National News
Muturi Atemwa Katika Baraza la Mawaziri

Rais William Ruto amefanya mabadiliko kadhaa katika baraza lake la mawaziri na kuwateua watu wengine kushikilia nyadhfa hizo huku aliyekuwa Waziri wa utumishi wa umma nchini Justin Muturi akitemwa nje.
Katika chapisho rasmi la gazeti la serikali ambalo limetiwa saini na mkuu wa utumishi wa umma nchini Felix Koskei, Rais Ruto kwa kuzingatia kipengele cha 152 ibara ya 2 ya katiba, amemteua Hanna Wendot Cheptumo kushikilia Wizara ya Jinsia, utamaduni na turathi.
Mwengine ni Mbunge wa Mbeere Geoffrey Kiringa Ruku ambaye ameteuliwa kushikilia Wizara ya utumishi wa umma nchini, Wizara ambayo ilikuwa ikishikiliwa na Justin Muturi ambaye ametemwa nje ya baraza la mawaziri.
Kiongozi wa taifa, ametumia mamlaka yake ya kikatiba kwa kuzingatia kipengele cha 152 ibara ya 5{a}, na kufanya uhamisho wa mawaziri kutoka Wizara moja hadi nyingine ambapo Waziri wa mazigira na misitu nchini Adan Duale amehamishiwa Wizara ya Afya nchini huku Deborah Barasa ambaye alikuwa akishinikilia Wizara hiyo akihamishiwa Wizara ya Mazingira na misitu.
Uteuzi huo mpya wa mawaziri pamoja na uhamisho, umejiri siku moja tu baada ya Rais Ruto kufanya kikao na viongozi kutoka mlima Kenya pamoja na viongozi wengine kutoka maeneo ya Magharibi mwa Kenya sawa na kikao tofauti na Viongozi wa kidini.
National News
Chonga: Wakenya Wanaosafiri Ughaibuni Kusaka Ajira Hawazingatii Sheria za Leba

Mwenyekiti wa kamati ya Leba katika bunge la kitaifa Ken Chonga amesema baadhi ya wakenya ambao wanasafiri katika mataifa ya miliki za kiarabu kusaka ajira wamekosa kuzingatia sheria za Wizara ya Leba nchini na kuangukia mikononi mwa walaghai.
Chonga amesema ni lazima wakenya hao wachunguze mawakala wanaowasafirisha katika mataifa hayo kama wanatambulika na serikali, ndipo waingie katika mikataba ya uajiri ambayo imezingatia sheria za Leba nchini.
Akizungumza na Wanahabari mjini Kilifi, Chonga ambaye pia ni Mbunge wa Kilifi Kusini amesema ili wakenya waepuke madhila mbalimbali kutoka kwa waajiri wao katika mataifa hayo ni lazima wasafirishwe na mawakala waliosajiliwa na serikali.
Wakati huo huo amesema japo serikali iko mbioni kuhakikisha inawatafutia wakenya kazi katika mataifa ya ughaibuni ni lazima wanaosaka ajira za ughaibuni waingie katika mkataba wa uajiri kabla ya kusafiri nje ya nchi.
National News
Chibule: Visa vya Dhulma za Kijinsi Vimepungua Kilifi

Serikali ya kaunti ya Kilifi imesema visa vya dhulma za kijinsia katika kaunti hiyo vimepungua kwa kiwango kikubwa.
Kulingana na Naibu Gavana wa kaunti hiyo Flora Mbetsa Chibule, visa hivyo viliongezeka zaidi msimu wa maambukizi ya virusi vya Corona, ambapo kaunti ya Kilifi iliorodheswa nafasi ya tatu nchini baada ya kaunti ya Bungoma na Samburu.
Chibule amesema kwa sasa ni asilimia 12.3 pekee ya visa hivyo vilivyoripotiwa tofauti na asilimia 30 wakati wa maambukizi ya Corona, akisisitiza kwamba juhudi hizo zimefanikiwa kupitia ushirikiano wa jamii na wadau mbalimbali.
Kiongozi huyo amedokeza kwamba serikali ya kaunti imetoa mafunzo kwa maafisa wa kutoa ushauri nasaha ili kusaidia kupambana na visa hivyo mashinani, akisema juhudi hizo zitaendelezwa sawa na kudhibiti madhila hayo.
Wakati uo huo ameweka wazi kwamba kaunti hiyo imekamilisha ujenzi wa sehemu salama ya kuwahifadhi watoto wanaopitia dhulma za kijinsia wakati kesi zao zikiendelea Mahakamani.