kwamba ameshindwa kuimarisha usalama katika maeneo mbalimbali ya taifa.
Wakiongozwa na Seneta wa Nandi Samson Cherargei, Viongozi hao wamesema Waziri Murkomen umeonyesha wazi kutowajibika katika majukumu yake pamoja na kushindwa kupanga kikamilifu usalama wa taifa.
Cherargei amemtaka rais William Ruto kumhamisha Waziri Murkomen katika Wizara hiyo na kumpa wadhfa wa ubalozi katika mataifa ya Pakistan, Gaza ama nchini Tanzania ili kushughulikia masuala ya kidiplomasia.
Cherargei anasema masuala ya usalama huwezi kufananisha na masuala ya barabara kwani usalama wa wananchi ni muhimu zaidi na kutowajibika kwa Waziri Murkomen kumechangia wakaazi wa maeneo ya Kerio Valley kupoteza maisha yao.